Ezra 10 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wanawake wa kigeni wanafukuzwa 1 Wakati Ezra alipokuwa anaomba na kuungama naye akilia na kujiangusha uso mpaka chini mbele ya nyumba ya Mungu, kundi kubwa la watu wa Israeli, wanaume, wanawake na watoto, wakakusanyika karibu naye wakilia kwa uchungu mwingi. 2 Halafu Sekania mwana wa Yehieli, wa ukoo wa Elamu, akamwambia Ezra: “Tumekosa uaminifu kwa Mungu kwa kuoa wanawake wa kigeni wa inchi hii, lakini hata hivyo bado kuna tumaini kwa ajili ya Israeli. 3 Kwa hiyo, tufanye agano na Mungu wetu, tuachane na wanawake hawa pamoja na watoto wao, kwa kufuatana na shauri lako na la wengine wanaotii amri za Mungu. Yote yatendeke kwa kufuatana na Sheria. 4 Amuka utende, sisi tutakuunga mukono. Kwa hiyo ujipe moyo ufanye hivyo.” 5 Ezra akasimama na kuanza kuwaapiza makuhani, viongozi, Walawi na Waisraeli wengine wote kwamba watafanya kama ilivyosemwa, nao wakakubali kufanya kiapo. 6 Kisha, Ezra akaondoka mbele ya nyumba ya Mungu, akaenda kwa nyumba ya Yehohanani mwana wa Eliasibu. Kule, Ezra akalala usiku kucha bila kula wala kunywa maji, kwa huzuni aliyokuwa nayo juu ya ukosefu wa imani ya watu waliotoka katika uhamisho. 7 Tangazo likatolewa kila pahali katika inchi ya Yuda na Yerusalema kwa wote waliotoka katika uhamisho kwamba wakusanyike Yerusalema. 8 Ikiwa mutu yeyote atashindwa kufika katika muda wa siku tatu, kulingana na amri iliyotolewa na viongozi, mali yake yote itanyanganywa, naye mwenyewe atatengwa mbali na makutano na jamii ya watu waliorudi kutoka katika uhamisho. 9 Katika siku hizo tatu, kwa siku ya makumi mbili ya mwezi wa tisa, watu wote walioishi katika majimbo ya Yuda na Benjamina wakafika Yerusalema na kukusanyika katika kiwanja cha nyumba ya Mungu. Watu wote walikuwa wakitetemeka kwa sababu ya shauri waliloitiwa na kwa ajili ya mvua nyingi iliyokuwa ikinyesha. 10 Kuhani Ezra akasimama kwa kuzungumuza na watu, akawaambia: “Hamukukuwa waaminifu kwa kuoa wanawake wa kigeni, na hivyo mumeiongezea Israeli kosa. 11 Sasa, mutubu zambi zenu mbele ya Yawe, Mungu wa babu zenu, na kufanya yale yanayomupendeza. Mujitenge na wakaaji wa inchi hii na kuwaacha wake zenu wa kigeni.” 12 Watu wote wakasema kwa sauti na kujibu kwa pamoja: “Ni sawa! Tunapaswa kufanya kama vile unavyosema.” 13 Lakini wakaongeza kusema: “Watu ni wengi na mvua inanyesha sana. Hatuwezi kuendelea kusimama hapa katika kiwanja, na hili si jambo ambalo litamalizika kwa siku moja au mbili! Tumefanya kosa kubwa sana juu ya shauri hili. 14 Afazali wakubwa wetu wabaki Yerusalema kushugulikia jambo hili kwa ajili ya watu wote. Kisha, kila mumoja ambaye ameoa mwanamuke wa kigeni akuje kwa zamu pamoja na viongozi na waamuzi wa muji wake, mpaka pale kasirani kali ya Mungu wetu itakapoondolewa kwetu.” 15 Hakuna aliyepinga mupango huu, isipokuwa tu Yonatani mwana wa Asaeli na Yazeya mwana wa Tikwa, nao wakaungwa mukono na Mesulamu na Mulawi Sabetayi. 16 Watu wote waliorudi kutoka katika uhamisho wakakubali mupango huo, kwa hiyo kuhani Ezra akawachagua wanaume kati ya viongozi wa ukoo mbalimbali na kuyaandika majina yao. Kwa siku ya kwanza ya mwezi wa kumi, watu hao wakaanza kazi yao ya uchunguzi wa shauri hilo. 17 Siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, walikuwa wamekwisha kumaliza uchunguzi wao juu ya wanaume wote waliokuwa wameoa wanawake wa kigeni. Wanaume waliooa wanawake wa kigeni 18 Hawa ndio makuhani waliooa wanawake wa kigeni: Wazao wa Yesua, wana wa Yehosadaki na wandugu zake: Maseya, Eliezeri, Yaribu na Gedalia. 19 Hao waliahidi kuwaacha wake zao, na wakatoa kondoo dume kuwa sadaka kwa ajili ya kosa yao. 20 Wazao wa Imeri: Hanani na Zebadia. 21 Wazao wa Harimu: Maseya, Elia, Semaya, Yehieli na Uzia. 22 Wazao wa Pashuri: Eliyoenayi, Maseya, Isimaeli, Netaneli, Yozabadi na Elasa. 23 Kati ya Walawi kulikuwa: Yozabadi, Simei, Kelaya (aliyejulikana pia kwa jina la Kelita), Petahia, Yuda na Eliezeri. 24 Kati ya waimbaji kulikuwa: Eliasibu. Walinzi wa milango: Salumu, Telemu na Uri. 25 Kati ya watu wengine wa Israeli kulikuwa: Wazao wa Parosi: Ramia, Izia, Malkia, Miyamini, Eleazari, Malkia na Benaya. 26 Wazao wa Elamu: Matania, Zakaria, Yehieli Abudi, Yeremoti na Elia. 27 Wazao wa Zatu: Eliyoenayi, Eliasibu, Matania, Yeremoti, Zabadi na Aziza. 28 Wazao wa Bebayi: Yehohanani, Hanania, Zabayi na Atilayi. 29 Wazao wa Bani: Mesulamu, Maluki, Adaya, Yasubu, Seali na Yeremoti. 30 Wazao wa Pahati-Moabu: Adina, Kelali, Benaya, Maseya, Matania, Besaleli, Binui na Manase. 31 Wazao wa Harimu: Eliezeri, Isia, Malkia, Semaya, Simeoni, 32 Benjamina, Maluki na Semaria. 33 Wazao wa Hasumu: Matenayi, Matata, Zabadi, Elifeleti, Yeremayi, Manase na Simei. 34 Wazao wa Bani: Madayi, Amuramu, Ueli, 35 Benaya, Bedeya, Keluhi, 36 Wania, Meremoti, Eliasibu, 37 Matania, Matenayi na Yasu. 38 Wazao wa Binui: Simei, 39 Selemia, Natani, Adaya, 40 Makinadebayi, Sasayi, Sarai, 41 Azareli, Selemia, Semaria, 42 Salumu, Amaria na Yosefu. 43 Wazao wa Nebo: Yeieli, Matitia, Zabadi, Zebina, Yadai, Yoeli na Benaya. 44 Hao wote walioa wanawake wa kigeni na wamoja kati yao walizaa na wanawake wale. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo