Isaya 28 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maonyo kwa ufalme wa kaskazini 1 Ole wa Samaria, muji unaokuwa kama taji juu ya bonde kwenye udongo muzuri. Walevi wa ajabu wa Efuraimu wanajivuna kwa ajili yake, lakini utukufu wake utatoweka kama ua linalonyauka! 2 Bwana amejichagulia mutu wake shujaa na mwenye nguvu, ambaye ni kama mvua ya mawe na zoruba kali, kama zoruba ya mafuriko makubwa; kwa mukono wake atawatupa chini. 3 Majivuno na utukufu wa walevi wa Efuraimu vitakanyagwakanyagwa chini, 4 utukufu wake unatoweka kama ua linalonyauka; utukufu uliotawala katika bonde kwenye udongo muzuri utakuwa kama tini za mwanzo mbele ya wakati wa mavuno; mutu akiziona anazichuma na kuzikula mara moja. 5 Siku ile Yawe wa majeshi atakuwa taji tukufu, kama kitambaa kizuri kwa watu wake watakaobaki wazima. 6 Atawaongoza waamuzi wa tribinali kuhukumu kwa haki, nao walinzi wa muji atawapa nguvu. Isaya na manabii walevi wa Yuda 7 Lakini kuna wengine waliolewa divai na kuyumbayumba kwa sababu ya pombe kali; makuhani na manabii wamelewa pombe kali, wamevurugika kwa divai. Wanayumbayumba kwa pombe kali; maono yao yamepotoka, wanajikwaa katika kutoa hukumu. 8 Meza zote zimejaa matapiko, hakuna pahali popote palipo safi. 9 Wao wananichekelea na kuuliza: Huyu nabii anataka kufundisha nani? Anazani atatuelezea sisi ujumbe wake? Sisi ni watoto wachanga walioachishwa kunyonya juzijuzi? 10 Anatufundisha kama watoto wadogo: kanuni juu ya kanuni, mustari juu ya mustari; mara hiki, mara hiki! 11 Basi! Yawe ataongea na watu hawa kwa njia ya watu wa luga tofauti wanaoongea luga ngeni. 12 Yeye alikuwa amewaahidia ninyi: Nitawaonyesha ninyi pumziko, nitawapa pumziko enyi muliochoka. Hapa ni pahali pa pumziko. Lakini wao hawakutaka kunisikiliza. 13 Basi Yawe atawafundisha kama watoto wadogo: kanuni juu ya kanuni, mustari juu ya mustari; mara hiki, mara hiki! Nao watalazimishwa kukimbia lakini wataanguka machalichali, watavunjika, watanaswa na kutekwa. 14 Basi, musikilize neno la Yawe, enyi wenye mazarau munaotawala watu wa Yerusalema: 15 Ninyi munajidai mumefanya agano na kifo mumefanya mapatano na kuzimu! Ninyi munasema kwamba hasara itakapokuja haitawapata, kwa sababu mumefanya uongo kuwa tegemeo lenu, na udanganyifu kuwa kikingio chenu! 16 Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ninaweka katika Sayuni jiwe la musingi, jiwe ambalo limeimarishwa. Jiwe la pembe, la bei kali, jiwe ambalo ni la musingi imara; jiwe linalokuwa na maandiko haya: Anayeamini hataanguka. 17 Nitatumia sheria kama kipimo changu, nitatumia haki kama timazi. Mvua ya mawe itaufagilia mbali uongo munaoutegemea, na mafuriko yataharibu kikingio chenu. 18 Halafu agano lenu na kifo litavunjika, na mapatano yenu na kuzimu yatafutwa. Ile hasara kubwa itakapokuja itawaangusha chini. 19 Kila mara itakapopita kwenu itawapata; nayo itapita kila asubui, muchana na usiku. Kusikia ujumbe huu tu kutakuwa kitisho. 20 Kwenu itakuwa kama anayejinyoosha juu ya kitanda kifupi sana, au kujifunika kwa blanketi inayokuwa ndogo sana! 21 Maana Yawe atasimama kama kule kwenye mulima Perasimu; atawaka hasira kama kule katika bonde la Gebeoni. Atatimiza mupango wake wa ajabu; atatenda kazi yake ya ajabu sana. 22 Basi, ninyi musikuwe na mazarau vifungo vyenu visipate kukazwa zaidi. Maana nimesikia kwamba Yawe wa majeshi amekusudia kuiangamiza inchi yote. Hekima ya Mungu 23 Mutege sikio, musikilize maneno ninayowaambia; musikilize vema hotuba yangu. 24 Mulimaji anayetaka kupanda mbegu anaendelea kulima tu siku zote? Anaendelea kutipua na kusawanisha shamba lake? 25 Hapana! Akisha kusawanisha shamba lake, anapanda mbegu za kunde na mbegu za vikolezo, anapanda ngano na shayiri kwa mustari, na kwenye mipaka ya shamba mimea mingine. 26 Mutu huyo anajua kufanya vile, kwa sababu Mungu wake anamufundisha. 27 Kunde haipepetwi kwa chombo kikali wala mbegu za vikolezo kwa gari! Lakini kunde zinapepetwa kwa fimbo na mbegu za vikolezo kwa kijiti. 28 Mulimaji anapopepeta ngano yake, haendelei kuipepeta mpaka kuvunja punje zake. Anajua jinsi ya kuipepeta kwa gurudumu la gari, bila kuharibu punje za ngano. 29 Ujuzi huu nao unatoka kwa Yawe wa majeshi. Mipango yake ni ya ajabu, hekima yake ni kamilifu kabisa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo