Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Isaya 44 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yawe ndiye Mungu pekee

1 Sikiliza, ewe Israeli, mutumishi wangu; sikiliza, enyi wazao wa Yakobo, muchaguliwa wangu.

2 Mimi, Yawe Muumba wako, niliyekutengeza tangia tumbo la mama yako, ninakuja kukusaidia wewe. Mimi Yawe ninasema hivi: Musiogope, enyi wazao wa Yakobo, mutumishi wangu, usiogope, ewe Yeshuruni, muchaguliwa wangu.

3 Nitaimwangilia maji inchi yenye kiu, na kutiririsha muto katika inchi iliyokauka. Nitajaza roho wangu juu ya wazao wako, nitawamwangia watoto wako baraka yangu.

4 Watachipuka kama nyasi penye maji mengi, kama majani kandokando ya vijito.

5 Mumoja atasema: “Mimi ni wa Yawe”, mwingine atajiita kwa jina la Yakobo, mwingine ataandika juu ya mukono wake: “Wa Yawe”, na kujitambulisha kwa jina la Israeli.

6 Yawe, Mufalme na Mukombozi wa Israeli, Yawe wa majeshi anasema hivi: Mimi ni wa kwanza na wa mwisho; hakuna mungu mwingine isipokuwa mimi.

7 Ni nani mungu anayekuwa kama mimi? Muache atangaze na kusema wazi mbele yangu. Nani alitangaza hapo zamani mambo ambayo yatatukia? Watuambie yale ambayo bado yatatokea.

8 Enyi watu wangu, musiogope wala musikuwe na hofu, Sikuwaambia tangu zamani mambo yatakayotokea? Ninyi ni washuhuda wangu. Kuna mungu mwingine isipokuwa mimi? Kuna mwenye nguvu mwingine? Yule simujui!


Upumbafu wa kuabudu sanamu

9 Watu wote wanaotengeneza sanamu za miungu ni bure kabisa; na vitu hivyo wanavyovifurahia haviwafalii kitu chochote. Wanaoshuhudia hiyo miungu ya uongo ni vipofu na wajinga. Kwa hiyo hao watafezeheshwa!


Wimbo wa sifa

10 Kuna faida gani kwa mutu kujitengenezea mungu au sanamu ya miungu?

11 Hakika wote wanaoshirikiana na sanamu watapata haya, tena hao wafundi wa sanamu ni wanadamu tu. Basi, wakutane wote, wajitokeze, nao wataogopa na kufezeheka.

12 Mufuaji wa vyuma anatwaa kipande cha chuma, anakiyeyusha kwa moto na kufua sanamu. Anakipondaponda na nyundo kusudi akipatie umbo kwa mikono yake yenye nguvu. Wakati wote huo yeye anasikia njaa na kuchoka; anasikia kiu na nguvu kuregea.

13 Vilevile muchoraji wa miti anafanya vipimo vyake kwa kamba, anachapa kitambulisho chake, kisha anatumia vifaa vyake kwa kuchonga. Halafu anatengeneza sanamu na kuipatia umbo la mutu na sura ya kupendeza; kisha anaweka sanamu hiyo ya mungu pahali pake pa pekee.

14 Mutu anakata muti wa mwerezi kusudi autumie, au anachagua muvula au mwalo. Anauacha ukomae kati ya miti ya pori. Au anaupanda mwerezi na mvua inaustawisha.

15 Sehemu ya muti huo itatumiwa kama kuni; mutu anaota moto wake na kuchoma mikate yake juu yake. Sehemu nyingine ya muti huohuo, mutu anajichongea mungu na kumwabudu; anajitengenezea sanamu ya mungu na kupiga magoti mbele yake.

16 Kisha anatwaa kuni zake, anakonga nazo moto, anachoma nyama juu yake, anaikula, na kushiba. Halafu anakaa pale akiota moto na kusema: Aa, kweli nimepata joto! Huo ndio moto!

17 Sehemu iliyobaki ya muti huohuo, anajichongea nayo mungu, anajifanyia sanamu yake, kisha anapiga magoti mbele yake na kuiabudu. Wanaomba mbele yake wakisema: Wewe ni mungu wangu, uniokoe!

18 Watu hao hawajui wala hawaelewi kitu chochote. Wamefungwa macho wasipate kuona na akili wasipate kufahamu.

19 Hakuna anayeweza kuwaza au kuwa na akili na kufikiri na kusema: Kipande cha muti huo nilikikonga moto; tena nikachoma mikate juu ya makaa yake, nikachoma nyama, nikakula. Basi, sehemu iliyobaki namna gani nitatengeneza nayo sanamu ambayo ni chukizo na kuabudu hicho kipande cha muti?

20 Hapana! Mawazo yao yameambatana na hicho ambacho ni majivu tu! Mutu huyo amepotoka hata hawezi kujiokoa mwenyewe na kusema: Kweli, hiki ninachokuwa nacho katika mukono wangu ni udanganyifu mutupu!


Yawe, hatawasahau Waisraeli

21 Yawe anasema hivi: Ewe Israeli, watu wa Yakobo, kumbuka kwamba wewe ni mutumishi wangu. Nilikuumba kusudi ukuwe mutumishi wangu, nami sitakusahau hata kidogo.

22 Nimezimisha makosa yako nayo yametoweka kama mawingu, nimefuta zambi zako, nazo zimepotea kama kunguku. Urudi kwangu maana mimi nimekukomboa.

23 Muimbe kwa furaha enyi mbingu, kwa sababu ya yale Yawe aliyotenda. Mupige kelele enyi vilindi vya dunia! Mupige vigelegele enyi milima! Enyi mapori na miti yote inayokuwa ndani yake, mushangilie. Maana Yawe amewakomboa wazao wa Yakobo, naye atatukuzwa katika inchi ya Israeli.

24 Yawe, Mukombozi wako, aliyekuumba tangu katika tumbo, anasema hivi: Mimi ndiye Yawe niliyeumba vitu vyote. Mimi peke yangu nilizitandaza mbingu, niliiumba dunia kwa nguvu yangu mwenyewe!

25 Mimi ninavuruga maono ya manabii wa uongo na ninapoteza akili za waaguzi. Mimi ninayapinga maneno ya wenye hekima na kufanya elimu yao kuwa upumbafu.

26 Lakini ninahakikisha ujumbe wa mutumishi wangu, na kukamilisha mipango ya wajumbe wangu. Mimi ndiye ninayesema juu ya Yerusalema: Wewe Yerusalema, watu watakaa ndani yako tena. Na juu ya miji ya Yuda: Ninyi mutajengwa tena: mabomoko yenu yatatengenezwa tena.

27 Mimi ndiye ninayeviamuru vilindi: Mukauke, nitakausha mito yenu.

28 Ndimi ninasema juu ya mufalme Kiro: Ni muchungaji niliyemuchagua kwa ajili yangu. Yeye atatimiza mipango yangu yote. Ndimi ninayesema juu ya Yerusalema: Wewe Yerusalema utajengwa tena upya; na juu ya hekalu: Musingi wako utawekwa tena.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan