Hosea 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu anawashitaki watu wake 1 Musikilize maneno ya Yawe, enyi Waisraeli. Yawe anawashitaki wakaaji wa inchi hii. Hakuna tena uaminifu wala wema katika inchi; hakuna anayemujua Mungu katika inchi hii. 2 Kuapa, uongo, mauaji, wizi na uzinzi vinatokea humo. Umwangaji wa damu unafuatana kwa mufululizo. 3 Kwa hiyo, inchi yote inakauka, wakaaji wake wote wanaangamia pamoja na nyama na ndege; hata samaki wanaangamizwa. Mungu anawashitaki makuhani 4 Lakini watu wasilaumiwe, wasishitakiwe; maana mimi ninakushitaki wewe kuhani. 5 Wewe utajikwaa muchana, naye nabii atajikwaa pamoja nawe usiku. Nitamwangamiza mama yako Israeli. 6 Watu wangu wameangamia kwa kutonijua, maana wewe kuhani umekataa mafundisho. Nimekukataa kuwa kuhani wangu. Kwa maana umeisahau sheria ya Mungu wako, nami vilevile nitawasahau watoto wako. 7 Kadiri makuhani walivyoongezeka, ndivyo wote walivyozidi kuniasi. Basi, nitageuza utukufu wao kuwa haya. 8 Wanajishibisha kwa sadaka za watu wangu wenye zambi. Wana hamu sana ya kuwaona wakitenda zambi. 9 Lakini yatakayowapata watu yatawapata makuhani; nitawaazibu kwa sababu ya mwenendo wao, nitawalipiza matendo yao wenyewe. 10 Watakula, lakini hawatashiba, watazini, lakini hawatapata watoto, kwa sababu wameniacha mimi Yawe, na kufuata miungu mingine. Mungu analaani ibada za miungu 11 Uasherati, divai mupya na ya zamani vinaondoa maarifa. 12 Watu wangu wanaomba shauri kutoka kwa muti; kijiti chao cha kuaguza ndicho kinachowapa shauri. Nia ya kufanya uzinzi imewapotosha; wamefanya uzinzi kwa kufuata miungu mingine, wakaniacha mimi Mungu wao. 13 Wanatambikia kwenye vilele vya milima; wanatoa sadaka kwenye vilima, chini ya miti ya mwalo, migude na mikwaju, maana kivuli chao ni kizuri. Kwa hiyo wabinti wenu wanafanya uzinzi, na bibi-arusi wenu anafanya uasherati. 14 Lakini sitawaazibu wabinti zenu wanapofanya uzinzi, wala bibi-arusi wenu wanapofanya uasherati, maana, wanaume wenyewe ndio wanaofuatana na wazinzi, na kutambikia pamoja nao katika ibada za uzinzi. Watu hawa wenye kukosa akili hakika wataangamia! 15 Ikiwa kweli ninyi Waisraeli ni wazinzi lakini, watu wa Yuda basi wasianguke ndani ya makosa! Musiende pahali patakatifu kule Gilgali, wala musiende kule Nyumba ya Uovu. Wala musiape mukisema: Kama vile Yawe anavyoishi! 16 Waisraeli ni wenye kichwa kigumu kama punda. Kwa nini basi Mungu ashugulike na kuwachunga, kama kondoo katika shamba kubwa la kuwakulishia? 17 Watu wa Efuraimu wamejiunga na sanamu. Basi! Uwaache waendelee tu! 18 Kama vile kundi la walevi, wanajizamisha wenyewe katika uzinzi; wanapendelea mambo ya haya kuliko heshima yao. 19 Basi, zoruba itawapeperusha, nao watapata haya kwa ajili ya sadaka zao. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo