Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Isaya 32 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mufalme wa haki

1 Kutatokea mufalme atakayetawala kwa haki, nao wakubwa wataongoza kwa kufuatana na sheria ya Mungu.

2 Kila mumoja atakuwa kama pahali pa kujikinga na upepo, kama pahali pa kujificha wakati wa mvua kubwa. Watakuwa kama vijito vya maji katika inchi yenye kukauka, kama kivuli cha jiwe kubwa katika jangwa.

3 Macho ya wanaoona hayatapofushwa tena, masikio ya wanaosikia yatabaki wazi.

4 Mioyo ya wasiofikiri itapata ufahamu, wenye vigugumizi watasema upesi.

5 Wapumbafu hawataitwa tena wenye cheo, wala watu wa ovyoovyo hawataitwa tena waheshimiwa.

6 Wapumbafu wanasema maneno ya upumbafu, na mafikiri yao ni kutenda maovu, kutenda mambo ya watu wasiomujua Mungu, kusema maneno ya kumutukana Yawe. Wanawaacha wenye njaa bila chakula, na wenye kiu wanawanyima kinywaji.

7 Matendo ya watu wadanganyifu ni mabaya; hao wanatunga maneno mabaya kwa kumwangamiza masikini kwa maneno ya uongo, hata kama masikini ni mwenye sheria.

8 Lakini wenye heshima wanatenda mambo ya heshima, nao wanatetea mambo yenye heshima.


Maonyo kwa wanawake wa Yerusalema

9 Musimame, enyi wanawake munaostarehe, munisikilize; musikilize maneno ninayosema, enyi wabinti musiojali kitu.

10 Katika mwaka mumoja hivi mutatetemeka ninyi muliotosheka; maana hamutapata mavuno yoyote, na mavuno ya mizabibu yatatoweka.

11 Mutetemeke kwa woga, enyi munaojiikalia tu; mutetemeke kwa hofu, enyi munaostarehe! Muvue nguo zenu, mubakie uchi, mujifungie nguo ya gunia katika viuno vyenu.

12 Mujipige kifua kwa huzuni, muomboleze, juu ya mashamba yaliyokuwa mazuri, juu ya mizabibu iliyokuwa ikizaa sana,

13 juu ya inchi ya watu wangu inayoota miiba na michongoma, juu ya nyumba zote zilizojaa watu wenye furaha, juu ya muji uliokuwa na shangwe.

14 Maana nyumba ya kifalme itaachwa ukiwa, muji huo wa watu wengi utahamwa. Mulima na munara wa ulinzi utakuwa mapango milele, punda wa mwitu watapitapita huko kwa furaha, kondoo watapata malisho yao humo.


Nyakati za amani

15 Hali itaendelea kuwa hivyo mpaka tujazwe Roho wa Mungu kutoka juu. Hapo jangwa litakuwa shamba lenye udongo muzuri tena, na mashamba yenye udongo muzuri yatakuwa pori.

16 Katika inchi jangwa, watu watafuata sheria ya Mungu, katika mashamba yenye udongo muzuri, watatenda kwa haki.

17 Kutokana na kutenda kwa haki, watu watapata amani, utulivu na usalama kwa milele.

18 Watu wangu watakaa katika makao ya amani, katika pahali penye usalama na nafasi yenye utulivu.

19 Lakini mvua ya mawe itanyesha na kuangusha pori, na muji wake utaangamizwa.

20 Lakini heri yenu ninyi: mutapanda mbegu zenu popote penye maji, ngombe na punda wenu watatembeatembea namna wanavyotaka.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan