Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Hesabu 27 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Haki ya kurizi kwa wanawake

1 Mala, Noa, Hogla, Milka na Tirsa walikuwa wabinti za Selofehadi. Naye Selofehadi alikuwa mwana wa Heferi mwana wa Gileadi mwana wa Makiri mwana wa Manase mwana wa Yosefu.

2 Basi, hao wabinti wane wakamwendea Musa, wakasimama mbele yake na kuhani Eleazari na viongozi wote wa Waisraeli, kwenye mulango wa hema la mukutano, wakasema:

3 Baba yetu alikufia katika jangwa na bila mutoto yeyote mwanaume. Yeye hakukuwa kati ya wafuasi wa Kora waliokusanyika mbele ya Yawe, lakini alikufa kutokana na zambi yake mwenyewe. Hakukuwa na mutoto mwanaume.

4 Kwa nini basi jina la baba yetu lifutwe katika ukoo wake kwa sababu hakukuwa na mutoto mwanaume? Utupatie urizi pamoja na wandugu za baba yetu.

5 Musa akaleta malalamiko yao mbele ya Yawe.

6 Yawe akamwambia Musa:

7 Wanachosema wabinti za Selofehadi ni kweli; uwape urizi pamoja na wandugu za baba yao, watwae urizi wake.

8 Kisha uwaambie Waisraeli kwamba mutu yeyote akikufa bila kuacha mutoto mwanaume, urizi wake utapewa kwa binti yake.

9 Ikiwa hana binti, basi urizi huo utapewa kwa wandugu zake wanaume.

10 Na ikiwa hana ndugu mwanaume, basi urizi wake utawaendea baba zake wakubwa na wadogo.

11 Na ikiwa baba yake hana ndugu mwanaume, basi urizi wake utamwendea wandugu zake wa karibu, naye ataurizi kama vile mali yake. Hii itakuwa sharti na agizo kwa Waisraeli, kama vile mimi Yawe nilivyokuamuru.


Yoshua anachaguliwa kuwaongoza Waisraeli
( Kumb 31.1-8 )

12 Yawe akamwambia Musa: Panda juu ya mulima huu wa miinuko ya Abarimu uangalie inchi ambayo nimewapa Waisraeli.

13 Ukisha kuiona, utakufa na kukutana na wazee wako, kama vile ndugu yako Haruni alivyokutana nao,

14 kwa sababu hamukuitii amri yangu kule katika jangwa la Sini, wakati watu wote pamoja waliponigombanisha kule Meriba. Ninyi hamukuacha utukufu wangu uonekane mbele yao walipotaka wapewe maji. (Meriba ni chemichemi ya maji ya Kadesi katika jangwa la Sini).

15 Naye Musa akamwomba Yawe:

16 Ee Yawe, Mungu unayekuwa asili ya uzima wote, ninakuomba umuchague mutu wa kusimamia watu hawa,

17 ambaye atawatangulia na kuwaongoza katika shuguli zao zote, kusudi wasikuwe kama kondoo wasiokuwa na muchungaji.

18 Yawe akamwambia Musa: Umutwae Yoshua mwana wa Nuni, mutu mwenye roho nzuri, kisha uweke mikono juu yake,

19 na kumusimamisha mbele ya kuhani Eleazari na watu wote, umupatie kazi hiyo.

20 Umupe sehemu ya mamlaka yako kusudi Waisraeli wote wamutii.

21 Yeye atamutegemea kuhani Eleazari ambaye atamujulisha mapenzi yangu kwa kutumia jiwe la shauri. Kwa njia hii, Eleazari atamwongoza Yoshua na Waisraeli wote wanapotoka na wanapoingia.

22 Musa akafanya kama vile alivyoamriwa na Yawe. Akamutwaa Yoshua na kumusimamisha mbele ya kuhani Eleazari na Waisraeli wote.

23 Kisha akamwekea mikono juu ya kichwa na kumupa mamlaka kama vile alivyoagizwa na Yawe.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan