Hosea 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Waisraeli watarudishiwa tena hali yao ya mbele 1 Lakini hesabu ya Waisraeli itakuwa kubwa kama muchanga wa bahari ambao haupimiki wala hauhesabiki. Pale ambapo Mungu aliwaambia: Ninyi si watu wangu, sasa atawaambia: Ninyi ni watoto wa Mungu Mwenye Uzima. 2 Watu wa Yuda na Waisraeli wataungana pamoja na kumuchagua mwongozi wao mumoja; nao watastawi katika inchi yao. Hiyo itakuwa siku kubwa ya Yezereheli. 3 Basi, muwaite wakaka zenu, “Watu wangu”, na wadada zenu, “Waliohurumiwa”. Muke muzinzi – taifa potovu la Israeli 4 Mumushitaki mama yenu, mumushitaki, maana sasa yeye si muke wangu wala mimi si mume wake. Mumushitaki aondoe vitambulisho vya uasherati juu ya uso wake, ajiepushe na mapambo ya uzinzi juu ya kifua chake. 5 Kama sivyo, nitamuvua nguo abaki uchi, nitamufanya akuwe sawa vile alivyozaliwa. Nitamufanya akuwe utupu sawa jangwa, akauke sawa inchi kavu. Nitamwua kwa kiu. 6 Na watoto wake sitawahurumia, maana ni watoto wa uzinzi. 7 Mama yao amefanya uzinzi, aliyebeba mimba yao amefanya mambo ya haya. Alisema: Nitaambatana na wapenzi wangu, ambao wananipatia chakula na maji, nguo za sufu na kitani, pamoja na mafuta na divai. 8 Basi, nitafunga njia yake kwa miiba, nitamuzungushia ukuta, asipate njia ya kutokea inje. 9 Atawafuata wapenzi wake, lakini hatawapata; atawatafuta, lakini hatawaona. Kwa hiyo atasema: Nitarudi kwa mume wangu wa kwanza; maana zamani nilikuwa na raha kuliko sasa. 10 Hakujua kwamba ni mimi niliyemupa ngano, divai na mafuta, niliyemujalia feza na zahabu kwa wingi, ambazo alimupelekea mungu Bali. 11 Kwa hiyo wakati wa mavuno nitaitwaa ngano yangu, nitaiondoa divai yangu kwa wakati wake. Nitamunyanganya nguo zangu za sufu na kitani, ambazo zilitumika kuufunika uchi wake. 12 Nitamuvua nguo abaki uchi mbele ya wapenzi wake, wala hakuna mutu atakayeweza kunizuia. 13 Nitakomesha furaha zake zote, sikukuu zake za mwandamo wa mwezi na za Sabato, na sikukuu zote zilizoamriwa. 14 Nitaiharibu mizabibu yake na tini zake, anayosema ni malipo kutoka kwa wapenzi wake. Nitaifanya ikuwe pori, nao nyama wa pori wataikula. 15 Nitamulipiza kwa ajili ya siku alizoabudu sanamu za mungu Bali, kwa ajili ya muda alioutumia kuzifukizia ubani, akajipamba kwa pete zake na ushanga, na kuwaendea wapenzi wake, akanisahau mimi. –Ni ujumbe wa Yawe. Upendo wa Yawe kwa watu wake 16 Kwa hiyo, nitamushawishi, nitamupeleka katika jangwa na kusema naye kwa upole. 17 Huko nitamurudishia mashamba yake ya mizabibu. Bonde la Akori litakuwa mulango wa tumaini. Ataniitikia vizuri kama vile alipokuwa kijana, kama wakati alipotoka katika inchi ya Misri. 18 Siku hiyo, wewe utaniita “Mume wangu”, na sio tena “Bali wangu”. –Ni ujumbe wa Yawe.– 19 Maana, nitalifanya jina la Bali lisitajike tena katika kinywa chako. 20 Nitafanya agano na nyama wa pori, ndege pamoja na vyote vinavyotambaa, kusudi wasikuumize. Nitaondoa upinde, upanga na silaha za vita katika inchi, na kukufanya uishi kwa usalama. 21 Nitakufanya muke wangu milele; ukuwe wangu kwa sheria na haki, kwa wema na huruma. 22 Kweli, nitakuoa kwa uaminifu, nawe utanijua mimi Yawe. 23 Siku hiyo, nitajibu kwa mahitaji ya mbingu ya kunyesha mvua, mbingu nazo zitajibu kwa mahitaji ya udongo. –Ni ujumbe wa Yawe.– 24 Udongo utajibu mahitaji ya ngano, divai na mafuta, navyo vyote vitajibu kwa mahitaji ya Yezereheli. 25 Nitamwotesha Yezereheli katika inchi; nitamuhurumia yule aliyeitwa “Asiyehurumiwa”, na wale walioitwa “Si wangu”, nitawaambia: “Ninyi ni watu wangu”. Nao watasema: Wewe ni Mungu wetu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo