Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Kutoka 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Waisraeli wanateswa katika inchi ya Misri

1 Haya ndiyo majina ya wana wa Israeli ambao walikwenda Misri, kila mumoja na jamaa yake:

2 Rubeni, Simeoni, Lawi, Yuda,

3 Isakari, Zebuluni, Benjamina,

4 Dani, Nafutali, Gadi, na Aseri.

5 Wazao wote wa Yakobo walikuwa watu makumi saba. Wakati ule Yosefu alikuwa amekwisha kutangulia kukaa kule Misri.

6 Kisha, Yosefu akakufa, vilevile na wandugu zake na kizazi kile chote.

7 Lakini wazao wa Israeli wakaongezeka sana, wakakuwa wengi na wenye nguvu sana, wakaenea kila pahali katika inchi ya Misri.

8 Basi, kukatokea mufalme mwingine kule Misri ambaye hakumujua Yosefu.

9 Naye akawaambia watu wake: “Muangalie jinsi Waisraeli wanavyokuwa wengi na wenye nguvu kuliko sisi.

10 Ni lazima tutafute werevu wa kuwapunguza na kuzuia wasiongezeke; kama sivyo, vita ikitokea watajiunga na waadui zetu na kutoroka inchi.”

11 Basi, Wamisri wakachagua wakubwa wawasimamie Waisraeli na kuwatesa kwa kazi ngumu. Waisraeli wakafanya kazi ya kumujengea mufalme wa Misri miji ya kuwekea akiba, Pitomu na Ramesesi.

12 Lakini kadiri walivyoteswa ndivyo Waisraeli walivyozidi kuongezeka na kuenea katika inchi. Hivyo Wamisri wakawaogopa sana watu wa Israeli.

13 Basi, Wamisri wakawatumikisha Waisraeli kwa kinguvu.

14 Wakayafanya maisha yao kuwa magumu kwa kazi ngumu ya kutengeneza chokaa na kufyatua matofali, na kazi zote za shamba. Katika kazi zile zote, Waisraeli walitumikishwa kwa kinguvu.

15 Kisha, mufalme wa Misri akawaambia wazalishaji wa Misri, Sifra na Puha, ambao waliwazalisha wanawake Waebrania:

16 “Munapofanya kazi ya kuzalisha wanawake Waebrania, ikiwa mutoto anayezaliwa ni mwanaume, mumwue. Ikiwa ni mwanamuke, mumwache aishi.”

17 Lakini kwa sababu wazalishaji wale walimwogopa Mungu, hawakufanya kama vile walivyoamuriwa na mufalme, lakini waliwaacha watoto wanaume wa Waisraeli waishi.

18 Basi, mufalme akawaita wazalishaji wale, akawauliza: “Kwa nini mumefanya hivyo? Mbona mumewaacha watoto wanaume waishi?”

19 Wao wakamujibu mufalme wa Misri: “Wanawake wa Waebrania si sawa na wanawake Wamisri. Wao ni hodari; mbele muzalishaji hajafika, wao wanakuwa wamekwisha kuzaa.”

20 Basi, Mungu akawajalia mema wazalishaji wale, nao Waisraeli wakazidi kuongezeka na kuwa na nguvu sana.

21 Na kwa sababu wazalishaji wale walimwogopa Mungu, Mungu akawajalia kupata jamaa zao wenyewe.

22 Kisha mufalme wa Misri akawaamuru watu wake wote hivi: “Kila mutoto mwanaume atakayezaliwa kwa Waebrania mumutupe ndani ya muto Nili. Lakini kila mutoto mwanamuke, mumwache aishi.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan