Habakuki 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maombi ya Habakuki 1 Maombi ya nabii Habakuki: 2 Ee Yawe, nimesikia juu ya utukufu wako, juu ya matendo yako, nami ninaogopa. Uyafanye tena mambo yale wakati wetu; uyafanye yajulikane wakati huu wetu. Unapokasirika tafazali ukumbuke huruma yako! 3 Mungu amekuja kutoka jimbo la Temani, Mungu mutakatifu anakuja kutoka mulima Parani. Utukufu wake umeenea pote mbinguni, nayo dunia imejaa sifa zake. 4 Anangaa kama jua; mishale ya mwangaza inatoka katika mukono wake ambamo nguvu yake inajificha. 5 Ugonjwa mukali unatangulia mbele yake, nyuma yake hasara inafuata. 6 Akisimama dunia inatikisika; akiyatupia mataifa jicho, hayo yanatetemeka. Milima ya milele inavunjwavunjwa, vilima vya zamani za kale vinaanguka; ni juu yao kulipokuwa njia zake za kale na kale. 7 Niliwaona watu wa Kusani wakiteseka, na watu wa Midiani wakitetemeka. 8 Ee Yawe, umeikasirikia mito? Umeyakasirikia maji ya bahari? Ulipanda juu ya gari lako la vita na kuendesha farasi kwa kupata ushindi. 9 Uliuweka tayari upinde wako, ukaweka mishale yako kwenye kamba. Uliupasua udongo kwa mito. 10 Milima ilikuona, ikanyauka; mafuriko ya maji yakapita mule. Vilindi vya bahari vilinguruma, na kurusha juu mawimbi yake. 11 Jua na mwezi vilikaa kimya katika makao yao, vilipoona mwangaza wa mishale yako ikienda mbio, vilipouona mukuki wako ukimetameta. 12 Kwa kasirani ulipita juu ya inchi, uliyakanyaga mataifa kwa hasira yako. 13 Ulitoka kwenda kuwaokoa watu wako, kumwokoa yule uliyemusimika kwa kumupakaa mafuta. Ulimuponda mutawala wa jamii ya waovu, ukawaangamiza kabisa wafuasi wake. 14 Umetoboa vichwa vya wakubwa wao kwa mikuki yao wenyewe, waliotufikia kama zoruba kututawanya, wakijivuna kwa kuwameza wamasikini kwa siri. 15 Kwa farasi wako ulitembea juu ya bahari, bahari inayosukwasukwa na mawimbi. 16 Nikasikia hayo, matumbotumbo yangu yakatetemeka. Midomo yangu inatetemeka kwa hofu, mifupa yangu inateguka, miguu yangu inatetemeka. Ninangojea kwa utulivu siku ile ya hasara, ambayo inawafikia wale wanaotushambulia. 17 Hata kama miti ya tini isipochanua maua wala mizabibu kuzaa zabibu, hata kama mizeituni isipozaa zeituni na mashamba yasipotoa chakula, hata kama kondoo wakitoweka katika zizi na nyama wa kufugwa kukosekana katika mazizi, 18 mimi nitaendelea kumufurahia Yawe. Nitamushangilia Mungu anayeniokoa. 19 Bwana, Yawe ndiye nguvu yangu, anaimarisha miguu yangu kama ya paa, ananiwezesha kupita juu katika milima. Kwa mwimbishaji: pamoja na ala za muziki wa nyuzi. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo