Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Isaya 9 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Watu waliotembea katika giza wameona mwangaza mukubwa. Watu walioishi katika inchi ya giza kubwa, sasa mwangaza umewaangazia.

2 Wewe, ee Mungu, umeongoza taifa, umezidisha furaha yake. Watu wanafurahi mbele yako wana furaha kama kwa wakati wa mavuno, kama vile wanaogawanya vitu walivyonyanganya wanavyofurahi.

3 Maana miti mizito waliyobeba, nira walizokuwa wamefungwa, na fimbo ya wasimamizi, umezivunjavunja kama wakati wa Wamidiani.

4 Viatu vyote vya washambulizi katika vita na nguo zote zenye kujaa damu vitateketezwa kama kuni za kuwasha moto.

5 Maana mutoto amezaliwa kwa ajili yetu, tumepewa mutoto mwanaume. Naye atapewa mamlaka ya kutawala. Ataitwa: “Mushauri wa Ajabu”, “Mungu Mwenye Nguvu”, “Baba wa Milele”, “Mufalme wa Amani”.

6 Utawala wake utastawi siku zote, amani ya ufalme wake haitakoma. Atakamata madaraka ya mufalme Daudi na kutawala juu ya ufalme wake; ataustawisha na kuuimarisha kwa kufuata sheria ya Mungu na kutenda kwa haki tangu sasa na hata milele. Yawe wa majeshi atafanya mambo hayo.


Azabu ya Waisraeli

7 Yawe ametoa neno juu ya Yakobo nalo litamupata Israeli.

8 Watu wote watatambua, ukoo wote wa Efuraimu na wakaaji wa Samaria. Kwa kiburi na majivuno wanasema:

9 Kuta za matofali zimeanguka lakini sisi tutazijenga kwa mawe yaliyochongwa! Nyumba za nguzo za mikuyu zimeharibiwa lakini pahali pake tutajenga za mierezi.

10 Basi, Yawe atawaletea wapinzani na kuwachochea waadui zao.

11 Waasuria kwa upande wa mashariki, Wafilistini kwa upande wa magaribi, wamepanua vinywa vyao kwa kuimeza Israeli. Hata hivyo, hasira yake haijatulia, angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu.

12 Ingawa aliwaazibu watu, hawakumurudilia Yawe wa majeshi.

13 Yawe atakata katika Israeli kichwa na mukia, tawi la mingazi na nyasi, kwa muda wa siku moja tu.

14 Kichwa ni wazee na waheshimiwa, mukia ni manabii wanaofundisha uongo.

15 Wale wanaoongoza watu hawa wamewapotosha, na hao wanaoongozwa nao wamepotoka.

16 Kwa hiyo, Yawe hawahurumii vijana wao, hana huruma juu ya wayatima na wajane wao; maana hakuna hata mumoja anayemufuata, kila mutu anasema upumbafu. Hata hivyo, hasira yake haijatulia, angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu.

17 Uovu unawaka kama moto unaoteketeza michongoma na miiba; unawaka kama moto katika pori, na kutoa moshi muzito unaopanda juu katika anga.

18 Kwa kasirani ya Yawe wa majeshi inchi imechomwa moto, na watu ni kama kuni za kuuwasha. Hakuna mutu anayemuhurumia ndugu yake;

19 wananyanganya upande mumoja na hawatosheki; wanakula upande mwingine lakini hawashibi. Kila mumoja anamushambulia mwenzake.

20 Manase anashambulia Efuraimu, Efuraimu anashambulia Manase na wote wawili wanashambulia Yuda. Hata hivyo, hasira ya Yawe haijatulia, angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan