Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Ezekieli 11 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Zambi ya Yerusalema

1 Roho wa Mungu akaninyanyua na kunipeleka mpaka kwenye mulango wa upande wa mashariki wa nyumba ya Yawe. Huko nikawaona watu makumi mbili na watano. Kati yao kulikuwa Yazania mwana wa Azuri na Pelatia mwana wa Benaya, ambao ni wakubwa wa Waisraeli.

2 Yawe akaniambia: Wewe mwanadamu, hawa ndio watu wanaofanya mipango ya uovu na kutoa mashauri mabaya katika muji huu.

3 Wanasema hivi: Wakati wa kujenga nyumba haujakaribia bado. Muji ni kama chungu kikubwa, na sisi ni kama nyama.

4 Kwa hiyo, utoe unabii juu yao! Tabiri ewe mwanadamu!

5 Kisha Roho wa Yawe akaniingia, naye akaniambia: Uwaambie watu kwamba: Yawe anasema hivi: Ni hivi ndivyo munavyosema, enyi Waisraeli. Ninajua mambo munayofikiri juu yake ndani ya moyo wenu.

6 Ninyi mumewaua watu wengi katika muji huu, na kujaza barabara zake na watu waliouawa.

7 Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kweli, muji huu ni chungu, na wale waliouawa ndio nyama. Ninyi lazima mutaondolewa katika muji.

8 Ninyi mumeogopa upanga? Basi, mimi nitaleta upanga juu yenu! –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.–

9 Nitawatoa ndani ya muji na kuwatoa katika mikono ya watu wa mataifa mengine, nami nitawahukumu.

10 Mutauawa kwa upanga, nami nitawahukumu katika inchi ya Waisraeli. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe.

11 Muji Yerusalema hautakuwa tena chungu chenu wala ninyi hamutakuwa nyama ndani yake. Mimi nitawahukumu katika inchi ya Waisraeli.

12 Nanyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe ambaye hamukufuata masharti yake na maagizo yake hamukuyatimiza, lakini mumetenda kufuatana na maagizo ya mataifa yanayowazunguka.

13 Nilipokuwa ninatabiri, Pelatia mwana wa Benaya akakufa. Nami nikaanguka uso mpaka chini, nikalia kwa sauti kubwa, nikisema: Ee Bwana Yawe, utawamaliza kabisa Waisraeli waliobaki?


Ahadi ya Mungu kwa wanaokuwa katika uhamisho

14 Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

15 Wewe mwanadamu, wandugu zako na wakaaji wa Yerusalema ambao vilevile ni wandugu zako wanasema juu yako na juu ya watu wote wa Israeli wanaokuwa katika uhamisho hivi: Ninyi munaokuwa katika uhamisho muko mbali sana na Yawe; maana Yawe ametupatia sisi inchi hii ikuwe mali yetu.

16 Lakini, uwaambie hao wanaokuwa katika uhamisho kwamba Bwana wao Yawe anasema hivi: Ingawa nimewapeleka mbali kati ya mataifa na kuwasambaza katika inchi zingine, hata hivyo, mimi nipo pamoja nao huko wanakokuwa, kama vile hekalu kwao.

17 Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitawakusanya toka kati ya watu, nitawakusanya kutoka katika inchi ambako mulisambazwa. Nitawarudisha katika inchi ya Israeli.

18 Nanyi mutakaporudi katika inchi yenu nitaondoa vitu vyote vichafu na machukizo yote.

19 Nitawapa moyo mupya na kuweka roho mupya ndani yenu. Nitauondoa ule moyo mugumu kama jiwe na kuwapa moyo musikilivu,

20 kusudi mupate kufuata masharti yangu na kuyatii maagizo yangu; nanyi mutakuwa watu wangu nami nitakuwa Mungu wenu.

21 Lakini hao ambao moyo wao umeambatana na vitu vichafu na machukizo yao, nitawaazibu kadiri ya mienendo yao. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.


Utukufu wa Mungu unatoka Yerusalema

22 Halafu wale makerubi waliyakunjua mabawa yao na kuanza kuruka pamoja na yale magurudumu yaliyokuwa pembeni yao, nao utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa juu yao.

23 Basi, utukufu wa Yawe ukapanda juu kutoka katikati ya muji, ukasimama juu ya mulima unaokuwa upande wa mashariki wa muji.

24 Nikiwa katika maono hayo, Roho wa Mungu alininyanyua na kunipeleka mpaka katika inchi ya Babeli, kwa watu wanaokuwa kule katika uhamisho. Kisha maono hayo yakatoweka.

25 Hapo nikawaelezea wale waliokuwa katika uhamisho mambo yote Yawe aliyonionyesha.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan