Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Isaya 34 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mungu atawaazibu waadui zake

1 Mujongee musikilize enyi mataifa, musikilize enyi watu. Sikiliza, ee dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake, ulimwengu na vyote vinavyotoka humo!

2 Yawe amekasirikia mataifa yote, amekasirikia majeshi yao yote. Ameyapangia mwisho wao, ameyatoa yaangamizwe.

3 Maiti zao zitatupwa inje; harufu ya maiti zao itasambaa; damu yao itatiririka juu ya milima.

4 Jeshi lote la anga litaharibika, anga zitakunjamana kama karatasi. Jeshi lake lote litanyauka, kama vile majani ya mizabibu au mitini yanavyonyauka.

5 Upanga wa Mungu uko tayari juu mbinguni. Angalia, unashuka kuwaazibu Waedomu, watu ambao ameamua kuwaangamiza.

6 Upanga utajaa damu na mafuta: damu ya kondoo na mbuzi, na mafuta ya figo za kondoo dume. Maana Yawe ana sadaka huko Bosira, kutakuwa mauaji makubwa katika inchi ya Edomu.

7 Mbogo wataangamizwa pamoja nao, wana-ngombe pamoja na ngombe dume. Inchi italewa na damu, udongo utashiba kwa mafuta yao.

8 Maana Yawe yuko na siku ya kulipiza kisasi; mwaka wa kulipiza waadui za Sayuni.

9 Vijito vya Edomu vitatiririsha kabulimbo, udongo wake utakuwa kiberiti; inchi yake itakuwa kabulimbo inayowaka.

10 Itawaka usiku na muchana bila kuzimika, moshi wake utapanda juu milele. Inchi itakuwa jangwa siku zote, hakuna atakayepitia huko milele.

11 Itakuwa makao ya ndege za jangwa: kozi, bundi na kibombobombo. Yawe atawaletea muvurugano, na timazi la fujo kwa wakubwa wake.

12 Inchi itaitwa Inchi bila Mufalme; wakubwa wake wote wametoweka.

13 Miiba itaota katika pango zake, miiba na michongoma ndani ya kuta zake. Itakuwa makao ya imbwa wa pori, nafasi ya mbuni.

14 Paka wa pori na fisi watakuwa humo, mapepo wataitana humo; sulukutu atatulia humo na kupata nafasi ya kupumzika.

15 Humo bundi watataga mayai na kuyaatamia, watatotoa vitoto na kuviweka chini ya kivuli chao. Humo tai watakutanana, kila mumoja na mwenzake.

16 Musome katika kitabu cha Yawe: Hakuna hata kiumbe kimoja kitakachokosekana, kila kimoja kitakuwa na mwenzake. Maana kinywa cha Yawe kimeamuru hivyo. Roho yake itawakusanya hao wote.

17 Yawe amepanga sehemu ya kila mumoja wao, ametumia kamba kuwapimia inchi hiyo; watairizi milele na milele, wataishi mule kizazi hata kizazi.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan