Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Ezekieli 43 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yawe anarudi katika hekalu

1 Kisha, yule mutu akanipeleka kwenye mulango unaoelekea upande wa mashariki.

2 Utukufu wa Mungu wa Israeli ulitokea upande wa mashariki. Pamoja nao kulikuwa mushindo wa kuja kwake kama mushindo wa maji mengi, inchi ilingaa kwa utukufu wake.

3 Maono hayo yalikuwa kama maono niliyoyaona wakati Mungu alipokuja kuuangamiza Yerusalema. Vilevile yalifanana na maono niliyoyaona karibu na muto Kebari. Nikaanguka uso mpaka chini.

4 Nao utukufu wa Yawe uliingia katika nyumba ya Yawe kwa njia ya mulango wa mashariki.

5 Kisha roho akanitwaa na kunipeleka kwenye kiwanja cha ndani. Nikaona utukufu wa Yawe ukiwa umeijaza nyumba ya Yawe.

6 Yule mutu akiwa anasimama karibu nami, nilisikia mutu fulani akisema nami kutoka katika nyumba ya Yawe;

7 naye akaniambia: Wewe mwanadamu! Hapa ndipo pahali pa kiti changu cha kifalme, pahali ninapoweka miguu yangu. Nitakaa kati ya watu wa Israeli milele. Na Waisraeli hawatalichafua jina langu, wao wenyewe, wala wafalme wao kwa kuziabudu sanamu au kuzika maiti za wafalme wao pahali hapa.

8 Wafalme wao walijenga vizingiti na miimo ya nyumba zao za kifalme karibu na vizingiti vya nguzo za hekalu langu, hivyo kati yangu na wao ulikuwa ni ukuta tu. Walichafua jina langu takatifu kwa machukizo yao waliyotenda, ndiyo maana nimewaangamiza kwa hasira yangu.

9 Sasa waache kuziabudu sanamu na waziondoe maiti za wafalme wao mbali nami, nami nitakaa kati yao milele.

10 Sasa, ewe mwanadamu, uwaelezee Waisraeli habari za nyumba ya Mungu na wajifunze taswira yake. Wapate haya kutokana na machukizo yao waliyotenda.

11 Wakipata haya kutokana na matendo yao, waeleze taswira ya nyumba ya Mungu: taswira yake yenyewe, milango ya kuingilia na kutokea, umbo lake lote, mipango ya kila kitu, kanuni zake na masharti yake. Uwaandikie hayo yote waziwazi kusudi waweze kuona namna yote yalivyopangwa na waweze kuzifuata kanuni na masharti yake.

12 Hii ni sheria juu ya nyumba ya Yawe: Eneo lote linalozunguka nyumba ya Yawe juu ya mulima linapaswa kuwa takatifu kabisa.


Mazabahu katika hekalu

13 Vipimo vya mazabahu, vitakuwa vilevile kama vipimo vya hekalu. Kutakuwa musingi wenye urefu wa sentimetre makumi tano na upana wa sentimetre makumi tano kuzunguka musingi wa mazabahu, pamoja na ukingo wenye urefu kuenda juu wa sentimetre makumi mbili na tano.

14 Sehemu ya mazabahu itakayokuwa chini kabisa tokea juu ya musingi itakuwa na kimo cha metre moja. Sehemu itakayofuata itawekwa nyuma kutoka kwenye ukingo sentimetre makumi tano muzunguko, na kimo cha metre mbili. Sehemu itakayofuata nayo itawekwa nyuma ya ukingo sentimetre makumi tano muzunguko.

15 Sehemu hii ya juu, ambayo itatumika kuteketezea sadaka, itakuwa muraba, kila upande metre mbili. Mujengo wa pembe za sehemu hii ya juu zitainuka kuliko sehemu zingine.

16 Sehemu ya juu ya mazabahu itakuwa muraba, metre sita kila upande.

17 Sehemu ya katikati, itakuwa muraba, sentimetre saba kila upande, nayo itakuwa na ukingo pembeni wenye kimo cha sentimetre makumi mbili na tano. Kutakuwa mufereji wenye upana wa sentimetre makumi tano. Na kutakuwa ngazi za kupandia kwenye mazabahu kila upande.


Kutakaswa kwa mazabahu

18 Bwana wetu Yawe akaniambia. Wewe mwanadamu! Yawe anasema hivi: Wakati mazabahu itakapojengwa utaitakasa, kwa kutoa sadaka za kuteketezwa juu yake na kuinyunyizia damu ya nyama waliotolewa.

19 Wale makuhani wanaokuwa wa kabila la Lawi ambao ni wazao wa Zadoki, ndio tu watakaokaribia mbele yangu kwa kunitumikia. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Utawapa ngombe dume muchanga kuwa sadaka ya kusamehewa zambi.

20 Utatwaa damu yake na kuitia juu ya pembe ine za mazabahu na juu ya chongo ine za daraja na juu ya muzunguko wake pande zote. Hivyo ndivyo utakavyoisafisha mazabahu na kuitakasa.

21 Utatwaa vilevile ngombe dume aliyetolewa kuwa sadaka ya kusamehewa zambi; watamuteketeza katika pahali palipochaguliwa ndani ya nyumba ya Yawe, lakini inje ya Pahali Patakatifu.

22 Kesho yake, utatoa beberu asiyekuwa na kilema, kuwa sadaka ya kusamehewa zambi; mazabahu itatakaswa kama ilivyotakaswa kwa damu ya ngombe dume.

23 Utakapokwisha kuitakasa, utatwaa ngombe dume mudogo asiyekuwa na kilema na kondoo dume mumoja asiyekuwa na kilema na

24 kuwaleta mbele yangu. Makuhani watawapakaa chumvi na kuwatoa kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa Yawe.

25 Kwa muda wa siku saba, kila siku utatoa beberu mumoja akuwe sadaka ya kusamehewa zambi. Vilevile watatoa ngombe dume mumoja na kondoo dume mumoja asiyekuwa na kilema.

26 Hivyo kwa muda wa siku saba, utafanya upatanisho na kuisafisha, na hivyo utatakasa mazabahu.

27 Kisha siku hizo saba, tokea siku ya nane na kuendelea, makuhani watatoa sadaka zenu za kuteketezwa na sadaka zenu za amani. Nami nitawakubali. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan