Hesabu 24 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Sasa Balamu akatambua kwamba Yawe alipenda kuwabariki Waisraeli, kwa hiyo hakukwenda sawa vile mara ingine kwa kutafuta uchawi. Akaelekea kwenye jangwa, 2 akainua macho, akawaona Waisraeli wamepiga kambi kila kabila pahali pake. Kisha Roho ya Mungu ikamufikia, 3 naye akasema mashairi haya ya Yawe: Mashairi yangu mimi Balamu mwana wa Peori mashairi ya mutu aliyefumbuliwa macho. 4 Anasema yeye aliyesikia maneno ya Mungu, mutu aliyeona maono ya Mungu Mwenye Nguvu, mutu anayeinama uso mpaka chini na kuona wazi. 5 Hema zenu zinapendeza sana, enyi watu wa Yakobo; hakika, kambi zenu, enyi watu wa Israeli! 6 Ni kama mabonde yanayotiririka maji, kama bustani kandokando ya muto, kama miti ya mishubiri Yawe aliyopanda, kama mierezi kandokando ya maji. 7 Watakuwa na hazina ya kutosha ya maji, mbegu yao itapata maji mengi, mufalme wao atakuwa mukubwa kuliko Agagi, na ufalme wake utatukuka sana. 8 Mungu aliwaondoa kutoka Misri, naye anawapigania kwa nguvu kama mbogo. Atayateketeza mataifa yanayokuwa waadui zao, atavunjavunja mifupa yao, atawachoma kwa mishale yake. 9 Atavizia na kulala chini kama simba, nani atasubutu kumwamusha? Abarikiwe yeyote atakayekubariki wewe Israeli, alaaniwe yeyote atakayekulaani. 10 Balaki akawaka hasira juu ya Balamu, akapiga mikono kwa kasirani na kumwambia: Nilikuita uwalaani waadui zangu, lakini mara hizi zote tatu umewabariki! 11 Sasa! Kwenda zako. Nilikuwa nimekuahidi kukupa zawadi nyingi, lakini Yawe hakukujalia kupata zawadi hizo, amekunyima! 12 Balamu akamujibu Balaki: Unakumbuka nilivyowaambia wajumbe uliowatuma kwangu. 13 Niliwaambia kwamba hata kama ungenipa nyumba yako imejaa feza na zahabu, mimi sitaweza kubadilisha agizo la Yawe, kwa kufanya jambo lolote, jema au baya kwa mapenzi yangu mwenyewe. Nilisema kwamba atakachosema Yawe ndicho nitakachosema. 14 Sasa ninarudi kwa watu wangu, lakini mbele sijaondoka, acha nikuambie mambo ambayo watu hao watawatendea watu wako siku zinazokuja. 15 Basi, Balamu akasema mashairi haya: Mashairi yangu mimi Balamu mwana wa Beori, mashairi ya mutu aliyefumbuliwa macho, 16 mashairi ya mutu aliyesikia maneno ya Mungu, na mutu anayejua maarifa ya Mungu Mukubwa, mutu anayeona maono ya Mungu Mwenye Nguvu, mutu anayeinama uso mpaka chini, macho wazi. 17 Ninamwona atakayekuja, ninamwona, lakini hayuko karibu. Nyota itatokea kwa wazao wa Yakobo, atatokea mufalme kati ya Waisraeli. Kwa fimbo yake atapiga viongozi wa Wamoabu, atawaangamiza wazao wote wa Seti. 18 Edomu itakuwa urizi wake, Seiri itakuwa mali yake, Israeli itapata ushindi mukubwa. 19 Mumoja wa wazao wa Yakobo atatawala naye atawaangamiza watakaobaki katika muji. 20 Kisha Balamu akawaangalia Waamaleki, akatoa mashairi haya: Amaleki ni taifa lenye nguvu kuliko yote, lakini kwa mwisho litaangamia kabisa. 21 Kisha Balamu akawaangalia Wakeni, akatoa mashairi haya: Makao yenu ni salama, enyi Wakeni, kama chicha juu kabisa ya mulima. 22 Lakini mutateketezwa, enyi Wakeni. Mutapelekwa mateka na Asuria mpaka wakati gani? 23 Tena Balamu akatoa mashairi haya: Ole! Nani ataishi Mungu atakapofanya hayo? 24 Mashua zitafika kutoka Kitimu, wataishambulia Asuria na Eberi, lakini nao vilevile wataangamia milele. 25 Basi, Balamu akaondoka, akarudi kwake; Balaki vilevile akaenda zake. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo