Isaya 45 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yawe anamuchagua mufalme Kiro 1 Yawe anasema hivi kwa Kiro, muchaguliwa wake: Nilikuchagua kuwa mufalme kwa kunitumikia. Ninaimarisha nguvu yako kusudi uyashinde mataifa mbele yako, na kuzivunja nguvu za wafalme. Mimi ninafungua milango ya muji mbele yako, na hakuna mulango utakaofungwa. 2 Mimi nitakutangulia, na kuisawanisha milima mbele yako. Nitaivunjavunja milango ya shaba, na kuvikatakata vifungio vyake vya chuma. 3 Nitakupa akiba zilizofichwa na mali inayokuwa pahali pa siri, upate kutambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wa Israeli, ninayekuita kwa jina lako. 4 Kwa ajili ya mutumishi wangu Yakobo, muchaguliwa wangu Israeli, nimekuita kwa jina lako; nimekupa jina la heshima ingawa wewe haunijui. 5 Mimi ni Yawe, wala hakuna mwingine; hakuna Mungu mwingine lakini mimi. Ninakuimarisha ingawa wewe haunijui, 6 kusudi watu wote, toka mashariki mpaka magaribi, wajue kwamba hakuna Mungu mwingine isipokuwa mimi tu. Mimi ni Yawe na hakuna mwingine. 7 Mimi ninafanya mwangaza na kuumba giza; ninaleta uheri na kusababisha hasara. Mimi Yawe ninatenda vitu hivi vyote. 8 Enyi mbingu, munyeshe umande kutoka kule juu, mawingu yatiririshe ushindi; dunia ifuguke, ichipushe wokovu, na kuotesha haki vilevile! Mimi, Yawe nimefanya hayo. Uwezo mukubwa wa Mungu 9 Ole kwake mutu anayebishana na Muumba wake: chombo cha udongo kubishana na mufinyanzi wake! Udongo unamwuliza anayeufinyanga: Unatengeneza nini hapa? au kumwambia: Kazi yako si kamili! 10 Ole kwake mutu anayemwambia baba: Umezaa nini? au anayemwambia mama: Umeleta nini katika dunia? 11 Yawe, Mutakatifu wa Israeli, Mungu, Muumba wa Israeli anasema hivi: Munataka kuniuliza juu ya watoto wangu, au kuniamuru juu ya kazi zangu mwenyewe? 12 Ni mimi niliyeifanya dunia, na kuumba mwanadamu anayeishi humo. Mikono yangu ndiyo iliyozitandaza mbingu, na kundi lote la nyota liko kwa amri yangu. 13 Ni mimi niliyemwamuru Kiro akuje, atimize mapenzi yangu. Nitazifanikisha njia zake zote. Ataujenga upya muji wangu Yerusalema, na kuwapa uhuru watu wangu wanaokuwa katika uhamisho, bila kutaka malipo wala zawadi. –Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. 14 Yawe anasema hivi: Utajiri wa Misri na faida ya uchuuzi za Kushi, pamoja na za watu wa Seba, wale watu warefu sana, zitakuja kwako mwenyewe wewe taifa la Israeli, zote zitakuwa mali yako. Watu hao watakufuata wakifungwa minyororo; watainama mbele yako na kukusihi wakisema: Kwako kuna Mungu wa kweli, wala hakuna Mungu mwingine lakini yeye. 15 Kweli wewe ni Mungu mwenye kufichama, Mungu wa Israeli, Mungu mwokozi. 16 Watengenezaji wa sanamu watapata haya na kuzarauliwa, wote pamoja watafezeheka. 17 Lakini taifa la Israeli litaokolewa na Yawe, litapata wokovu wa milele. Halitapata haya wala kuzarauliwa milele. 18 Hivi ndivyo anavyosema Yawe aliyeumba mbingu, ndiye Mungu aliyeipa dunia umbo na kuifanya na kuiimarisha. Hakuiumba kusudi ibaki ukiwa, lakini aliipa umbo kusudi iikaliwe na viumbe vyake: Mimi ni Yawe, wala hakuna mwingine. 19 Mimi sikusema kwa siri, wala katika inchi yenye giza. Mimi sikuwaambia wazao wa Yakobo wanitafute pahali kusipokuwa kitu. Mimi Yawe ninasema ukweli, maneno yangu ni ya kuaminika. 20 Enyi watu wa mataifa muliobaki, mukusanyike pamoja mukuje! Ninyi mumekosa akili: ninyi munabeba sanamu za miti na kumwomba mungu asiyeweza kuokoa watu. 21 Mutangaze na kusema habari zenu. Mufanye shauri pamoja! Ni nani aliyetangaza zamani matukio ya sasa? Ni nani aliyesema mambo haya zamani? Haikukuwa mimi Yawe? Hakuna Mungu mwingine isipokuwa mimi! Mimi ni Mungu wa haki na mwokozi; hakuna mwingine isipokuwa mimi. 22 Munigeukie mimi mupate kuokolewa, popote munapokuwa katika dunia. Maana mimi ni Mungu, wala hakuna mwingine. 23 Mimi nimeapa kwa nafsi yangu, ninachosema ni ukweli, neno langu halitarudi nyuma: kila mwanadamu atanipigia magoti, kila mutu atafanya kiapo. 24 Watasema juu yangu: Haki na nguvu viko kwa Yawe peke yake. Wote waliomukasirikia Yawe watakuja kwake na haya. 25 Lakini wazao wa Israeli watapata ushindi toka kwa Yawe na kufurahi. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo