Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Isaya 40 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Tumaini la kukombolewa kwa Waisraeli

1 Mungu wenu anasema hivi: Muwafariji watu wangu. Muende kuwafariji.

2 Museme na watu wa Yerusalema kwa upole, muwaambie kwamba utumwa wao umekwisha, wamesamehewa uovu wao. Yawe amewaazibu mara mbili kwa sababu ya zambi zao zote.

3 Sauti inatangaza katika jangwa: Mutengenezee Yawe njia, munyooshe barabara kubwa kwa ajili ya Mungu wetu.

4 Kila bonde litafunikwa, kila mulima na kilima vitasawanishwa; njia zenye lukumba zitanyooshwa, nazo zenye mashimo zitalainishwa.

5 Kisha utukufu wa Yawe utafunuliwa, na watu wote pamoja watauona. Maneno haya yanatoka katika kinywa cha Yawe.

6 Sauti inasema: Tangaza! Nami nikauliza: Nitangaze nini? Naye: Tangaza: wanadamu wote ni kama majani; usitawi wao ni kama maua ya shamba.

7 Majani yananyauka na maua yanafifia, Yawe anapovumisha upepo juu yake. Hakika wanadamu ni kama majani.

8 Majani yananyauka na maua yanafifia, lakini neno la Mungu wetu linadumu milele.

9 Kwenda juu ya mulima murefu, ewe Sayuni, utangaze habari njema. Lalamika kwa nguvu, ewe Yerusalema, utangaze habari njema. Lalamika bila kuogopa. Uambie miji ya Yuda: Muangalie: Mungu wenu!

10 Bwana wetu Yawe anakuja na nguvu, kwa mukono wake anatawala. Yeye anakuja na mapato yake, anafika na mushahara wake.

11 Atachunga kundi lake kama muchungaji, atawakusanya wana-kondoo katika mikono yake, atawabeba kwa kifua chake, na atawaongoza polepole kondoo wanaonyonyesha.


Mungu wa Israeli hana kilinganisho

12 Ni nani anayeweza kupima maji ya bahari katika kitanga cha mukono wake, na kuzipima mbingu kwa mikono yake? Ni nani anayeweza kuutia udongo wa dunia katika kikombe; kuipima milima kwa mizani au vilima kwa kipimo cha uzito?

13 Nani anayeweza kuiongoza akili ya Yawe, au kuwa mushauri wake na kumufundisha?

14 Yawe alitaka shauri toka kwa nani, halafu akapata kuwa mwenye akili? Nani aliyemufundisha kuhukumu kwa haki? Nani aliyemufundisha maarifa, na kumwonyesha namna ya kuwa na akili?

15 Kwake mataifa ni kama tone la maji katika mbeketi, ni kama mavumbi juu ya kilo. Kwake visanga ni vyepesi kama mavumbi laini.

16 Kuni zote za Lebanoni na nyama wake wote havitoshi kwa sadaka ya kuteketezwa mbele yake.

17 Mataifa yote si kitu mbele yake; kwake ni vitu vya ovyo na bure kabisa.

18 Mutamulinganisha Mungu na nini basi, au ni kitu gani cha kumufananisha nacho?

19 Anafanana na sanamu? Hiyo, fundi anaichonga, mufuaji wa zahabu anaipakaa zahabu, na kuitengenezea mukufu wa feza!

20 Au ni sanamu ya muti mugumu? Hiyo ni kuni mutu anayochagua, akamutafuta fundi anayeelewa kazi, naye anamuchongea sanamu imara!

21 Ninyi hamujui bado? Hamujapata kusikia? Hamukuambiwa tangu mwanzo? Hamujafahamu mwanzo wa dunia?

22 Dunia iliumbwa na yule anayeikaa juu ya mbingu; kutoka huko wakaaji wa dunia ni kama mapanzi! Yeye ametandika mbingu kama pazia, na kuzikunjua kama hema la kuishi ndani yake.

23 Yeye anawashusha wakubwa wenye nguvu, anawafanya watawala wa dunia kuwa si kitu.

24 Mara tu wanaposimikwa na kuanza kuota, hata mbele hawajatoa mizizi kama miti katika udongo, Yawe akiwapulizia wananyauka, upepo mukali unawapeperusha kama makapi!

25 Mungu Mutakatifu anauliza hivi: Basi, mutanilinganisha na nani? Kuna mutu anayeweza kuwa sawasawa mimi?

26 Muinue macho yenu juu mbinguni! Ni nani aliyeziumba nyota hizo? Ni yule anayeziongoza kama jeshi lake, anayeijua hesabu yake yote, anayeziita kila moja kwa jina lake. Kwa sababu yeye ni mwenye nguvu nyingi, hakuna hata moja inayokosekana.

27 Enyi watu wa Israeli wazao wa Yakobo, kwa nini munalalamika na kusema: Yawe hatujali sisi! Mungu wetu hajali haki yetu!

28 Ninyi hamujui bado? Hamujapata kusikia? Yawe ndiye Mungu wa milele; yeye ndiye Muumba wa kila kitu katika dunia. Yeye haregei hata kidogo wala kuchoka. Maarifa yake hayachunguziki.

29 Yeye anawapatia nguvu wanaokuwa zaifu, anawaongezea nguvu wale wanaoregea.

30 Hata vijana wataregea na kuchoka; kweli washujaa wataanguka kwa muchoko.

31 Lakini wote wanaomutumainia Yawe, watapata nguvu mupya. Watapanda juu kwa mabawa kama tai, watakimbia bila kuchoka, watatembea bila kuregea.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan