Isaya 48 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu anatangaza matukio mapya 1 Musikilize, enyi watu wa Yakobo, enyi munaojulikana kwa jina la Israeli, ninyi munaokuwa wa uzao wa Yuda. Ninyi munaapa kwa jina la Yawe, na kudai kwamba munamwabudu Mungu wa Israeli; lakini hayo si ukweli wala sawa. 2 Ninyi munaona utukufu kujiita watu wa muji mutakatifu, na kujidai kumutegemea Mungu wa Israeli, ambaye jina lake ni Yawe wa majeshi. 3 Nilitangaza zamani matukio ya mbele, niliyatangaza mimi mwenyewe na kuyafanya yajulikane kwenu. Mara moja nikaanza kuyatimiza, nayo yakapata kutukia. 4 Lakini nilikujua wewe kuwa na moyo mugumu; kichwa kigumu kama chuma, uso wako kama shaba. 5 Kwa hiyo nilikutangazia mambo yale tangu zamani, mbele hayajatukia, mimi nilikujulisha, kusudi usiseme: Ni sanamu yangu iliyotenda mambo hayo, sanamu zangu za chuma ndizo ziliyaagiza. 6 Wewe uliyasikia na sasa unayaona yote. Kwa nini hauwezi kuyakubali? Tangu sasa nitakujulisha mambo mapya; mambo yaliyofichwa ambayo haukuyajua. 7 Mambo hayo yanatukia sasa; haukupata kuyasikia mbele ya siku ya leo, hivyo hauwezi kusema: Aa! Nilikwisha kuyajua. 8 Haujapata kuyasikia wala kuyajua hata kidogo; tangu zamani masikio yako hayakuyasikia. Nilijua kwamba wewe ni mudanganyifu, na kwamba wewe ni mwasi tangu kuzaliwa. 9 Kwa heshima ya jina langu, ninatuliza hasira yangu; kwa ajili ya heshima yangu, ninajizuiza kusudi nisikuangamize. 10 Mimi nimekusafisha lakini si kama feza katika furu. Nimewapima katika furu ya taabu. 11 Ninafanya hivyo kwa ajili yangu mwenyewe. Kwa nini jina langu lizarauliwe? Siwezi kumupatia mwingine utukufu wangu! Kiro, muchaguliwa wa Yawe 12 Unisikilize ee taifa la Yakobo, unisikilize ee Israeli niliyekuita. Mimi ndiye. Mimi ni wa kwanza na wa mwisho. 13 Kwa mukono wangu niliuweka musingi wa dunia, mimi mwenyewe nilizitandaza mbingu. Nikiziita mbingu na dunia, zinasimama haraka mbele yangu. 14 Mukusanyike wote musikilize! Nani kati yenu alitabiri vitu hivi? Yule ambaye Yawe anamupenda atatimiza mapenzi yake juu ya Babeli, atawashambulia Wakaldea. 15 Mimi –ni mimi!– nimesema na kumwita; nimemuleta, naye atafanikiwa katika mupango wake. 16 Musogee karibu nami musikie jambo hili: Tangu mwanzo mimi sikusema kwa siri, tangu mambo hayo yaanze kutendeka, nimekuwa pale. Sasa, Bwana wetu Yawe amenituma, na kunipa nguvu ya Roho wake. Mupango wa Mungu kwa watu wake 17 Yawe, Mutakatifu wa Israeli, Mukombozi wako, anasema hivi: Mimi ndiye Yawe, Mungu wako; ninayekufundisha kwa faida yako na kukuongoza katika njia unayotakiwa kwenda. 18 Ingekuwa heri ungalizitii amri zangu! Halafu baraka zingekutiririkia kama muto, ungefanikiwa kwa wingi kama mawimbi ya bahari. 19 Wazao wako wangekuwa wengi kama muchanga, kama chembe za muchanga. Jina lao lisingalisahauliwa hata kidogo, wala halingalifutwa mbele yangu. 20 Sasa, muondoke Babeli! Mukimbie kutoka kwa Wakaldea! Mutangaze jambo hili kwa sauti za shangwe. Mueneze habari zake kila pahali katika dunia. Museme: Yawe amekomboa taifa la mutumishi wake Yakobo. 21 Alipowaongoza katika jangwa hawakuona kiu, aliwatiririshia maji kutoka katika jiwe, alipasua jiwe maji yakabubujika. 22 Lakini Yawe anasema hivi: Hakuna amani kwa watu waovu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo