Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Ezekieli 47 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Chemichemi inayotoka katika hekalu

1 Yule mutu akanirudisha kwenye kiingilio cha hekalu. Huko, maji yalikuwa yakitoka chini ya kizingiti cha hekalu kuelekea upande wa mashariki, (kwa maana hekalu lilielekea upande wa mashariki). Maji yalikuwa yakitiririka kutoka chini ya upande wa kusini wa mulango wa hekalu, upande wa kusini wa mazabahu.

2 Kisha akanipeleka inje kwa njia ya mulango wa kaskazini. Akanizungusha kwa njia ya inje mpaka kwenye mulango wa inje, upande wa mashariki; na maji yalikuwa yanatoka upande wa kusini.

3 Yule mutu akapima kwa ufito wake, akapima metre mia tano kwenda chini upande wa mashariki, akanipitisha kwenye maji. Maji yalifika kwenye miguu tu.

4 Kisha akapima tena metre mia tano, akaniongoza kuvuka maji. Maji yakafika mpaka kwa magoti yangu. Akapima tena metre zingine mia tano, naye akaniongoza kuvuka maji. Maji yakafika mpaka kwenye kiuno changu.

5 Akapima metre mia tano zingine, na muto ukakuwa na kilindi kirefu hata sikuweza kuuvuka tena. Haikuwezekana kuuvuka lakini kwa kuogelea.

6 Yule mutu akaniambia: Wewe mwanadamu! Shika mambo hayo yote kwa uangalifu. Kisha, akanirudisha mpaka kwenye ukingo wa muto.

7 Nilipofika huko niliona miti mingi sana kwenye kingo za muto.

8 Akaniambia: Maji haya yanatiririka kupitia katika inchi mpaka katika bonde la Yordani, na yakifika huko yatayafanya maji ya bahari ya Chumvi kuwa maji mazuri.

9 Kila pahali muto huu utakapopita, kutaishi aina zote za nyama na samaki. Muto huu utayafanya maji ya bahari ya Chumvi kuwa maji baridi. Kokote utakakopita utaleta uzima.

10 Wavuvi watasimama kandokando ya bahari, na nafasi toka Engedi mpaka Eni-Eglaimu itakuwa ya kuanikia nyavu. Kutakuwa aina nyingi za samaki kama zinavyokuwa katika bahari ya Mediteranea.

11 Lakini sehemu zake zenye majimaji na tingitingi kandokando ya bahari, zitakuwa na maji mazuri. Lakini hayo yatabaki kuwa maji ya chumvi.

12 Kisha kwa ukingo wa muto huo kutaota kila namna ya miti inayotoa chakula. Majani yake hayatanyauka wala miti hiyo haitaacha kuzaa matunda. Itazaa matunda mapya kila mwezi, kwa sababu inapata maji yanayotiririka kutoka hekalu la Mungu. Matunda yake yatakuwa chakula na majani yake yatatumika kwa kuponyesha magonjwa.


Mipaka ya inchi

13 Bwana wetu Yawe anasema hivi: Hii ndiyo mipaka ya inchi mutakayoigawanyia makabila kumi na mawili ya Waisraeli. Lakini kabila la Yosefu lipewe mara mbili.

14 Ninyi wote mutagawanyana sawa. Niliapa kuwa nitawapa babu zenu inchi hii, nayo itakuwa mali yenu.

15 Upande wa kaskazini mupaka utapita kutoka bahari ya Mediteranea, kuelekea muji wa Hetiloni, hata pahali pa kuingia Hamati na kuendelea mpaka Zedada.

16 Kutoka hapo utaendelea mpaka Berota na Sibraimu (unaokuwa kati ya Damasiki na Hamati), na mpaka muji wa Hazori-Hatikoni unaokuwa katika inchi ya Haurani.

17 Hivyo mupaka utakwenda kutokea bahari ya Mediteranea kuelekea mashariki mpaka katika muji wa Hazorenoni ukipakana na maeneo ya Damasiki na Hamati kwa upande wa kaskazini.

18 Upande wa mashariki, mupaka utakuwa muto Yordani unaoelekea kati ya Haurani na Damasiki, Gileadi na inchi ya Israeli. Vilevile mupaka utapitia upande wa mashariki wa bahari ya Chumvi mpaka Tamari.

19 Upande wa kusini, toka Tamari mupaka utaendelea mpaka kwenye chemichemi ya Meriba-Kadesi. Kutoka Meriba-Kadesi mupaka utaelekea kusini magaribi mpaka bahari ya Mediteranea ukipitia upande wa mashariki ya inchi ya Misri.

20 Upande wa magaribi, mupaka ni bahari ya Mediteranea na utapanda upande wa kaskazini mpaka pahali pa kuingilia Hamati.

21 Basi, mutagawanya inchi hii kati yenu kulingana na makabila ya Waisraeli.

22 Mutaigawanya kuwa mali yenu. Wageni watakaokaa kati yenu, wale watakaozalia watoto kati yenu, wapewe vilevile sehemu ya inchi munapoigawanya. Hao wanapaswa kutendewa kama wanainchi wa Israeli na wana haki ya kupiga kura kwa kupata sehemu ya inchi pamoja na makabila ya Waisraeli.

23 Kila mugeni anayekaa nanyi atapewa sehemu yake pamoja na watu wa kabila ambamo anaishi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan