Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Ezekieli 8 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Ibada za sanamu katika Yerusalema

1 Katika mwaka wa sita, siku ya tano ya mwezi wa sita tangu tulipopelekwa katika uhamisho, nilikuwa nikiikaa ndani ya nyumba yangu pamoja na wazee wa Yuda. Basi, kwa rafla nikajazwa na uwezo wa Yawe.

2 Nilipoangalia, nikaona kitu kilichofanana na mwanadamu. Sehemu yake ya chini, iliyoonekana kama ndio kiuno chake, ilikuwa kama moto. Toka kiuno chake kwenda juu alimetameta kama vile shaba.

3 Basi, akanyoosha kitu kinachokuwa kama vile mukono, akanikamatia kwa nywele zangu. Roho wa Mungu akaninyanyua kati ya dunia na mbingu, akanipeleka mpaka Yerusalema nikiwa katika maono hayo ya Mungu. Nikafika kwenye kiingilio cha mulango wa baraza ya ndani inayoelekea upande wa kaskazini, pahali palipowekwa sanamu iliyomuletea Mungu wivu.

4 Utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa hapo; nao ulikuwa kama utukufu ule niliouona katika maono kule katika bonde.

5 Kisha Mungu akaniambia: Wewe mwanadamu, angalia upande wa kaskazini. Nami nikaangalia upande wa kaskazini, na huko upande wa kaskazini wa mulango wa mazabahu, niliona ile sanamu iliyomuchukiza Mungu.

6 Basi, Mungu akaniambia hivi: Wewe mwanadamu, unaona mambo wanayofanya, machukizo makubwa Waisraeli wanayofanya kusudi wapate kunifukuza kutoka katika hekalu langu? Tena utaona machukizo mengine makubwa zaidi.

7 Kisha akanipeleka mpaka kwenye mulango wa kuingilia ndani ya uwanja. Nilipoangalia nikaona tundu juu ya ukuta.

8 Naye akaniambia hivi: Wewe mwanadamu, toboa ukuta huu. Nami, nikatoboa, nikaona kulikuwa mulango.

9 Tena akaniambia: Ingia ndani uangalie machukizo mabaya wanayofanya humo.

10 Basi, nikaingia, nikaona vitu vya kuchukiza vimechorwa kuzunguka ukuta: kila aina ya nyama wanaotambaa, vidudu, na sanamu zote za miungu ya Waisraeli.

11 Na mbele yao kulikuwa wazee makumi saba wa taifa la Waisraeli pamoja na Yazania mwana wa Safanu. Kila mumoja alikuwa na chetezo katika mukono, na moshi wa ubani ulipanda juu.

12 Kisha Mungu akaniambia: Wewe mwanadamu, umeona mambo wazee wa Waisraeli wanayotenda kwa uficho, kila mutu katika chumba chake cha sanamu. Wanasema: Yawe hatuoni. Yawe ameiacha inchi.

13 Tena akaniambia: Utaona tena machukizo makubwa zaidi wanayotenda.

14 Kisha akanipeleka mpaka kwenye mulango wa upande wa kaskazini wa nyumba ya Yawe. Huko kulikuwa wanawake wameikaa wakimwombolezea mungu Tamuzi.

15 Mungu akaniambia: Wewe mwanadamu, umeyaona hayo? Utaona tena machukizo mengine makubwa kuliko hayo.

16 Kisha akanipeleka mpaka katika uwanja wa ndani wa nyumba ya Yawe. Huko kwenye mulango wa hekalu, kati ya baraza na mazabahu, kulikuwa wanaume yapata makumi mbili na watano, wakigeuzia mugongo wao upande wa hekalu, na nyuso zao zikielekea upande wa mashariki. Walikuwa wanaabudu jua wakielekea upande wa mashariki.

17 Mungu akaniambia: Wewe mwanadamu, umeyaona mambo hayo? Hata hivyo, watu wa Yuda wanaona machukizo hayo kuwa ni kidogo. Wanajaza mateso makali katika inchi na kuzidi kunikasirikisha. Angalia jinsi wananichukiza!

18 Kwa sababu ya mambo hayo watasikia uzito wa kasirani yangu. Sitamwacha hata mutu mumoja aponyoke wala sitamwonea huruma mutu yeyote. Hata wakinililia kwa sauti kubwa mimi sitawasikiliza.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan