Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Esteri 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mordekayi anaomba musaada wa Esteri

1 Mordekayi alipojua yote yaliyotukia, akapasua nguo zake, akavaa nguo ya gunia, na kujitia majivu. Kisha, akapita katikati ya muji akilia kwa sauti ya uchungu.

2 Akakwenda mpaka kwenye mulango wa nyumba ya mufalme, lakini hakuweza kuingia kwa sababu hakuna mutu aliyeruhusiwa kuingia katika nyumba ya kifalme akiwa amevaa nguo ya gunia.

3 Katika kila jimbo, mara tu amri ya mufalme ilipotangazwa, kilio kikubwa kiliwapata Wayuda. Wakafunga, wakalia na kuomboleza; na wengi wao wakalala katika majivu wakiwa wamevaa magunia.

4 Malkia Esteri alipoarifiwa na matowashi na wajakazi wake habari za Mordekayi akahuzunika sana. Akamupelekea Mordekayi nguo za kuvaa kwa pahali pa nguo ya gunia, lakini Mordekayi akazikataa.

5 Basi, akamwita Hataki, mumoja wa matowashi wa mufalme aliyechaguliwa na mufalme amutumikie Esteri, akamutuma kwa Mordekayi kuuliza maneno na maana ya tukio hilo.

6 Hataki akamwendea Mordekayi katika uwanja, mbele ya mulango wa nyumba ya kifalme.

7 Mordekayi akamwelezea Hataki yote yaliyokuwa yamemupata, na kiasi kamili cha feza ambayo Hamani alikuwa ameahidi kulipa katika hazina ya mufalme kama Wayuda wote wangeangamizwa.

8 Akamupa na barua moja ya tangazo lililokuwa limetolewa katika muji wa Susani juu ya kuangamizwa kwa Wayuda, akamwomba amupelekee Esteri na kumwelezea jinsi hali inavyokuwa, na kumwambia aende kumusihi mufalme na kumwomba awahurumie Wayuda, watu wa Esteri.

9 Hataki akaenda akamwelezea Esteri maneno yote Mordekayi aliyosema.

10 Naye Esteri akamwambia Hataki arudie amwambie Mordekayi:

11 “Watumishi wote wa mufalme na watu wote wa majimbo yote wanajua kwamba mutu yeyote yule akiingia katika kiwanja cha ndani na kumwona mufalme bila kuitwa, huyo anapaswa kuuawa. Anayeweza kuponyoka ni yule tu ambaye mufalme atamunyooshea fimbo yake ya zahabu kwa kumuponyesha. Na mimi sijaitwa na mufalme, yapata mwezi muzima sasa.”

12 Mordekayi alipopata ujumbe wa Esteri,

13 akamutumia onyo hili: “Usizani kwamba kwa sababu upo katika nyumba ya kifalme wewe uko salama zaidi kuliko Muyuda mwingine yeyote.

14 Ukikaa kimya wakati kama huu, musaada utawafikia Wayuda kutoka pahali pengine, nao wataokolewa; lakini wewe utakufa, na jamaa ya baba yako itaangamia. Ni nani anayejua pengine umefanywa kuwa malkia kwa ajili ya wakati kama huu!”

15 Esteri akamupelekea Mordekayi jibu hili:

16 “Kwenda uwakusanye pamoja Wayuda wote wanaokuwa katika muji wa Susani. Mufunge, musikule wala musikunywe kwa siku tatu, usiku na muchana, kwa ajili yangu. Na mimi na wajakazi wangu tutafanya vile vile. Kisha, nitamwendea mufalme, ingawa ni kinyume cha sheria. Kama ni kuuawa, niuawe.”

17 Basi, Mordekayi akaenda zake na kufanya kama vile Esteri alivyomwambia.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan