Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Ezekieli 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Kiti cha kifalme cha Mungu

1 Kwa siku ya tano ya mwezi wa ine, mwaka wa makumi tatu, wakati nilipokuwa katikati ya wale watu waliopelekwa katika uhamisho, karibu na muto Kebari, mbingu zikafunguka, nikapata maono toka kwa Mungu.

2 Katika siku ya tano ya mwezi (ulikuwa mwaka wa tano tangu mufalme Yoyakinu alipopelekwa katika uhamisho katika Babeli),

3 neno la Yawe lilimufikia kuhani Ezekieli mwana wa Buzi, alipokuwa Babeli karibu na muto Kebari. Yawe alinijaza uwezo wake.

4 Nilipoangalia niliona upepo wa zoruba unavuma kutokea upande wa kaskazini: kulikuwa wingu kubwa lililozungukwa na mwangaza, na moto ulitokea humo mufululizo na katikati ya huo moto kulikuwa kitu kinachometameta kama shaba.

5 Kutoka humo nilitambua viumbe vine, ambavyo vilionekana hivi: Vilikuwa na umbo la mwanadamu.

6 Kila kimoja kilikuwa na nyuso ine na mabawa mane.

7 Miguu yao ilikuwa yenye kunyooka; upande wa chini wa miguu yao ulikuwa kama kwato za miguu ya mwana-ngombe, nazo zilimetameta kama shaba safi.

8 Chini ya mabawa yao, kulikuwa mikono inayokuwa sawa ya mutu. Mikono hiyo ilikuwa inaelekea kwenye pande zote ine pamoja na nyuso zao na mabawa yao.

9 Incha za mabawa yao ziligusana kila bawa na bawa lingine. Vilipotembea, vilikwenda mbele moja kwa moja pasipo kugeuka.

10 Juu ya nyuso zao: kila kimoja kilikuwa na uso wa mutu upande wa mbele, uso wa simba upande wa kuume, uso wa ngombe upande wa kushoto, na uso wa tai upande wa nyuma.

11 Mabawa mawili ya kila kimoja yalikuwa yamekunjuliwa juu na kugusana; na kwa mabawa yale mengine mawili, vilifunika miili yao.

12 Popote roho alipotaka kwenda, ndiko vilikwenda; kila kimoja kilikwenda mbele moja kwa moja pasipo kugeuka.

13 Katikati ya vile viumbe kulikuwa kitu kilichoonekana kama mienge ya moto iliyoangaza huku na huku kati ya hivyo viumbe. Moto huo ulikuwa ukiwaka sana na umeme ulitokea humo.

14 Viumbe vile vilikwenda na kurudia mbio kama vile umeme unavyoonekana.

15 Nilipokuwa nikiangalia viumbe vile, nikaona chini karibu na kila kiumbe kulikuwa gurudumu.

16 Magurudumu hayo yalionekana kuwa ya namna moja, yanametameta kama jiwe la zabarajadi na umbo lao lilikuwa kama gurudumu ndani ya gurudumu lingine.

17 Yalipotembea yalikwenda kwa pande zote ine pasipo kugeuka yanapokwenda.

18 Miviringo ya hayo magurudumu ilikuwa mirefu na ya kuogopesha nayo ilikuwa inajaa macho pande zote.

19 Vile viumbe vilipokwenda, magurudumu nayo yalikwenda kandokando yao; na viumbe vile viliponyanyuka juu kutoka kwenye udongo, magurudumu hayo yaliinuka.

20 Popote roho alipokwenda vilikwenda, nayo magurudumu yaliinuka pamoja navyo; maana roho ya hivyo viumbe ilikuwa katika magurudumu hayo.

21 Viumbe hivyo vilipokwenda, magurudumu nayo yalikwenda; viliposimama, nayo yalisimama; vilipoinuka juu kutoka kwenye udongo, magurudumu nayo yaliinuka pamoja navyo. Maana roho wa vile viumbe vya ajabu ilikuwa katika magurudumu hayo.

22 Juu ya vichwa vya vile viumbe kulikuwa kitu kinachofanana na anga, kinangaa kama kioo.

23 Viumbe vile vilisimama chini ya kitu hicho; mabawa mawili ya vile viumbe yalikuwa yamekunjuliwa, moja likielekea lingine, na kwa mabawa mengine mawili vilifunika miili yao.

24 Vilipokuwa vinakwenda, nilisikia sauti ya mabawa yao; sauti ya muvumo huo ilikuwa kama ile ya maji mengi, kama sauti ya ngurumo kutoka kwa Mungu wa majeshi, na kama kelele ya jeshi. Viliposimama, vilikunja mabawa yao.

25 Nilisikia sauti kutoka juu ya kitu kile kinachokuwa kama anga kilichokuwa juu ya vichwa vyao.

26 Juu ya kitu hicho niliona kitu kimoja kinachofanana na kiti cha kifalme chenye rangi la jiwe la yakuti. Juu yake kulikuwa kunaikaa kitu kinachofanana na mutu.

27 Sehemu ya juu ya mwili wake ilingaa kama shaba, nao ulikuwa sawa unazungukwa na moto pande zote. Tokea sehemu ya chini ya mwili wake, niliona kitu kama moto. Mwangaza ulimuzunguka.

28 Ulionekana kama upindi wa mvua wakati wa mvua. Ulionekana kufanana na utukufu wa Yawe. Nilipouona, nilianguka uso mpaka chini, nikasikia sauti ya mutu mwenye kusema.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan