Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Ezekieli 25 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Unabii juu ya Waamoni

1 Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

2 Wewe mwanadamu! Ugeukie upande wa inchi ya Waamoni, utoe unabii juu yao.

3 Uwaambie Waamoni hivi: Musikilize neno la Bwana wetu Yawe: Ninyi mulifurahia kuona hekalu langu likichafuliwa, inchi ya Waisraeli ikiangamizwa na watu wa Yuda wakipelekwa katika uhamisho.

4 Basi, nitawatoa ninyi katika mikono ya watu wa mashariki; watapiga hema zao kati yenu na kufanya makao yao katika inchi yenu. Nao watakula matunda yenu na kunywa maziwa yenu.

5 Nitaufanya muji wa Raba kuwa nafasi ya kukulishia ngamia na inchi ya Amoni kuwa zizi la kondoo. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe.

6 Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa sababu mulipiga mikono, mukarukaruka kwa furaha na kushangilia sana juu ya inchi ya Waisraeli,

7 basi, mimi nimeunyoosha mukono juu yenu kwa kuwaazibu; nitawaacha mukamatwe mateka na watu wa mataifa mengine. Nitawaangamiza kabisa, nanyi hamutakuwa taifa tena wala kuwa na inchi. Kwa hiyo mutatambua kwamba mimi ni Yawe.


Unabii juu ya Moabu

8 Bwana wetu Yawe alisema: Kwa sababu Wamoabu wamesema kwamba watu wa inchi ya Yuda ni sawa tu na mataifa mengine,

9 mimi nitaifanya miji inayolinda mipaka ya Moabu ishambuliwe, hata miji ile bora kabisa, ni kusema Beti-Yesimoti, Bali-Meoni na Kiriataimu.

10 Nitatoa inchi hiyo pamoja na inchi ya Waamoni katika mikono ya watu wa mashariki wakuwe mali yao. Inchi ya Moabu haitakuwa taifa tena.

11 Mimi nitaiazibu inchi ya Moabu, nao watatambua kwamba mimi ni Yawe.


Unabii juu ya Waedomu

12 Bwana wetu Yawe alisema hivi: Kwa sababu Waedomu wamefanya kisasi na Yuda, wakawalipiza watu wa Yuda kisasi kibaya sana

13 basi, Bwana wetu Yawe anasema: Nitanyoosha mukono juu ya inchi ya Edomu kwa kuwaazibu na kuwaua watu wote na nyama. Nitaifanya kuwa ukiwa kutoka muji wa Temani mpaka muji wa Dedani. Watu wa inchi hiyo watauawa kwa upanga.

14 Nitawafanya watu wangu Waisraeli walipize kisasi juu ya Waedomu nao watawatendea Waedomu kadiri ya hasira na kasirani yangu. Halafu Waedomu watatambua uzito wa kisasi changu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.


Unabii juu ya Wafilistini

15 Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa sababu Wafilistini walifanya kisasi, wakawalipiza kisasi waadui zao kwa ubaya sana na kuendelea kuwa waadui zao siku zote,

16 basi, mimi Bwana wenu Yawe ninawaambia hivi: Nitanyoosha mukono juu ya Wafilistini kwa kuwaazibu; nitawaangamiza hao watu wa Kereti na wakaaji wa kandokando ya bahari.

17 Nitawalipiza kisasi kikali kwa azabu ya kasirani. Halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan