Isaya 22 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ujumbe wa Mungu juu ya Yerusalema 1 Ujumbe wa Mungu juu ya Bonde la Maono. Kuna nini, ee Yerusalema? Mbona watu wote mumepanda juu ya nyumba? 2 Kwa nini munapiga kelele za shangwe, na muji wote umechangamuka na kujaa vigelegele? Watu wenu waliokufa hawakuuawa katika vita, wala hawakuuawa katika mapigano. 3 Wakubwa wenu wote walikimbia, wakakamatwa hata mbele ya kufyatua mushale mumoja. Watu wako wote waliopatikana walitekwa, ingawa walikuwa wamekimbilia mbali. 4 Ndiyo maana ninawaambia ninyi: musijali chochote juu yangu, muniache nilie machozi ya uchungu. Musijisumbue kunifariji kwa ajili ya kuangamizwa kwa watu wangu. 5 Maana leo Yawe wa majeshi ametuletea fujo, kushindwa na wasiwasi katika Bonde la Maono. Kuta za muji zimebomolewa. Kilio cha wakaaji wake kinasikilika mpaka kwenye milima. 6 Majeshi ya Elamu, pinde na mishale katika mikono, walikuja wamepanda farasi na magari ya vita; nalo jeshi la Kiri lilitayarisha ngao zake. 7 Mabonde yako mazuri, ewe Yerusalema, yalijaa magari ya vita na farasi; wapanda-farasi walijipanga tayari kwenye milango yako. 8 Ulinzi wote wa Yuda uliporomoka. Siku hiyo mulikwenda kutafuta silaha zilizokuwa zimelindwa katika Nyumba ya Pori, 9 mukaona kwamba nyufa za kuta za muji wa Daudi ni nyingi, mukajaza maji ndani ya birika la chini. 10 Mulizikagua nyumba za Yerusalema, mukazibomoa kwa kupata mawe ya kukaza kuta za muji. 11 Katikati ya kuta hizo mulijijengea birika la kulinda maji yanapotiririka kutoka birika la zamani. Lakini hamukumutafuta Mungu aliyepanga mambo haya yote; hamukumujali yeye aliyepanga hayo yote tangu zamani. 12 Siku hiyo, Yawe wa majeshi alitaka mulie na kuomboleza, munyoe nywele na kuvaa nguo za gunia. 13 Lakini ninyi mukafurahi na kusherehekea. Mulichinja ngombe na kondoo, mukakula nyama na kunywa divai. Ninyi mulisema: Acha tukule na kunywa maana kesho tutakufa. 14 Yawe wa majeshi alinifunulia haya akisema: Hakika uovu huu hautasahauliwa mbele ya kufa kwenu. Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. Ujumbe wa Mungu juu ya Sebuna 15 Bwana wetu Yawe wa majeshi aliniambia niende kwa Sebuna, musimamizi wa jamaa ya kifalme, nimwambie hivi: 16 Una haki gani kuwa huku? Una ndugu yeyote hapa, hata ukajichongea kaburi ndani ya jiwe juu ya mulima? 17 Wewe bwana, Yawe atakutupilia mbali kwa nguvu. Atakubana kabisa 18 na kukuzungushazungusha, kisha atakutupa kama mupira mpaka katika inchi pana. Huko utakufia karibu na magari yako ya vita unayojivunia, wewe unayezaraulisha nyumba ya bwana wako. 19 Yawe atakuongoa toka katika madaraka yako na kukuporomosha kutoka pahali unapokuwa. 20 Siku hiyo, nitamuleta mutumishi wangu Eliakimu mwana wa Hilkia. 21 Nitamuvalisha nguo yako ya heshima, na mukaba wako na kumupa madaraka yako. Yeye atakuwa baba kwa watu wa Yerusalema na kwa ukoo wa Yuda. 22 Nitaweka juu ya bega lake ufunguo wa ukoo wa Daudi. Akifungua, hakuna atakayeweza kufunga na akifunga, hakuna atakayeweza kufungua. 23 Nitamwimarisha Eliakimu kama musumari uliopigiliwa pahali pagumu, naye atapata heshima tukufu katika ukoo wa wazee wake. 24 Watu wote na jamaa yake, wadogo kwa wakubwa watajitegemeza kwake kama chungu na vikombe vilivyotundikwa kwenye musumari. 25 Lakini siku moja, –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi– ule musumari uliopigiliwa pahali pagumu utaregea kwa uzito. Utakatwa na kuanguka. Yawe amesema. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo