Ezekieli 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Azabu ya wanaoabudu sanamu 1 Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: 2 Wewe mwanadamu, uelekeze uso wako kwenye milima ya Israeli, nawe utoe unabii kwa ajili ya wakaaji wake 3 na kusema hivi: Musikilize neno la Bwana wetu Yawe, enyi wakaaji wa milima ya Israeli! Anawaambia ninyi wakaaji wenye kuwa katika milima na vilima na katika maporomoko na mabonde kwamba: Mimi mwenyewe, Bwana wenu Yawe, nitaleta upanga na kuharibu sehemu zenu zote zilizoinuka za kutambikia. 4 Mazabahu zenu zitaharibiwa na pahali penu pa kufukizia ubani patavunjwavunjwa. Wale watakaouawa nitawatupa mbele ya sanamu zenu za miungu. 5 Maiti za Waisraeli nitazilalisha mbele ya sanamu zao za miungu, na mifupa yenu nitaisambaza kandokando ya mazabahu zenu. 6 Pahali pote munapoishi, miji yenu itakuwa ukiwa na sehemu zenu zinazoinuka za kutambikia zitabomolewa, mazabahu zenu zitabomolewa na kuwa ukiwa, sanamu zenu za miungu zitavunjwa na kuharibiwa. Pahali penu pa kufukizia ubani patabomolewa na chochote mulichofanya kitatoweka. 7 Wale watakaouawa wataanguka kati yenu, nanyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe. 8 Hata hivyo, nitawaacha wengine wabaki wazima; wamoja kati yenu wataponyoka upanga nao watasambazwa katika inchi mbalimbali. 9 Halafu wale walioponyoka watanikumbuka katikati ya mataifa ambamo watakuwa wamepelekwa katika uhamisho. Nitakuwa nimewavunja moyo wao wa uzinzi ambao ulinitupilia mbali, na macho yao yaliyozini na sanamu zao. Kwa hiyo watajichukia wao wenyewe kwa sababu ya maovu na machukizo yao yote waliyoyatenda. 10 Nao watajua kwamba mimi ni Yawe; sikusema bure kwamba nitawaletea hasara hizo zote. 11 Bwana wetu Yawe akaniambia hivi: Upige mikono, piga kishindo kwa muguu na kusema: Ole kwenu Waisraeli kwa sababu ya machukizo yenu yote; kwa sababu mutakufa kwa upanga, njaa na kwa ugonjwa mukali. 12 Anayekuwa mbali sana atakufa kwa ugonjwa mukali. Anayekuwa karibu atauawa kwa upanga. Atakayekuwa amebaki na kuponyoka hayo mawili atakufa kwa njaa. Ndivyo nitakavyotimiza kasirani yangu juu yao. 13 Wakati maiti zao zitakapokuwa zimelala kati ya sanamu zao za miungu, na kwenye mazabahu zao juu ya kila mulima, chini ya kila muti wenye kivuli, chini ya kila muti wa mwalo wenye majani na popote walipotolea sadaka zenye harufu nzuri ya kuzipendeza sanamu zao za miungu. Nanyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe. 14 Nitanyoosha mukono wangu juu yao, na kuiharibu inchi yao. Tangu huko katika jangwa upande wa kusini mpaka katika muji wa Dibla kwa upande wa kaskazini, nitaifanya inchi yao kuwa matongo kabisa wasipate pahali pa kuishi. Nao watatambua kwamba mimi ni Yawe. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo