Habakuki 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Haya ni maono ambayo nabii Habakuki aliyofunuliwa na Mungu. Malalamiko ya nabii 2 Ee Yawe, nitakulilia mpaka wakati gani, nawe usinisikilize na kunisaidia? Kwa nini ninalia “Mateso makali!” nawe hautuokoi? 3 Kwa nini unaniachilia kuona mabaya na taabu? Uharibifu na mateso makali vinanizunguka, ugomvi na mabishano yanatokea. 4 Hivyo sheria haina nguvu, wala haki haifuatiliwi. Waovu wanawazunguka wenye haki, hivyo hukumu inatolewa na sheria imepotoshwa. Jibu la Mungu 5 Mungu akasema: Muangalie mataifa, muone! Mustaajabu na kushangaa. Maana ninatenda kitu ukiwa bado unaishi, kitu ambacho ungeambiwa haungesadiki. 6 Maana ninawachochea Wakaldea, taifa lile kali na lenye nguvu, taifa linalopita katika inchi yote, kwa kunyanganya makao ya watu wengine. 7 Wao ni watu wa kuchukiza na kutisha; wao wanajiamulia sheria wenyewe na kujipatia mamlaka. 8 Farasi wao ni wepesi kuliko chui, wakali kuliko imbwa wa pori wenye njaa. Waaskari wapanda-farasi wao wanatoka mbali, wanaruka mbio kama tai anavyorukia nyama. 9 Wote wanakuja kwa kutesa kwa ukali; wanafukuzia wakikaza macho mbele, wanakusanya wafungwa wengi kama muchanga. 10 Wanawachekelea wafalme, na kuwazarau watawala. Kila kuta kwao ni muzaha, wanailundikia udongo na kuiteka. 11 Kisha wanasonga mbele kama upepo, wanapita na kufanya makosa. Nguvu zao ndio mungu wao! Habakuki analalamika tena 12 Wewe si ndiwe Yawe, tangu zamani sana? Wewe ndiwe Mungu wangu, Mutakatifu wangu, usiyekufa. Ee Yawe, umewachagua Wakaldea watuhukumu! Ewe kimbilio letu, umewaimarisha kusudi watuazibu! 13 Wewe ni mutakatifu kabisa, hauwezi kutazama uovu, hauwezi kuvumilia hata kidogo kuona mabaya. Mbona basi unawaona wafanya maovu na kunyamaza, kwa nini unanyamaza waovu wanapowamaliza wale watu wanaokuwa wenye haki kuliko wao? 14 Umewafanya watu kama samaki katika bahari, kama viumbe vinavyotambaa visivyokuwa na mwongozi! 15 Wakaldea wanawavua watu kwa ndoana, wanawakokotea inje kwa nyavu zao, wanawakusanya wote katika wavu wao, kisha wanafurahi na kushangilia. 16 Kwa hiyo, wanazitambikia nyavu zao, na kuzifukizia ubani; maana kwa njia ya vitu hivyo mapato yao yanaongezeka, na wanakuwa na chakula kingi. 17 Hawataacha hata kidogo kuvuta upinde wao? Wataendelea tu kuwanasa watu, na kuyaangamiza mataifa bila huruma? |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo