Isaya 19 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu ataazibu inchi ya Misri 1 Ujumbe wa Mungu juu ya inchi ya Misri. Yawe amepanda juu ya wingu linaloenda mbio na kuja mpaka katika inchi ya Misri. Sanamu za miungu ya Wamisri zitatetemeka mbele yake, mioyo ya Wamisri itayeyuka kwa woga. 2 Mimi nitawachonganisha Wamisri wao kwa wao. Ndugu atapigana na ndugu yake, jirani atapigana na jirani yake, muji mumoja na muji mwingine, mufalme mumoja na mufalme mwingine. 3 Nitawaondolea Wamisri uhodari wao. Nitaivuruga mipango yao. Watatafuta shauri kwa sanamu na mizimu, wachawi, mizuka na pepo. 4 Nitawatia Wamisri katika mikono ya bwana mukali, mufalme mukali ambaye atawatawala. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe wa majeshi. 5 Maji ya muto Nili yatakaushwa, nao utakauka kabisa. 6 Mifereji yake itatoa harufu mbaya, vijito vyake vitapunguka na kukauka. Nyasi na matete yake yataoza. 7 Sehemu za kandokando ya Nili zitakuwa tupu. Mimea yote iliyopandwa humo itakauka na kupeperushiwa mbali na kutoweka. 8 Wavuvi wataomboleza, wote wanaotumia ndoana watalalamika, wote wanaotega nyavu humo watavunjika moyo. 9 Wafuma nguo za kitani watafazaika, wote kwa pamoja watavunjika moyo. 10 Wafuma nguo watafezeheshwa, na wafanya kazi watahuzunika. 11 Wakubwa wa muji wa Soani ni wapumbafu kabisa, washauri wa Mufalme wa Misri wanatoa shauri la kijinga! Kila mumoja anaweza namna gani kumwambia Mufalme wa Misri: Mimi ni wa uzao wa wenye hekima, wa uzao wa wafalme wa zamani! 12 Wako wapi, ewe Mufalme wa Misri, wenye hekima wako? Uwaache basi wakwambie na kukujulisha mambo Yawe wa majeshi aliyopanga juu ya Misri! 13 Lakini wakubwa wa Soani ni wapumbafu, wakubwa wa Nofi wamedanganyika. Hao wanaokuwa musingi wa makabila yao wamelipotosha taifa la Misri. 14 Yawe amewamwangia roho ya fujo, wakawapotosha Wamisri katika mipango yao yote, nao wakakuwa kama mulevi anayeyumbayumba akitapika. 15 Hakuna mutu yeyote katika inchi ya Misri, mutawala au wanainchi, wakubwa au watu wadogo, anayeweza kufanya jambo lolote la maana. Wamisri watamwabudu Yawe 16 Siku ile watu wa Misri wataogopa kama wanawake. Watatetemeka kwa hofu watakapomwona Yawe wa majeshi ameunyoosha mukono wake juu yao. 17 Yuda atakuwa kitisho kikubwa kwa Wamisri. Wote watakaoambiwa habari za Yuda wataingiwa na woga kwa sababu ya jambo Yawe wa majeshi aliloamua kuwatendea. 18 Siku hiyo luga ya Kiebrania itatumika katika miji mitano ya Misri, na watu wa miji hiyo wataapa kuwa waaminifu kwa Yawe wa majeshi. Muji mumoja kati ya miji hiyo utaitwa “Muji wa Jua”. 19 Siku hiyo, kutakuwa mazabahu kwa ajili ya Yawe katikati ya inchi ya Misri, na nguzo iliyotakaswa kwa ajili ya Mungu kwenye mpaka wa Misri. 20 Mazabahu hayo yatakuwa kitambulisho na ushuhuda kwa Yawe wa majeshi katika inchi ya Misri. Watu wakimulilia Yawe humo kwa sababu ya kugandamizwa, yeye atawapelekea mukombozi atakayewatetea na kuwakomboa. 21 Yawe atajijulisha kwa Wamisri na hapo ndipo Wamisri watakapomwitikia na kumwabudu kwa kumutolea matoleo na sadaka za kuteketezwa. Vilevile watafanyia Yawe viapo ambavyo watavitimiza. 22 Yawe atawaazibu Wamisri na kuwaponya. Nao watamurudilia, naye atayasikiliza maombi yao na kuwaponya. 23 Wakati huo, kutakuwa barabara kubwa kutoka inchi ya Misri mpaka katika inchi ya Asuria. Waasuria watawatembelea Wamisri, na Wamisri watawatembelea Waasuria; nao wote watamwabudu Mungu pamoja. 24 Wakati huo, Israeli itahesabiwa pamoja na Misri na Asuria; mataifa haya matatu yatakuwa baraka kwa dunia yote. 25 Yawe wa majeshi atawabariki na kusema: Wabarikiwe Wamisri watu wangu, vilevile na Waasuria ambao ni kitambulisho cha kazi yangu na Waisraeli wanaokuwa urizi wangu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo