Esteri 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mordekayi anapewa heshima na mufalme 1 Usiku ule, mufalme hakupata usingizi. Basi, akaamuru kitabu cha Mambo ya Siku cha matukio ya kila siku, kiletwe, nacho kikasomwa mbele yake. 2 Ikaonekana jinsi ilivyoandikwa ikielezwa jinsi Mordekayi alivyopasha habari ya shauri la kumwua mufalme iliyokuwa imefanywa na Bigitani na Teresi, hao wawili kati ya matowashi wa mufalme waliokuwa walinzi wa vyumba vya mufalme. 3 Mufalme akauliza: “Tumemupa Mordekayi heshima au sifa gani kwa jambo hili?” Watumishi wake wakamujibu: “Hajafanyiwa jambo lolote.” 4 Mufalme akauliza: “Kuna mukubwa yeyote katika kiwanja?” Ikakuwa wakati ule Hamani alikuwa ameingia katika kiwanja cha inje cha nyumba ya kifalme; alikuwa amekuja kwa mufalme kuomba Mordekayi auawe kwenye muti ambao alikuwa amekwisha kumutayarishia. 5 Basi, watumishi wakamujibu mufalme: “Hamani yuko katika kiwanja.” Mufalme akasema: “Mumukaribishe ndani.” 6 Hamani alipoingia ndani, mufalme akamwuliza: “Nimufanyie nini mutu ambaye ningependa sana kumupatia heshima?” Hamani akafikiri ndani ya moyo wake: “Ni nani huyo ambaye mufalme angependa kumupatia sana heshima? Bila shaka ni mimi.” 7 Basi, Hamani akamujibu mufalme: “Mutu huyo ambaye mufalme angependa kumupatia heshima, 8 inafaa watumishi wa mufalme walete nguo safi ya kitani mufalme aliyovaa na farasi wake mwenyewe, 9 na mumoja wa washauri wako wa kuheshimika ee mufalme amuvalishe mutu yule nguo hizo za kifalme, na kumwongoza mutu yule akiwa amepanda juu ya farasi wako mpaka kwenye kiwanja cha muji, naye akitangaza: ‘Hivi ndivyo anavyotendewa mutu ambaye mufalme amependa kumupa heshima.’ ” 10 Hapo mufalme akamwambia Hamani: “Fanya haraka! Twaa nguo hizi na farasi, umupatie Mordekayi heshima hii, yule Muyuda ambaye anaikaa kwenye mulango wa nyumba ya kifalme. Usiache kumufanyia hata jambo moja kati ya hayo uliyoyataja.” 11 Basi, Hamani akatwaa nguo zile na kumuvalisha Mordekayi, akamutembeza kwenye kiwanja cha muji akiwa juu ya farasi wa mufalme, naye akitangaza: “Hivi ndivyo anavyotendewa mutu ambaye mufalme amependa kumupa heshima.” 12 Kisha Mordekayi akarudi kwenye mulango wa nyumba ya kifalme. Lakini Hamani akakimbilia kwake, akijaa huzuni naye akifunika kichwa chake kwa ajili ya haya. 13 Kule akawaelezea Zeresi, muke wake, na warafiki zake wote mambo yote yaliyomupata. Zeresi na hao warafiki zake wakamwambia: “Ikiwa huyu Mordekayi, ambaye umeanza kupoteza madaraka yako kwa ajili yake ni wa kabila la Wayuda, basi, hautamuweza; atakushinda kabisa.” Hamani anauawa 14 Walipokuwa bado wanaongea juu ya hayo, matowashi wa mufalme wakafika kumutwaa Hamani kwenda kwenye karamu ya Esteri. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo