Ezekieli 23 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Samaria ni muzinzi 1 Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: 2 Wewe mwanadamu! Kulikuwa wabinti wawili, wote wa mama mumoja. 3 Katika ujana wao walipokuwa wanakaa kule Misri, wakakubali maziba yao kupapaswa, wakapoteza ubikira wao, wakafanya uzinzi. 4 Yule mukubwa aliitwa Ohola, na yule mudogo Oholiba. Basi, wote wakakuwa wangu, wakanizalia watoto, wana na wabinti. Basi, Ohola ni Samaria na Oholiba ni Yerusalema! 5 Ingawa Ohola alikuwa muke wangu, lakini aliendelea kuwa muzinzi na kuwatamani wapenzi wake Waasuria. 6 Kati yao kulikuwa waaskari, wenye kuvaa nguo za bei kali za rangi nyekundu-nyeusi, kulikuwa vilevile maliwali na waamuzi. Wote walikuwa vijana wa kuvutia na waaskari wapanda-farasi hodari. 7 Ohola alifanya uasherati na wale wakubwa wote wenye vyeo vya juu wa Waasuria, naye akajichafua kwa kuabudu sanamu zote kila mwanaume wake aliyetamani. 8 Aliendelea na uzinzi wake aliouanza kule Misri wakati huo wa ujana wake, wanaume walivunja ubikira wake na kuzitimiza tamaa zao kwake. 9 Kwa hiyo nikamutoa katika mikono ya Waasuria wapenzi wake, ambao aliwatamani sana. 10 Hao walimuvua nguo zake na kumwacha uchi. Waliwakamata watoto wake, naye mwenyewe wakamwua kwa upanga. Azabu hiyo aliyopata ikakuwa fundisho kwa wanawake wengine. 11 Dada yake Oholiba aliona jambo hilo, lakini akazidi kupotoka kuliko yeye katika tamaa yake, na uzinzi wake ulikuwa mubaya kuliko wa dada yake. 12 Aliwatamani sana Waasuria: maliwali, waamuzi, waaskari waliovaa nguo zao za kiaskari, waaskari wapanda-farasi hodari, wote wakiwa vijana wa kuvutia. 13 Nilimutambua kuwa muchafu. Kweli wote wawili walikuwa na tabia hiyo moja. 14 Lakini Oholiba alizidisha uzinzi wake; akapendezwa na picha za Wakaldea za rangi nyekundu zilizochorwa juu ya ukuta, 15 na mikaba katika viuno, vitambaa vikubwa juu ya vichwa; hizo zote zilifanana na wakubwa. Ni picha ya Wababeli, wakaaji wa inchi ya Kaldea. 16 Alipoziona picha hizo, mara moja akashikwa na tamaa, akatuma wajumbe kwenda Kaldea. 17 Basi, Wababeli wakamwendea katika kitanda cha mapenzi. Wakamuchafua kwa njia ya tamaa zao mbaya. Alipokwisha kujichafua, akajitenga nao. 18 Alipoendelea na uzinzi wake na kufunua uchi wake, mimi nilimwacha kama nilivyomwacha dada yake. 19 Hata hivyo, akazidisha uzinzi wake akifanya kama wakati wa ujana wake alipofanya uzinzi kule Misri. 20 Aliwatamani sana wanaume wenye viungo kama viungo vya punda na wenye kuwaka tamaa kama farasi dume. Muji Yerusalema utaazibiwa 21 Oholiba aliutamani uchafu wake wa ujana alipokuwa Misri, ambako Wamisri walivunja ubikira wake, na kuyapapasa maziba yake machanga. 22 Sasa Oholiba, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitawasukuma wapenzi wako, wale uliochukizwa nao wakushambulie; nitawaleta wakushambulie kutoka pande zote. 23 Nitawachochea Wababeli na Wakaldea wote, watu toka Pekodi, Soa na Koa, pamoja na Waasuria wote. Nitawachochea vijana wote wa kuvutia, maliwali, waamuzi, majemadari na waaskari wote wakiwa wapanda-farasi. 24 Watakuja kutoka upande wa kaskazini, pamoja na magari ya vita na ya mizigo, wakiongoza kundi kubwa la watu. Watakuzunguka pande zote kwa ngao kubwa na ndogo na kofia za chuma. Nimewapa uwezo wa kukuhukumu, nao watakuhukumu kadiri ya sheria zao. 25 Nami nitakuelekezea kasirani yangu, nao watakutendea kwa hasira kali. Watakukata pua na masikio na watu wako watakaobaki watauawa kwa upanga. Watawatwaa wana na wabinti zako, na watu wako watakaobaki watateketezwa kwa moto. 26 Watakuvua nguo zako na kukunyanganya vitu vyako vizuri vya bei kali. 27 Nitaukomesha uasherati na uzinzi wako ulioufanya tangu ulipokuwa kule Misri. Hautaziangalia sanamu zozote tena wala kuifikiria tena inchi ya Misri. 28 Kweli, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitakutia katika mikono ya watu unaowachukia, watu unaowaona kuwa kinyaa. 29 Kwa vile wanakuchukia, watakunyanganya matunda yote ya kazi yako na kukuacha uchi, bila nguo na kuonyesha haya ya uzinzi wako. Uzinzi wako na uasherati wako 30 ndivyo vilivyokuletea hali hiyo. Wewe ulizini na mataifa, ukajichafua kwa kuabudu miungu yao. 31 Kwa sababu ulifuata njia ya dada yako, basi, mimi nitakupa kikombe kilekile cha azabu ukikunywe. 32 Bwana wetu Yawe anasema hivi: Utakunywa toka kikombe cha dada yako; kikombe kikubwa na kirefu. Watu watakuchekelea na kukuzarau; na kikombe chenyewe kimejaa. 33 Kitakulewesha na kukuhuzunikisha sana. Kikombe cha dada yako Samaria, ni kikombe cha hofu na maangamizi. 34 Utakikunywa na kukimaliza kabisa; utakipasua vipandevipande kwa meno, na kurarua navyo maziba yako. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. 35 Kwa hiyo Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa kuwa umenisahau na kunigeuzia mugongo, basi, utabeba muzigo wa uasherati na uzinzi wako. Hukumu ya Mungu juu Samaria na Yerusalema 36 Yawe aliniambia: Wewe mwanadamu! Uko tayari kuwahukumu Ohola na Oholiba? Basi, uwatangazie matendo yao ya kuchukiza! 37 Wamefanya uzinzi na mauaji. Wamefanya ukahaba kwa sanamu zao, hata kuzitambikia watoto walionizalia wao wenyewe. 38 Tena si hayo tu! Wamekufuru hekalu langu na kuvunja Sabato zangu. 39 Siku ileile walipozitambikia watoto wao wenyewe kwa sanamu, waliingia Pahali Patakatifu pangu kusudi wapachafue. Hayo ndiyo waliyofanya katika nyumba yangu. 40 Hata walituma wajumbe wawaite watu wa mbali, nao wakakuja. Kwa ajili yao, walikoga, wakajitia wanja na kuvaa vitu vya kujipamba. 41 Kisha wakaikaa kwenye vitanda vizurivizuri, na mbele yao meza imetandikwa. Juu ya meza hiyo uliweka ubani wangu na mafuta yangu. 42 Basi, kukasikilika sauti za kundi la watu wasiojali kitu, kundi la wanaume walevi walioletwa kutoka katika jangwa. Waliwavalisha hao wanawake vikomo kwa mikono yao na taji nzuri juu ya vichwa vyao. 43 Halafu nikasema: Wanazini na mwanamuke aliyechakaa kwa uzinzi. 44 Kila mumoja alimwendea kama wanaume wanavyomwendea kahaba. Ndivyo walivyowaendea Ohola na Oholiba wale wanawake waasherati. 45 Lakini waamuzi wa haki watawahukumu jinsi wanavyohukumu wazinzi na wauaji; kwa maana ni wazinzi na wauaji. 46 Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kundi la watu litaletwa, litawatisha na kuwanyanganya mali zao. 47 Kundi hilo la watu litawapiga mawe, litawashambulia kwa upanga na kuwaua wana wao na wabinti zao, na nyumba zao wataziteketeza kwa moto. 48 Ndivyo nitakavyokomesha uasherati wao katika inchi nzima, ikuwe onyo kwa wanawake wote wasifanye uzinzi kama huo mulioufanya. 49 Na ninyi Ohola na Oholiba, mutaazibiwa kutokana na uzinzi wenu na zambi yenu ya kuziabudu sanamu za miungu. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Bwana wenu Yawe. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo