Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Ezra 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Ujenzi wa hekalu unapingwa

1 Kisha waadui za watu wa Yuda na Benjamina waliposikia kwamba watu waliorudi kutoka katika uhamisho wanalijenga upya hekalu la Yawe, Mungu wa Israeli,

2 wakamwendea Zerubabeli na viongozi wa ukoo, na kumwambia: “Tafazali tushirikiane katika ujenzi wa hekalu. Sisi kama vile ninyi tunamwabudu Mungu wenu, na tumekuwa tukimutolea sadaka tangu zamani za Esari-Hadoni, mufalme wa Asuria aliyetuleta hapa.”

3 Lakini Zerubabeli, Yesua na viongozi wengine wa ukoo za Waisraeli wakawaambia: “Sisi hatuhitaji musaada wowote kutoka kwenu kwa kuijenga nyumba ya Mungu wetu. Sisi wenyewe tutamujengea Yawe, Mungu wa Israeli, kama vile mufalme Kiro wa Persia alivyotuamuru.”

4 Hapo, watu waliokuwa wanaishi pahali pale wakaanza kuwavunja moyo na kuwatisha Wayuda kusudi wasiendelee kama walivyokusudia.

5 Tena wakawalipa wakubwa wa serikali ya Persia kituliro kusudi wapinge kazi ya Wayuda. Wakaendelea kufanya hivyo muda wote wa utawala wa Kiro, mpaka wakati wa utawala wa Dario.


Ujenzi mupya wa Yerusalema unapingwa

6 Kwa mwanzo wa utawala wa mufalme Ahasuero, waadui za watu waliokaa Yuda na Yerusalema wakaandika mashitaki juu yao.

7 Tena wakati wa utawala wa Artasasta, mufalme wa Persia, Bisilamu, Mitiredati, Tabeli na warafiki zao, wakamwandikia barua mufalme Artasasta. Barua hiyo iliandikwa katika herufi za Kiaramea na kutafsiriwa.

8 Vilevile mutawala Rehumu na Simusayi, karani wa jimbo, wakamwandikia Artasasta barua hii juu ya Yerusalema:

9 Hii barua inatoka kwa mutawala Rehumu na kwa Simusayi, karani wa jimbo pamoja na wenzetu, na waamuzi, wakubwa wote ambao pale mbele walitoka Ereki, Babeli, Susani, Dini, Afarsati, Terpeli, Deha na Elamu,

10 pamoja na watu wa mataifa mengine ambao Asurbanipali, mutu mukubwa na mwenye nguvu akawahamisha na kuwaweka katika muji wa Samaria na pahali pengine katika jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati.

11 Kwa mufalme Artasasta: Sisi watumishi wako katika jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, tunakutumia salamu.

12 Tungependa ufahamu, ewe mufalme, kwamba Wayuda waliokuja hapa kutoka maeneo mengine ya ufalme wako wamekwenda Yerusalema na wanaujenga upya muji huo wa waasi na waovu. Wanamalizia kujenga kuta zake na kutengeneza musingi.

13 Tungependa ufahamu, ewe mufalme, kwamba muji huu ukijengwa upya na kuta zake zikimalizika, watu hawatalipa kodi, malipo ya kuvuka mipaka, na mengine mbalimbali na hazina yako itapunguka.

14 Sasa, kwa sababu ni mapaswa yetu ee mufalme, hatungependa kuona ukivunjiwa heshima, ndiyo maana tumeona ni vizuri tukuarifu

15 kusudi ufanye uchunguzi katika kitabu cha habari za babu zako. Humo utagundua kwamba tangu zamani, muji huu ulikuwa wa waasi na umewasumbua sana wafalme na watawala wa majimbo, na kuwa tangu zamani watu wake ni wachochezi sana; ndiyo sababu muji huo uliangamizwa.

16 Kwa hiyo tunakujulisha kwamba ikiwa muji huu utajengwa upya na kuta zake zikimalizika, hautaweza kutawala jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati.

17 Kisha mufalme akatuma jibu hili: Kwa mutawala Rehumu, kwa Simusayi, karani wa jimbo, pamoja na wenzenu wote wanaoishi Samaria na pahali pengine katika jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati.

18 Barua muliyonitumia imetafsiriwa na kusomwa mbele yangu.

19 Nimetoa amri uchunguzi ufanyike na imegunduliwa kuwa ni kweli kwamba tangu zamani muji huu wa Yerusalema umekuwa ukiwapinga wafalme na kwamba watu wake wamekuwa waasi na wachochezi wakubwa.

20 Wafalme wenye nguvu wamepata kuutawala muji ule pamoja na jimbo la upande wa magaribi wa Furati wakilipisha kodi, malipo ya kuvuka mipaka na mengine.

21 Kwa hiyo, mutoe amri watu hao waache kuujenga upya muji ule mpaka pale nitakapotoa maagizo mengine.

22 Tena, muangalie sana musichelewe kufanya hivyo, kusudi nisipate hasara.

23 Mara tu waliposomewa barua hii kutoka kwa Artasasta, Rehumu, karani Simusayi na wenzao wakaharakisha kwenda Yerusalema na kuwalazimisha kwa nguvu Wayuda waache kuujenga muji.


Ujenzi wa hekalu unaanza tena

24 Kazi ya kuijenga upya nyumba ya Mungu katika Yerusalema ilisimama, na hali hiyo ikaendelea mpaka mwaka wa pili wa utawala wa Dario, mufalme wa Persia.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan