Hagai 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu anaamuru hekalu lijengwe upya 1 Katika mwaka wa pili wa utawala wa mufalme Dario wa Persia, siku ya kwanza ya mwezi wa sita, kwa njia ya nabii Hagai, neno la Yawe liliwafikia Zerubabeli mwana wa Saltieli pamoja na Kuhani Mukubwa Yoshua mwana wa Yosadaki kusema hivi: 2 Yawe wa majeshi anasema hivi: Watu hawa wanasema kwamba wakati wa kuijenga upya nyumba ya Yawe haujafika. 3 Neno la Yawe lilifika kwa njia ya nabii Hagai kusema hivi: 4 Ni sawa kwenu kukaa katika nyumba zenu nzuri wakati nyumba yangu ni mabomoko matupu? 5 Basi, Yawe wa majeshi anasema hivi: Mufikiri vizuri juu ya namna munavyofanya! 6 Munapanda mbegu kwa wingi, lakini munavuna kidogo. Munakula, lakini hamushibi. Munakunywa divai, lakini hamutosheki. Munavaa nguo, lakini bado munasikia baridi. Mushahara wa mutumishi unakuwa kama umetumbukizwa katika mufuko uliotoboka. 7 Yawe wa majeshi anasema hivi: Mufikiri vizuri juu ya namna munavyofanya! 8 Sasa basi muende kwenye milima mulete miti, muijenge upya nyumba yangu, nipate kuifurahia na kutukuzwa. –Ni Yawe anayesema hivyo. 9 Mulitazamia mavuno mengi, lakini mulipata kidogo tu. Mulipoyaleta kwenye nyumba, niliyapeperusha mbali. Kwa nini? Kwa sababu nyumba yangu ni mabomoko matupu wakati kila mumoja wenu anashugulikia nyumba yake. 10 Ndiyo maana mbingu zimeacha kunyesha mvua, nao udongo hauoteshi mavuno. 11 Nimeleta ukavu katika inchi, juu ya vilima na mashamba ya ngano, mashamba ya mizabibu na mashamba ya mizeituni na kila mumea, watu na nyama, na chochote mulichokitoshea jasho. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi. 12 Halafu Zerubabeli mwana wa Saltieli, na Kuhani Mukubwa Yoshua mwana wa Yosadaki, pamoja na watu wote waliokuwa wamerudi kutoka katika uhamisho wakafanya kama vile Yawe, Mungu wao alivyowaambia na kama vile walivyoambiwa na Hagai, yule nabii aliyetumwa na Yawe, Mungu wao. Watu wakamuheshimia Yawe. 13 Kisha Hagai, mujumbe wa Yawe, akawapa watu ujumbe huu kutoka kwa Yawe: Mimi niko pamoja nanyi. –Ni ujumbe wa Yawe. 14 Basi, Yawe akamutia moyo mutawala Zerubabeli wa Yuda pamoja na Kuhani Mukubwa Yoshua na watu wote waliokuwa wamerudi kutoka katika uhamisho. Wakaanza kazi hiyo ya kuijenga upya nyumba ya Yawe wa majeshi, Mungu wao, 15 katika siku makumi mbili na ine ya mwezi wa sita, mwaka wa pili wa utawala wa mufalme Dario. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo