Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Habakuki 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Mimi nitasimama pahali pa kuchungulia, na kuikaa juu katika munara; nitakaa macho wazi nipate kuona ataniambia nini, atajibu nini juu ya malalamiko yangu.


Mungu anamujibu Habakuki

2 Kisha, Yawe akanijibu hivi: Uyaandike maono haya; uyaandike wazi juu ya vibao, anayepitia pale apate kuyasoma haraka.

3 Maono haya yanangoja wakati uliopangwa; ni maono ya ukweli juu ya mwisho. Kama yanaonekana kuchelewa, uyangojee; hakika yatafika, wala hayatachelewa.

4 Andika: Uwaangalie wenye kiburi, hao wataangamia; lakini wenye haki wataishi kwa kumwamini Mungu.


Waovu wataangamia

5 Zaidi ya hayo, divai inapotosha; mutu mwenye kiburi hatadumu. Yuko tayari kuwameza wengine kama kuzimu; kama vile kifo, hatosheki na kitu. Anajikusanyia mataifa yote, na watu wote kama mali yake.

6 Kila mutu atamuchekelea mutu wa namna hiyo na kumutungia misemo ya kitambi: Ole wako unayejilundikia visivyokuwa vyako, na kutwaa rehani mali za watu lakini haulipi! Utaendelea kufanya hivyo mpaka wakati gani?

7 Siku moja wale waliokukopesha watasimama kwa rafla, wale wanaokutetemesha wataamuka. Halafu utakuwa mateka wao.

8 Wewe umenyanganya mataifa mengi, lakini wote wanaobaki watakunyanganya wewe, kwa mauaji na mateso uliyoitendea dunia, uliyoifanyia miji na wakaaji wake wote.

9 Ole wako unayejitajirisha kwa hasara ya mwingine, unayejenga nyumba yako juu katika milima ukizani kuwa salama mbali na hasara.

10 Lakini kwa mipango yako umefezehesha jamaa lako. Kwa kuyaangamiza mataifa mengi, umeyaangamiza maisha yako mwenyewe.

11 Ndiyo maana hata mawe yatalalamika juu ya ukuta, na miti ya nyumba itayaunga mukono.

12 Ole wako unayejenga muji kwa mauaji unayesimika kijiji kwa maovu!

13 Yawe wa majeshi anasababisha juhudi za watu zipotelee katika moto, na mataifa yajishugulishe bure.

14 Utukufu wa Yawe utaenea pote katika dunia, kama vile maji yanavyoenea katika bahari.

15 Ole wako unayewalewesha jirani zako, na kutia sumu katika divai yao kusudi upate kuwaona wakiikaa uchi.

16 Utajaa haya pahali pa heshima. Utakunywa wewe mwenyewe na kupepesuka! Yawe mwenyewe atakulewesha, na haya itaifunika heshima yako!

17 Mateso uliyoyatenda kule Lebanoni yatakulemea wewe; uliwaua nyama, nyama nao watakuogopesha. Yote hayo yatakupata wewe, kwa mauaji na mateso uliyoitendea dunia, uliyoifanyia miji na wakaaji wake wote.

18 Sanamu mutu aliyotengeneza inafaa kwa nini? Sanamu ni madini yaliyoyeyushwa, ni kitu cha kueneza udanganyifu! Mutengenezaji wa sanamu anatumainia kile alichotengeneza mwenyewe, sanamu ambayo haiwezi hata kusema!

19 Ole wake mutu anayeambia kipande cha muti: Amuka! au jiwe bubu: Simama! Sanamu inaweza kumufundisha mutu? Angalia imepakwa zahabu na feza, lakini haina uzima wowote.

20 Lakini Yawe yuko katika hekalu lake takatifu; dunia yote ikae kimya mbele yake.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan