Hosea 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Walimu wabaya wa Israeli 1 Musikilize, enyi makuhani! Mutege sikio, enyi Waisraeli! Musikilize, enyi ukoo wa kifalme! Ninyi mulipaswa kulinda haki, pahali pake mumekuwa kama mutego kule Misipa, mumekuwa kama wavu wa kuwanasa kule Tabori. 2 Mumechimba shimo refu la kuwanasa kule Sitimu. Lakini mimi nitawaazibu ninyi wote. 3 Ninawajua watu wa Efuraimu, Waisraeli hawakufichwa kwangu. Ninyi watu wa Efuraimu mumefanya uzinzi, watu wote wa Israeli wamejichafua. Hosea anatoa maonyo juu ya ibada za miungu 4 Matendo yao yanawazuia wasimurudilie Mungu wao. Wamejaa uzinzi ndani ya mioyo yao; hawanijui mimi Yawe. 5 Kiburi cha Waisraeli kinaonekana wazi; watu wa Efuraimu watajikwaa katika makosa yao, nao watu wa Yuda watajikwaa pamoja nao. 6 Watakwenda na makundi yao ya kondoo na ngombe, kumutafuta Yawe; lakini hawataweza kumupata, kwa sababu amejitenga nao. 7 Wamevunja uaminifu kwa Yawe, wamezaa watoto wa haramu. Mwezi mumoja utatosha kwa kuwaangamiza, pamoja na mashamba yao. 8 Mupige baragumu kule Gibea, na ngunga kule Rama. Mupige kelele la kujulisha hatari kule Beti-Aweni. Enyi watu wa Benjamina, adui yenu yuko nyuma! 9 Siku nitakapotoa azabu, Efuraimu itakuwa kama jangwa! Ninachotangaza kati ya makabila ya Israeli, ni jambo litakalotukia kwa hakika. 10 Waongozi wa Yuda wamekuwa wenye kubadilisha mipaka ya inchi. Mimi nitawamwangia hasira yangu kama maji. 11 Efuraimu ameteswa, haki zake zimetwaliwa; maana alikusudia kufuata mambo isiyokuwa na maana. 12 Hivyo mimi Mungu niko kama nondo kwa Efuraimu, kama kidonda kibaya kwa watu wa Yuda. 13 Watu wa Efuraimu walipogundua ugonjwa wao, watu wa Yuda walipogundua kidonda chao, watu wa Efuraimu walikwenda Asuria kuomba musaada kwa mufalme mukubwa; lakini yeye hakuweza kuwatunza, hakuweza kuponyesha kidonda chao. 14 Maana mimi nitakuwa kama simba kwa Efuraimu, kama simba mukali kwa watu wa Yuda. Mimi mwenyewe nitawararua na kuondoka, nitawakamata na hakuna atakayewaokoa. 15 Nitarudi mahali pangu na kujitenga nao mpaka watambue kosa lao na kunirudilia. Taabu zao zitawafundisha wanitafute. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo