Hosea 10 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kuharibishwa kwa vitu vya ibada vya Israeli 1 Waisraeli walikuwa kama muzabibu muzuri, muzabibu wenye kuzaa matunda. Kadiri matunda yalivyozidi kuongezeka, ndivyo walivyozidi kujijengea mazabahu. Kadiri inchi yao ilivyozidi kustawi, ndivyo walivyozidi kupamba nguzo zao za ibada. 2 Mioyo yao imejaa udanganyifu. Sasa ni lazima wabebe makosa yao. Yawe atabomoa mazabahu zao na kuziharibu nguzo zao. 3 Wakati huo watasema: Hatuna tena mufalme, kwa maana hatumwogopi Yawe; lakini, naye mufalme atatufanyia nini? 4 Wanachosema ni maneno matupu; wanaapa na kufanya mapatano ya bure; haki imekuwa si haki tena, inachipuka kama mimea yenye sumu katika shamba. 5 Wakaaji wa Samaria watatetemeka kwa sababu ya sanamu ya mwana-ngombe wa kule Beteli. Watu wake watamwombolezea mwana-ngombe yule, hata makuhani wanaomwabudu watamulilia; maana utukufu wa mwana-ngombe yule umeondolewa. 6 Sanamu hiyo itapelekwa Asuria, kama zawadi kwa mufalme mukubwa. Watu wa Efuraimu watafezeheka, Waisraeli watapata haya kwa ajili ya sanamu yao. 7 Mufalme wa Samaria atapelekwa, kama kipande cha muti juu ya maji. 8 Pahali pa kutambikia juu ya vilima pa Aweni, pahali Waisraeli walipofanyia zambi, pataharibiwa. Miiba na michongoma vitaota katika mazabahu zao. Nao wataiambia milima: Mutufunike na vilima: Mutuangukie! Israeli atavuna alichopanda 9 Enyi Waisraeli, ninyi mumetenda zambi tangia kule Gibea, na mpaka sasa munaendelea. Hakika vita itawaangamizia kulekule Gibea. 10 Nitawaendea watu hawa wapotovu na kuwaazibu; watu wa mataifa watakusanyika kwa kuwashambulia, watakapoazibiwa kwa ajili ya zambi zao nyingi. 11 Efuraimu ni mwana-ngombe aliyefundishwa vizuri, akapenda kupepeta ngano. Lakini sasa shingo yake nzuri nitaifunga nira. Yuda atalima kwa jembe yeye mwenyewe, Yakobo atakokota jembe la kupalilia. 12 Mupande haki kwa faida yenu, nanyi mutavuna wema; mulime mashamba yaliyoachwa, maana wakati wa kutafuta Yawe umefika kusudi awanyeshee haki kama mvua. 13 Lakini ninyi mumepanda uovu, ninyi mumevuna ubaya; mumekula matunda ya uongo wenu. Wewe Israeli ulitegemea nguvu zako mwenyewe, na wingi wa waaskari wako. 14 Kwa hiyo fujo ya vita itawafikia watu wako, kuta zako zote zitaharibiwa. Kama vile mufalme Salmani alivyoharibu Beti-Arbeli katika vita, wamama wakapondwa pamoja na watoto wao. 15 Ndivyo itakavyokuwa kwenu enyi watu wa Beteli, kwa sababu ya uovu wenu mukubwa. Kutakapopambazuka mufalme wa Israeli atauawa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo