Kutoka 12 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Pasaka ( Kumb 16.1-8 ) 1 Yawe akamwambia Musa na Haruni, walipokuwa wangali katika inchi ya Misri: 2 “Mwezi huu utakuwa kwenu mwezi wa kwanza wa mwaka. 3 Muwaambie Waisraeli wote pamoja kwamba katika siku ya kumi ya mwezi huu, mutatwaa mwana-kondoo mumoja kwa kila jamaa moja. 4 Kama jamaa moja ni ndogo sana hata isiweze kumaliza kondoo mumoja, itashirikiana na jamaa jirani kadiri ya hesabu ya watu wake. Kisha watachagua nyama ambaye kila mutu ataweza kula. 5 Mwana-kondoo yule asikuwe na kilema chochote, akuwe dume wa mwaka mumoja. Anaweza kuwa mwana-kondoo au mwana-mbuzi. 6 Mutamuweka nyama yule mpaka siku ya kumi na ine ya mwezi huu. Siku hiyo, Waisraeli watawachinja nyama wale wakati wa magaribi. 7 Kisha, watatwaa damu ya wale nyama na kuipakaa juu ya miimo na vizingiti vya kila nyumba watakamokulia nyama wale. 8 Watakula nyama hiyo usiku uleule kisha kuichoma. Wataikula pamoja na mukate usiotiwa chachu na mboga chungu za majani. 9 Imekatazwa kuikula ikiwa mbichi au imetokoteshwa kwa maji, lakini inapaswa kuchomwa yote, pamoja na kichwa, miguu na nyama zake za ndani. 10 Vilevile musiache nyama yoyote mpaka asubui. Nyama yoyote itakayobaki mpaka asubui mutaiteketeza kwa moto. 11 Na hivi ndivyo mutakavyokula nyama yule: mutakuwa tayari kwa kusafiri, na kuvaa viatu na kuwa na fimbo zenu katika mikono. Tena mutamukula kwa haraka. Hiyo ni Pasaka ya Yawe. 12 “Usiku ule, nitapita katika inchi ya Misri na kuwaua wazaliwa wa kwanza wa Misri, watu na nyama. Nitaiazibu miungu yote ya Misri. Mimi ni Yawe. 13 Basi, ile damu itakuwa kitambulisho chenu cha kuonyesha nyumba mutakamokuwa. Nami nitakapoiona ile damu, nitawapita ninyi, hamutapatwa na hasara yoyote wakati nitakapoipiga inchi ya Misri. 14 Vizazi hata vizazi mutakumbuka tukio hilo kwa sikukuu kubwa kwa heshima yangu mimi Yawe. Hilo litakuwa agizo la milele kwenu.” Sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu 15 Yawe akaendelea kusema: “Kwa muda wa siku saba, mutakula mikate isiyotiwa chachu. Siku ya kwanza ya siku hizo saba, mutaondoa chachu katika nyumba zenu. Mutu yeyote akikula kitu kilichotiwa chachu katika muda ule wa siku saba, anapaswa kuondolewa kati ya Waisraeli. 16 Siku ya kwanza na siku ya saba mutakuwa na mukutano mutakatifu. Katika siku hizo mbili hamutaruhusiwa kufanya kazi yoyote isipokuwa kazi ya lazima ya kutayarisha chakula. 17 Mutashika sikukuu hii ya Mikate Isiyotiwa Chachu kama ukumbusho wa siku nilipowatoa ninyi vikundi vya Israeli kutoka Misri. Sikukuu hiyo itashikwa na vizazi vyenu vyote vinavyokuja, kama agizo la milele. 18 Basi, mutakula mikate isiyotiwa chachu kuanzia magaribi ya siku ya kumi na ine ya mwezi wa kwanza, mpaka magaribi ya siku ya makumi mbili na moja ya mwezi uleule wa kwanza. 19 Katika siku hizo saba, musikuwe na chachu yoyote katika nyumba zenu. Mutu yeyote, akuwe mugeni au mwenyeji, akikula kitu kilichotiwa chachu, ataondolewa katika kusanyiko la Waisraeli. 20 Popote pale munapoishi, hamutakula chochote kilichotiwa chachu. Munapaswa kula mikate isiyotiwa chachu.” Pasaka ya kwanza 21 Basi, Musa akawaita wazee wote wa Waisraeli, akawaambia: “Muchague kila mumoja wenu, kulingana na jamaa yake, mwana-kondoo na kumuchinja kwa sikukuu ya Pasaka. 22 Mutatwaa majani ya hisopo na kuyachovya katika damu ndani ya beseni na kupakaa vizingiti na miimo yote miwili ya milango ya nyumba zenu. Mutu yeyote asitoke inje ya nyumba usiku ule mpaka asubui. 23 Maana Yawe atapita kuwaua Wamisri. Lakini atakapoona damu iliyopakwa kwenye vizingiti na miimo ya nyumba zenu, atapita na wala hatamuruhusu mwangamizaji kuingia katika nyumba zenu na kuwaua. 24 Mushike jambo hili ninyi na wazao wenu kama agizo la milele. 25 Mutakapoingia katika inchi ile ambayo Yawe atawapa, kama alivyoahidi, munapaswa kulitimiza. 26 Kila wakati watoto wenu watakapowauliza: ‘Jambo hili lina maana gani?’, 27 ninyi mutawajibu: ‘Hii ni sadaka ya Pasaka kwa Yawe, kwa sababu alipita nyumba za Waisraeli katika inchi ya Misri. Aliwaua Wamisri, lakini sisi hakutuua.’ ” Waisraeli wakainamisha vichwa na kumwabudu Yawe. 28 Kisha Waisraeli wakaenda, wakafanya kama vile walivyoambiwa na Musa na Haruni kulingana na amri ya Yawe. Pigo la kumi: Kuuawa kwa wazaliwa wa kwanza wa Wamisri 29 Katikati ya usiku, Yawe akawaua wazaliwa wa kwanza wote wa Misri. Wote walikufa, tangu muzaliwa wa kwanza wa mufalme wa Misri, murizi wa ufalme, mpaka muzaliwa wa kwanza wa mufungwa katika kifungo. Hata wazaliwa wa kwanza wa nyama nao walikufa. 30 Basi mufalme, watumishi wake na wakaaji wote wa Misri wakaamuka usiku. Kukakuwa kilio kikubwa katika inchi yote ya Misri kwa maana hakukuwa hata nyumba moja ambamo mutu hakukufa. 31 Halafu mufalme wa Misri akaita Musa na Haruni, usiku uleule, akawaambia: “Musimame! Muondoke kati ya watu wangu. Muende, ninyi pamoja na wale Waisraeli, mumutumikie Yawe kama vile mulivyosema. 32 Mutwae makundi yenu ya kondoo na ngombe, muondoke. Muniombee na mimi baraka.” 33 Wamisri wakawasukuma Waisraeli waondoke haraka, wakisema: “Hakika tutakufa sisi wote!” 34 Basi, Waisraeli wakatwaa unga wao uliopondwa mbele haujatiwa chachu na mabakuli yao ya kupondea mikate walikuwa wamezifunga kwa nguo na kubeba juu ya mabega. 35 Waisraeli walikuwa wamekwisha kufanya kama vile Musa alivyowaagiza pale mbele. Waliwaomba Wamisri wawapatie vyombo vya feza na zahabu na nguo. 36 Naye Yawe alikwisha kuwafanya Waisraeli wapate kukubaliwa mbele ya Wamisri, nao Wamisri wakawapa kila kitu walichoomba. Ndivyo Waisraeli walivyonyanganya Wamisri mali yao. Waisraeli wanaondoka Misri 37 Waisraeli waliondoka katika muji wa Ramesesi, wakasafiri kwa miguu kuelekea Sukoti. Walikuwa wanaume yapata elfu mia sita, bila kuhesabu wanawake na watoto. 38 Kulikuwa vilevile kundi la watu wengine waliokwenda pamoja nao na mifugo mingi, kondoo na ngombe. 39 Kwa sababu walikuwa wameondoka Misri kwa haraka, hawakuweza kutayarisha chakula cha safari, ila tu ule unga uliopondwa bila kutiwa chachu. Basi, wakapika mikate isiyotiwa chachu. 40 Waisraeli walikuwa wameishi katika inchi ya Misri kwa muda wa miaka mia ine na makumi tatu. 41 Katika siku ya mwisho ya mwaka wa mia ine na makumi tatu, siku ileile ndipo makabila yote ya Yawe yaliondoka katika inchi ya Misri. 42 Usiku ule ambao Yawe alikesha kwa kuwatoa Waisraeli katika inchi ya Misri, unapaswa kukumbukwa na Waisraeli wote na vizazi vyao vyote, kama usiku wa kukesha kwa heshima ya Yawe. Utaratibu wa Pasaka 43 Yawe akamwambia Musa na Haruni: “Haya ndiyo maagizo juu ya Pasaka. Mugeni yeyote hatashiriki chakula cha Pasaka. 44 Lakini mutumwa yeyote aliyenunuliwa kwa feza, nyuma ya kumutahiri, ataruhusiwa kushiriki. 45 Musafiri yeyote, wala mutumishi yeyote wa mushahara, hatashiriki chakula hicho. 46 Mwana-kondoo wa Pasaka atakuliwa katika nyumba moja. Hamutatoa nyama yoyote inje ya nyumba alimochinjiwa, wala hamutavunja hata mufupa mumoja wa nyama wa Pasaka. 47 Waisraeli wote pamoja watashika sikukuu hiyo. 48 Mugeni yeyote anayeishi kati yenu akipenda kushiriki sikukuu ya Pasaka, anapaswa kwanza kutahiri wanaume wote wa nyumba yake. Halafu atahesabiwa kuwa kama mwenyeji na kuruhusiwa kushiriki. Mwanaume yeyote asiyetahiriwa asishiriki hata kidogo. 49 Sheria zilezile zitaelekea Mwisraeli aliyezaliwa katika inchi na wageni watakaoishi kati yenu.” 50 Waisraeli wote walitii sheria hiyo na kufanya kama vile Yawe alivyowaagiza Musa na Haruni. 51 Siku hiyohiyo Yawe aliwatoa Waisraeli katika inchi ya Misri kwa makundi. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo