Esteri 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Esteri anawaalika mufalme na Hamani kwa karamu 1 Kisha siku tatu ya kufunga kwake, Esteri akavaa nguo zake za kimalkia, akaenda kusimama katika kiwanja cha ndani cha nyumba ya mufalme, kuelekea chumba cha mufalme. Mufalme alikuwa mule ndani akiikaa katika kiti chake cha kifalme, kuelekea mulango wa nyumba ya mufalme. 2 Mufalme alipomwona malkia Esteri akisimama katika kiwanja, Esteri akapata kukubaliwa mbele yake, naye akamunyooshea fimbo ya zahabu aliyokuwa akishika katika mukono wake. Esteri akakaribia, akagusa incha ya fimbo. 3 Hapo mufalme akauliza: “Unataka nini Esteri? Uniambie unachotaka, nawe utapata – hata kama ni nusu ya ufalme wangu.” 4 Esteri akamujibu: “Ikikupendeza, ewe mufalme, ukuje leo pamoja na Hamani, kwenye karamu ninayotayarisha kwa ajili yako, mufalme.” 5 Mufalme akatoa amri Hamani akuje upesi, kama vile Esteri alivyoomba. Basi, mufalme na Hamani wakaenda kwenye karamu Esteri aliyotayarisha. 6 Walipokuwa wanakunywa divai, mufalme akamwuliza tena Esteri: “Unataka nini? Uniambie, nawe utapata. Ombi lako ni nini? Hata kama ni nusu ya ufalme wangu, utapewa.” 7 Esteri akamujibu: “Ombi langu ni hili: 8 Kama nimepata kukubaliwa mbele yako, ewe mufalme, na ikikupendeza kukubali ombi langu, basi, ninaomba wewe na Hamani mukuje kesho kwenye karamu nyingine nitakayowaandalia. Wakati huo nitakujulisha ombi langu.” Hamani anapanga kumwua Mordekayi 9 Hamani akatoka kule kwenye karamu mwenye furaha tele na moyo mukunjufu. Lakini alipomwona Mordekayi kwenye mulango wa nyumba ya kifalme, hasimami wala hamupi heshima, Hamani akawaka hasira. 10 Hata hivyo, akajizuia, akaenda kwake. Halafu akawaalika kwake warafiki zake, na kumwomba muke wake Zeresi ajiunge nao. 11 Halafu akaanza kueleza juu ya utajiri anaokuwa nao, wana anaokuwa nao, jinsi mufalme alivyomupandisha cheo, na jinsi alivyopewa madaraka zaidi kuliko wakubwa wengine wote wa mufalme. 12 Hamani akaendelea kujitapa: “Vilevile malkia Esteri hakumwalika mutu mwingine yeyote pamoja na mufalme isipokuwa mimi tu. Hata kesho tena, ametualika mimi na mufalme. 13 Lakini yote haya hayanifalii kitu ikiwa nitaendelea kumwona yule Muyuda Mordekayi kwenye mulango wa nyumba ya kifalme.” 14 Basi, muke wake Zeresi na warafiki zake wakamushauria hivi: “Kwa nini asitengenezewe muti wa kutundikia, wenye urefu wa metre makumi mbili na mbili? Kesho asubui, unaweza kuzungumuza na mufalme kusudi Mordekayi auawe juu yake, kisha uende ukule karamu na mufalme kwa furaha.” Wazo hilo lilimufurahisha Hamani, naye akatengeneza muti ule. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo