Isaya 33 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Hasara kwa mwangamizaji 1 Ole kwako! Unaangamiza ingawa hauangamizwi. Unadanganya ingawa haudanganywi. Utakapokwisha kuangamiza, wewe utaangamizwa! Utakapomaliza kudanganya, wewe utadanganywa. 2 Ee Yawe, utuonee huruma, kwako tumeliweka tumaini letu. Ukuwe kikingio chetu kila siku, mwokozi wetu wakati wa taabu. 3 Kwa kishindo cha sauti yako watu wanakimbia; unaposimama tu, mataifa yanatawanyika. 4 Waadui zao wanakusanya vitu walivyonyanganya, wanavirukia kama mapanzi. 5 Yawe ametukuzwa, yeye anaishi juu mbinguni. Ameujaza Sayuni usawa na haki. 6 Enyi watu wa Yerusalema, Yawe atawajalia usalama, atawaokoa na kuwapa hekima na maarifa. Akiba yenu kubwa ni kumwogopa Yawe. 7 Muangalie, washujaa wao wanalia, wajumbe wa amani wanaomboleza. 8 Barabara kubwa zimebaki tupu; hakuna anayesafiri kupitia ndani yao. Mapatano yanavunjwa ovyo, washuhuda wanazarauliwa. Hakuna anayejali tena maisha ya wanadamu. 9 Inchi inaomboleza na kunyauka; pori ya Lebanoni imekauka, bonde zuri la Saroni limekuwa jangwa, kule Basani na mulima Karmeli majani yote yamekauka. Yawe anawaonya waadui zake 10 Yawe anasema hivi: Sasa mimi nitasimama; sasa nitajiweka tayari; sasa mimi nitatukuzwa. 11 Mipango yenu yote ni kama maganda, na matokeo yake ni takataka tupu. Pumzi yangu itawaangamiza kama moto. 12 Watu watakuwa kama wamechomwa kuwa majivu, kama miiba iliyokatwa na kuteketezwa katika moto. 13 Musikilize mambo muliyofanya, enyi munaokuwa mbali; nanyi munaokuwa karibu, mutambue uwezo wangu. 14 Wenye zambi katika Sayuni wanaogopa, wasiomwamini Mungu wanatetemeka na kusema: Nani anayeweza kuvumilia moto huu mukali? Nani anayeweza kuvumilia ndimi za moto usiozimika? 15 Ni mutu anayekuwa hivi: anaishi kwa haki na kusema kwa usawa, anazarau kabisa utajiri wa unyanganyi, anakataa kupokea kituliro, hakubali hata kidogo kusikia mipango ya mauaji, wala hakubali macho yake yaone maovu. 16 Mutu wa namna hiyo anaishi kwenye nafasi ya juu, pahali salama, penye pango na mawe makubwa; atapewa chakula chake siku zote, na maji yake ya kunywa hayatakosekana. Wakati muzuri unaokuja 17 Mutaweza kumwona mufalme katika utukufu wake, mutaiona inchi anayotawala, kubwa na pana. 18 Mutakumbuka kitisho kilichopita na kujiuliza: Wako wapi wale waliokadirisha na kuchunguza kodi? Wako wapi wale waliopeleleza ugumu wa kuta zetu? 19 Hamutawaona tena watu wale wenye kiburi, wanaozungumuza luga isiyoeleweka. 20 Muangalie Sayuni tunamofanyia sikukuu zetu; muangalie Yerusalema, makao matulivu, hema imara; misumari yake haitaongolewa hata kidogo, kamba zake hazitakatwa hata moja. 21 Humo Yawe atatuonyesha ukubwa wake. Kutakuwa mito mikubwa na vijito, lakini mashua za vita hazitapita, wala mashua kubwa kuingia. 22 Maana Yawe ni mwamuzi wetu, yeye ni mutawala wetu; Yawe ni mufalme wetu, yeye ndiye anayetuokoa. 23 Ewe Sayuni, kamba zako zimeregea, haziwezi kushikilia matanga yake, wala kufungia paa zao. Lakini vitu vingi vilivyonyanganywa vitagawanywa; hata vilema wataweza kupata sehemu yao. 24 Hakuna atakayesema tena ni mugonjwa; watu watasamehewa uovu wao wote. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo