Hosea 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Waefuraimu waliposema, watu wote walitetemeka; Waefuraimu walikuwa na uwezo mukubwa katika inchi ya Israeli, lakini walianza kumwabudu mungu Bali, wakajiletea kifo. 2 Waefuraimu wanaendelea kutenda zambi, wanajitengenezea sanamu za feza yenye kuyeyushwa, sanamu zinazotengenezwa kwa ufundi wao, zote zikiwa kazi ya wafundi. Wanasema: Muzitambikie! Wanaume wanabusu sanamu ya mwana-ngombe! 3 Basi, watatoweka kama ukungu wa asubui, kama umande unaotoweka upesi; kama makapi yanayopeperushwa kwenye nafasi ya kupepetea, kama moshi unaotoka katika munara wa kutoshea moshi inje. 4 Yawe anasema: Lakini mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatoa katika inchi ya Misri; hakuna mungu mwingine lakini mimi, wala hakuna anayeweza kuwaokoa. 5 Ni mimi niliyewachunga mulipokuwa katika jangwa, katika inchi iliyokuwa yenye kukauka. 6 Lakini mulipokwisha kula na kushiba, mulianza kuwa na kiburi, mpaka mukanisahau. 7 Basi, nitakuwa kama simba kwenu ninyi wote; nitawavizia kama chui katika njia. 8 Nitawarukia kama dubu aliyenyanganywa watoto wake. Nitawararua vifua vyenu na kuwakula palepale kama simba; nitawararua vipandevipande kama nyama wa pori. 9 Nitawaangamiza, enyi Waisraeli. Nani ataweza kuwasaidia? 10 Yuko wapi sasa mufalme wenu awaokoe? Wako wapi wale wakubwa wenu wawalinde? Ninyi ndio mulioomba: Utupatie mufalme na wakubwa watutawale. 11 Kwa hasira yangu mimi nikawapa mufalme, kisha nikamwondoa kwa kasirani yangu. 12 Uovu wa Efuraimu uko umeandikwa, zambi yake imewekwa akiba. 13 Maumivu kama ya kuzaa mutoto yanamufikia. Lakini yeye ni mutoto mupumbafu; wakati wa kuzaliwa unapofika yeye anakataa kutoka ndani ya tumbo la mama! 14 Inanipasa kuwakomboa hawa watu kutoka kuzimu; sharti niwaokoe kutoka kifo! Ewe kifo, mapigo yako ni wapi? Ewe kuzimu, kuangamiza kwako ni wapi? Mimi sitawaonea tena huruma! 15 Hata kama Efuraimu atastawi kama nyasi, mimi Yawe nitavumisha upepo mukali wa mashariki, upepo utakaotokea kule katika jangwa, nao utakausha visima vyake, chemichemi zake zitakauka. Vitu vyake vyote vya bei kali vitaharibiwa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo