Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Isaya 59 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Nabii analaani zambi za watu

1 Musifikiri kwamba mukono wa Mungu ni mufupi, hata asiweze kuwaokoa, au kwamba masikio yake yamefungana, hata asiweze kuwasikiliza ninyi.

2 Zambi zenu ndizo zinazowatenga na Mungu wenu, zambi zenu zimemufanya ajifiche mbali nanyi hata asiweze kuwasikiliza ninyi.

3 Maana mikono yenu imechafuka kwa damu, na vidole vyenu kwa matendo maovu. Midomo yenu imesema uongo, na ndimi zenu zinasema uovu.

4 Hakuna anayemushitaki mwenzake kwa haki, wala anayejitetea kwa ukweli. Munategemea mambo ya bure; munasema uongo. Munafanya mipango ya kuleta hasara na kuzaa uovu.

5 Munatoa mayai ya nyoka yenye sumu, munafuma wavu wa buibui. Anayekula mayai yenu anakufa, na yakipasuliwa, nyoka anatokea ndani yake.

6 Wavu wenu haufai kama nguo, watu hawawezi kujifunikia munachofuma. Kazi zenu ni kazi za uovu, matendo yenu yote ni mateso makali.

7 Muko mbio kutenda maovu, muko wepesi kumwanga damu isiyokuwa na kosa. Mawazo yenu ni mawazo ya uovu, popote munapokwenda munaacha ukiwa na uharibifu.

8 Njia ya amani hamuijui hata kidogo; hamufuati sheria ya Mungu. Mumejifanyia njia potovu, yeyote anayepitia humo hapati amani.


Watu wanatambua zambi yao

9 Kwa hiyo, kufuata sheria ya Mungu kuko mbali nasi, haki haifiki kwetu. Tulitazamia kupata mwangaza, kumbe ni giza tupu; tulingojea mwangaza, lakini tunatembea katika giza.

10 Kama vipofu tunapapasapapasa ukuta; tunasitasita kama watu wasiokuwa na macho. Tunajikwaa muchana kati, sawa vile ni usiku; kati ya wenye afya, sisi ni kama wafu.

11 Tunanguruma kama dubu, tunaomboleza kama njiwa. Tunatazamia watu wanaofuata sheria ya Mungu, lakini hakuna, tunatazamia wokovu, lakini uko mbali nasi.

12 Makosa yetu mbele yako ni mengi sana, zambi zetu zinashuhudia juu yetu. Kweli, makosa yetu yanaandamana nasi, tunayajua maovu yetu.

13 Tumekuasi na kukukana, ee Yawe, tumekataa kukufuata, ewe Mungu wetu. Tunasema maneno ya kutesa na uasi, katika mioyo yetu tunatunga na kutoa maneno ya uongo.

14 Sheria ya Mungu imewekwa pembeni, haki iko mbali; ukweli unakanyagwa katika tribinali, usawa hauwezi kuingia humo.

15 Ukweli umekosekana, naye anayeacha uovu ananyanganywa. Mungu aliona mambo hayo. Alichukizwa kwamba watu hawafuati sheria yake.


Mungu anajitayarisha kuwakomboa watu wake

16 Aliona kwamba hakuna mutu aliyejali, akashangaa kwamba hakuna aliyeingilia kati. Basi akaamua kunyoosha mukono wake mwenyewe, haki yake ikamusaidia.

17 Alivaa haki kama vile nguo ya kujikinga kifua, na wokovu kama kofia ya chuma juu ya kichwa. Alivaa nguo ya kulipiza kisasi, na kujifunika na kanzu ya wivu.

18 Atawaazibu waadui kadiri ya matendo yao, kasirani yake na kisasi vitawapata waadui zake; atawaazibu hata wakaaji wa inchi za mbali.

19 Toka magaribi mpaka mashariki, kila mutu atamwogopa Yawe na kutambua utukufu wake. Maana atakuja kama muto wenye kuporomoka mbio, muto unaosukumwa kwa upepo wa Yawe.

20 Naye atakuja katika Sayuni kama Mukombozi, Mukombozi wa wazao wa Yakobo ambao wataachana na makosa yao. –Ni ujumbe wa Yawe.

21 Yawe anasema: Mimi ninafanya nanyi agano hili: Roho wangu anayekuwa juu yenu, maneno niliyoyaweka katika kinywa chenu, hayataondoka kwenu hata kidogo, wala kwa watoto na wajukuu wenu, tangu sasa na hata milele.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan