Isaya 26 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wimbo wa ushindi 1 Siku ile watu wataimba wimbo huu katika inchi ya Yuda: Sisi tuna muji imara: Mungu anatulinda kwa kuta na upango. 2 Mufungue milango ya muji, taifa aminifu liingie; taifa linalotenda mambo ya haki. 3 Ee Mungu, unawaweka katika amani wanaokuwa imara, unawaweka katika amani kwa sababu wanakutegemea. 4 Mutumainie Yawe siku zote kwa maana yeye ni kikingio chetu kwa milele. 5 Amewaporomosha waliokaa pande za juu, muji wenye utukufu ameuangusha mpaka chini, ameutupa mpaka katika mavumbi. 6 Sasa muji huo unakanyagwakanyagwa kwa miguu ya watu wamasikini na wazaifu. 7 Njia ya watu wa haki ni yenye kunyooka; ewe Mungu mwenye haki, unasawanisha njia yao. 8 Katika njia ya maamuzi yako tunakungojea ee Yawe; tamaa yetu ni kulikumbuka jina lako. 9 Moyo wangu unakutamani usiku kucha, nafsi yangu inakutafuta kwa moyo. Utakapohukumu dunia, watu wote katika ulimwengu watajifunza haki. 10 Lakini waovu hata wakipewa rehema, hawawezi kujifunza kutenda haki. Hata katika inchi ya usawa, wao bado wanatenda maovu, wala hawajali ukubwa wako wewe Yawe. 11 Ee Yawe umeinua mukono kwa kuwaazibu, lakini hawauoni. Uwaonyeshe namna unavyowapenda watu wako nao watapata haya. Moto unaowatayarishia waadui zako, uwateketeze! 12 Wewe, ee Yawe, umetupatia amani; umefanikisha shuguli zetu zote. 13 Ee Yawe, Mungu wetu, tulipata kutawaliwa na wabwana wengine ambao si wewe, lakini tunakubali wewe pekee kuwa Mungu wetu. 14 Watu hao wamekufa, wala hawataishi tena; wamekuwa mizimu, wala hawatafufuka. Maana wewe umewaazibu na kuwaangamiza, hakuna atakayeweza kuwakumbuka tena. 15 Umezidisha taifa letu, ee Yawe, umelizidisha taifa letu. Umeipanua mipaka yote ya inchi, kwa hiyo wewe unatukuzwa. 16 Ee Yawe, walipotaabika walikutafuta, walikuomba musaada ulipowaazibu. 17 Kama vile mama mwenye mimba anayezaa analia na kugaagaa kwa uchungu, ndivyo tulivyokuwa kwa sababu yako, ee Yawe. 18 Sisi tulipata maumivu ya kuzaa, lakini tukazaa tu upepo! Hatukupata ushindi wowote kwa ajili ya inchi yetu, hatukuweza kuongeza hesabu ya watu katika inchi. 19 Wafu wako wataishi tena, miili yao itafufuka. Wanaolala katika mavumbi wataamuka na kuimba kwa furaha! Mungu atapeleka umande wake wa uzima, nao wanaokuwa kwa wafu watatoka wazima. Kisha azabu ni faraja 20 Mukuje watu wangu, muingie ndani ya nyumba zenu, mujifungie humo ndani. Mujifiche kwa muda mufupi, mpaka kasirani ya Yawe ipite. 21 Maana Yawe anakuja kutoka kwake juu, kutoka makao yake huko mbinguni; kuwaazibu wakaaji wa dunia kwa uovu wao. Nayo dunia haitaficha tena wale waliouawa, lakini itaufichua umwagaji wa damu wote. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo