Isaya 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Amani ya kudumu ( Mika 4.1-3 ) 1 Haya ndiyo mambo Isaya mwana wa Amozi aliyofunuliwa juu ya inchi ya Yuda na Yerusalema. 2 Katika siku zinazokuja, itatukia kwamba mulima wa nyumba ya Yawe utaimarishwa kupita milima yote, utainuliwa juu ya vilima vyote. Mataifa yote yatajaa kule, 3 watu wengi wataenda kule na kusema, Mukuje tupandie kwenye mulima wa Yawe, tuende kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo, apate kutufundisha njia zake, nasi tutafuata mapito yake. Maana sheria itakuja kutoka Sayuni; neno la Yawe kutoka Yerusalema. 4 Mungu atafanya hukumu kati ya mataifa; ataamua maneno kati ya watu wengi. Watu watafua panga za vita kuwa majembe na mikuki yao kuwa visu vya kuvuna. Taifa halitapigana na taifa lingine wala hayatafanya tena mazoezi ya vita. 5 Sasa, enyi wazao wa Yakobo, mukuje, tutembee katika mwangaza wa Yawe. Kiburi kitaondolewa 6 Sasa, ee Mungu, umewatupa watu wako, wazao wa Yakobo. Maana kweli wachawi kutoka mashariki wamejaa kati yao; kuna waaguzi kama vile kwa Wafilistini. Wanashirikiana na watu wageni. 7 Inchi yao imejaa feza na zahabu, akiba yao ni kubwa zaidi. Inchi yao imejaa farasi, magari yao ya vita hayana hesabu. 8 Inchi yao imejaa sanamu za miungu, watu wake wanaabudu kazi ya mikono yao, vitu walivyotengeneza wao wenyewe. 9 Kwa hiyo, kila mutu atapata haya na kufezeheshwa. Usiwasamehe hata kidogo, ee Mungu! 10 Muingie chini ya jiwe, mujifiche katika mavumbi, kwa kuepuka kitisho cha Yawe, mbali na mwangaza wa utukufu wake. 11 Macho yenye kiburi ya wanadamu yatanyenyekezwa, watu wenye majivuno watashushwa chini, na Yawe peke yake atatukuzwa siku hiyo. 12 Kweli, siku ya Yawe wa majeshi inakuja juu ya wote wenye kiburi na majivuno, juu ya wote wanaojitukuza, 13 juu ya miti ya mierezi yote ya Lebanoni ambayo ni mirefu na mizuri, juu ya miti ya mialo yote katika inchi ya Basani, 14 juu ya milima yote mirefu, juu ya vilima vyote vinavyoinuka juu sana; 15 juu ya minara yote mirefu, juu ya kuta zote ndefu, 16 juu ya mashua yote makubwa ya Tarsisi, na juu ya mashua yote mazuri. 17 Kiburi cha wanadamu kitashushwa, majivuno ya watu yatanyenyekezwa, na Yawe peke yake atatukuzwa siku hiyo. 18 Sanamu zote za miungu zitatoweka kabisa. 19 Muingie katika mapango chini ya mawe, katika mashimo ndani ya udongo, kwa kuepuka kitisho cha Yawe, mbali na mwangaza wa utukufu wake, atakapokuja kuogopesha dunia. 20 Siku hiyo, watu watawatupia panya na popo sanamu za feza na zahabu walizojitengenezea kusudi waziabudu. 21 Nao wataingia katika mapango chini ya mawe na kwenye nyufa za mawe, kwa kuepuka kitisho cha Yawe, mbali na mwangaza wa utukufu wake, atakapokuja kuogopesha dunia. 22 Usimutumainie mwanadamu, uzima wake ni kama pumzi tu. Yeye anafaa kitu gani? |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo