Ezra 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ezra anafika Yerusalema Pasaka 1 Nyuma ya mambo yale, wakati wa utawala wa mufalme Artasasta wa Persia, kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Ezra. Ezra alikuwa mwana wa Seraya mwana wa Azaria mwana wa Hilkia 2 mwana wa Salumu mwana wa Zadoki mwana wa Ahitubu 3 mwana wa Amaria mwana wa Azaria mwana wa Merayoti 4 mwana wa Zerahia mwana wa Usi mwana wa Buki 5 mwana wa Abisua mwana wa Finehasi mwana wa Eleazari mwana wa Haruni, Kuhani Mukubwa. 6 Ezra akaondoka Babeli, yeye alikuwa mwandishi mwenye ujuzi mwingi sana katika Sheria ambayo Yawe, Mungu wa Israeli, alikuwa amemupatia Musa. Na kwa musaada wa Yawe, Mungu wake, mufalme alimupatia Ezra kila kitu alichohitaji. 7 Katika mwaka wa saba wa utawala wa mufalme Artasasta, Ezra akafunga safari kutoka Babeli kwenda Yerusalema. Alikwenda pamoja na watu wamoja wa Israeli, makuhani, Walawi, waimbaji, walinzi wa milango na watumishi wa hekalu. 8 Wakafika Yerusalema katika siku ya kwanza ya mwezi wa tano katika mwaka wa saba wa utawala wa mufalme Artasasta. 9 Yawe akaifanikisha sana safari yao waliyokuwa wameianza siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza. 10 Ezra alikuwa amejitoa kwa moyo wote kujifunza Sheria ya Yawe, kuitii na kuwafundisha watu wa Israeli masharti na maagizo zake. Barua kutoka kwa Artasasta 11 Huu ndio mufano wa barua ambayo Artasasta alimupa Ezra, kuhani na mwandishi, na mwenye ujuzi katika amri na masharti ambayo Yawe aliwapa watu wa Israeli. 12 Mimi Artasasta, mufalme wa wafalme, ninatuma barua hii kwa Ezra, kuhani na mutu mwenye ujuzi katika Sheria ya Mungu wa mbinguni. 13 Ninaamuru kwamba katika utawala wangu, Mwisraeli yeyote, au kuhani wao, au Mulawi, akitaka kurudi Yerusalema kwa mapenzi yake, anaweza kwenda pamoja nawe. 14 Mimi pamoja na washauri wangu saba, tunakutuma uende ufanye uchunguzi kule Yuda na Yerusalema kuona kama Sheria ya Mungu wako ambayo umepewa inafuatwa kikamilifu. 15 Utatwaa feza na zahabu ambayo mimi na washauri wangu tumemutolea kwa utashi wetu Mungu wa Israeli ambaye hekalu lake liko katika muji Yerusalema. 16 Utatwaa vilevile feza na zahabu yote utakayokusanya katika jimbo lote la Babeli, pamoja na matoleo ya mapenzi Waisraeli na makuhani wao waliyotoa kwa ajili ya nyumba ya Mungu wao inayokuwa Yerusalema. 17 Feza hiyo utaitumia kwa uangalifu sana kwa kununua ngombe dume, kondoo dume, wana-kondoo na sadaka ya unga na divai, na kuvitoa kwenye mazabahu katika nyumba ya Mungu wenu inayokuwa Yerusalema. 18 Feza na zahabu itakayobaki unaweza kuitumia pamoja na wanainchi wenzako kama vile mutakavyopenda, kufuatana na mapenzi ya Mungu. 19 Vyombo ambavyo umepewa kwa ajili ya ibada ya nyumba ya Mungu wako, utamutolea Mungu wa Yerusalema. 20 Ukihitaji kitu kingine chochote kwa ajili ya nyumba ya Mungu wako unaweza kukipata kutoka katika hazina ya mufalme. 21 Mimi mufalme Artasasta, ninatoa amri kwa walinzi wa hazina wote katika jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati kwamba kitu chochote Ezra atakachohitaji, kuhani na mwandishi wa Sheria ya Mungu wa mbinguni, mutamupa, tena bila kusita, 22 feza kiasi anachotaka mpaka kufikia kilo elfu tatu mia ine, ngano kilo elfu kumi, divai litre elfu mbili, mafuta litre elfu mbili, na chumvi kiasi chochote atakachohitaji. 23 Kila kitu Mungu wa mbinguni alichoagiza kwa ajili ya nyumba yake, kinapaswa kutimizwa kikamilifu, kusudi asipate kukasirikia ufalme wangu au wana wangu. 24 Tunawafahamisha tena kwamba inakatazwa kuwadai kodi ya mapato, malipo ya kuvuka mupaka na mengine makuhani, Walawi, waimbaji, walinzi wa mulango, wafanyakazi au watumishi wengine wa nyumba hii ya Mungu. 25 Nawe Ezra, kwa kutumia hekima Mungu wako aliyokupa, hiyo unayokuwa nayo, chagua wanasheria, na waamuzi watakaowaongoza wakaaji wote wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati ambao wanaishi kufuatana na Sheria ya Mungu wako. Na yule ambaye haijui Sheria hiyo, umufundishe. 26 Mutu yeyote ambaye hatatii Sheria ya Mungu wako na ya mufalme, ahukumiwe mara moja: kufa, kuhamishwa, kunyanganywa mali yake au kufungwa. Ezra anamusifu Mungu 27 Ezra akasema: “Asifiwe Yawe, Mungu wa babu zetu, ambaye amemupatia mufalme moyo wa kupamba nyumba ya Yawe inayokuwa Yerusalema. 28 Kwa wema wa Mungu, nimepata musaada wa mufalme na wakubwa wake wenye uwezo mukubwa. Nilipata nguvu kwa sababu Yawe, Mungu wangu, alikuwa pamoja nami, hata nikawakusanya viongozi wa Israeli kusudi warudi pamoja nami.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo