Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Ezekieli 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Azabu ya mwisho ya Waisraeli

1 Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

2 Wewe mwanadamu, uwaambie wakaaji wa inchi ya Israeli kwamba Bwana wenu Yawe anasema hivi: Ni Mwisho! Mwisho umeifikia inchi yote, kutoka pande zote ine!

3 Sasa mwisho umewafikia; sasa mutausikia ukali wa hasira yangu juu yenu. Nitawahukumu kufuatana na mwenendo wenu. Nitawaazibu kwa ajili ya machukizo yenu yote.

4 Sitawaachilia wala sitawaonea huruma. Nitawaazibu kulingana na mienendo yenu, nayo machukizo yenu yangali bado kati yenu. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe.

5 Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mutapatwa na hasara! Hasara isiyoonekana bado!

6 Mwisho umekuja! Kweli, mwisho umefika! Umewafikia ninyi!

7 Enyi wakaaji wa inchi hii, maangamizi yenu yamekuja! Wakati umekuja, siku imekaribia. Hiyo ni siku ya makelele na siyo ya sauti za shangwe kwenye mulima.

8 Sasa mutausikia uzito wa hasira yangu juu yenu. Nitawahukumu kulingana na mwenendo wenu; nitawaazibu kufuatana na machukizo yenu.

9 Sitawaachilia wala sitawaonea huruma. Nitawaazibu kulingana na mienendo yenu nayo machukizo yangali bado kati yenu. Halafu mutatambua kwamba ni mimi Yawe ninayewaangamiza.

10 Muangalie, siku ile inakuja! Maangamizi yenu yamekuja. Ubaya uko kila pahali na kiburi kimepanda sana.

11 Mateso makali yanaendelea kuwa mubaya zaidi. Hakuna hata mumoja kati yenu atakayebaki, wala vitu mulivyojilundikia kwa wingi au utajiri wenu; hakutakuwa mutu mwenye heshima kati yenu.

12 Wakati umetimia, ile siku imekaribia. Mununuzi asifurahi wala muchuuzi asiomboleze; kwa sababu kasirani yangu itawaangukia watu wote.

13 Wachuuzi watahomba kabisa hata ikiwa wangali wazima. Kwa maana unabii huu ni juu ya watu wote nao hautavunjwa. Kutokana na uovu wake, mutu hatayaokoa maisha yake.

14 Baragumu imepigwa na kuwafanya wote wakuwe tayari. Lakini hakuna anayekwenda kwa vita, kwa maana kasirani yangu iko juu ya watu wote.

15 Inje kuna kifo kwa upanga na ndani ya muji kuna ugonjwa mukali na njaa. Wanaokuwa katika vijiji watakufa kwa upanga; wanaokuwa katika muji wataangamizwa na njaa na ugonjwa mukali.

16 Ikiwa kuna watu walioponyoka, watakimbilia kwenye milima kama njiwa waliotishwa katika bonde. Kila mumoja wao ataomboleza kwa ajili ya zambi zake.

17 Mikono ya kila mutu itakuwa zaifu na magoti yake yataregea kabisa.

18 Watavaa gunia, hofu itawashika, nao watapata haya na vichwa vyao vyote vitanyolewa.

19 Watatupa feza yao ndani ya barabara na zahabu yao itakuwa kama kitu kichafu. Feza na zahabu zao hazitaweza kuwaokoa katika siku hiyo ya kasirani ya Yawe; wala hawataweza kushiba au kujaza tumbo zao feza na zahabu waliyojilundikia; maana mali hiyo ndiyo iliyosababisha zambi yao.

20 Walijivuna kwa ajili ya vitu vyao vizuri vya mapambo, wakajifanyia sanamu za miungu zinazochukiza, vitu vibaya kabisa. Kwa sababu hiyo nitavifanya kuwa uchafu mbele yao.

21 Utajiri wao nitautia katika mikono ya mataifa mengine; watu waovu wa dunia wataunyanganya na kuuchafua.

22 Nitageuza uso wangu usiwaelekee; nitaachilia hekalu langu lichafuliwe. Wanyanganyi wataingia humo ndani na kulichafua.

23 Tengeneza munyororo; kwa maana inchi imejaa makosa ya umwangaji wa damu na muji umejaa mateso makali.

24 Nitaleta watu wa mataifa mabaya sana nao watarizi nyumba zao. Nitakikomesha kiburi chao, na pahali pao pa kutambikia patachafuliwa.

25 Uchungu mukali utakapowafikia, watatafuta amani, lakini haitapatikana.

26 Watapata hasara kwa mufululizo; nazo habari mbaya zitafuatana. Watamwomba nabii awatabirie. Makuhani hawatakuwa na sheria yoyote; na wazee watakosa shauri la kuwapatia.

27 Mufalme ataomboleza, mukubwa atakata tamaa na watu watatetemeka kwa hofu. Nitawatendea kufuatana na mienendo yao, nitawahukumu kama nilivyowahukumu wengine. Halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan