Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Danieli 9 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Danieli anawaombea watu wake

1 Katika mwaka Dario mufalme wa Wamedi mwana wa Ahasuero, alipoanza kutawala juu ya ufalme wa Wakaldea,

2 mimi Danieli nilikuwa nikisoma kwa uangalifu vitabu vitakatifu, na humo nikaelewa maana ya jambo lile Yawe alilomufahamisha nabii Yeremia juu ya ile miaka makumi saba, muda ambao utahusika na kuharibiwa kwa Yerusalema.

3 Nilimwomba Yawe, kwa moyo, nikimutolea maombi pamoja na kufunga kula chakula, nikavaa gunia na kuikaa kwenye majivu.

4 Nilimwomba Yawe, Mungu wangu, na kuitikia zambi, nikisema: Ee Bwana, wewe ni Mungu mukubwa na wa kuogopesha. Wewe unashika agano lako na kutenda mema kwa wanaokupenda na kuzitii amri zako.

5 Tumetenda zambi, tumekosa, tumetenda maovu na kukuasi. Tumevunja amri zako na maagizo yako.

6 Hatukuwasikiliza watumishi wako manabii, ambao kwa jina lako walisema na wafalme wetu, wakubwa wetu, babu zetu na taifa letu lote.

7 Kwako, ee Bwana, kuna haki, lakini sisi tumepata haya siku zote. Jambo hili ni kweli kwetu sisi wote tunaoishi Yudea, wakaaji wa muji Yerusalema na Waisraeli wote ambao umewatawanya katika inchi za mbali na za karibu kwa sababu ya kukosa uaminifu kwako.

8 Ee Bwana, sisi tumefezeheka, wafalme wetu, wakubwa wetu na babu zetu, kwa sababu tumekutendea zambi.

9 Wewe, Bwana Mungu wetu, una huruma na musamaha, ingawa sisi tumekuasi.

10 Tulikataa kukusikiliza, ee Bwana wetu, Mungu wetu; hatukutenda kulingana na sheria zako ulizotupatia kwa njia ya watumishi wako manabii.

11 Waisraeli wote wameiasi sheria yako, wamekuacha wakakataa kukutii. Kwa sababu tumekukosea, tumemwangiwa laana na viapo vilivyoandikwa katika Sheria ya Musa, mutumishi wako.

12 Umetimiza yale uliyosema utatutendea sisi pamoja na watawala wetu kwa kuuazibu Yerusalema vikali zaidi ya muji mwingine wowote katika dunia.

13 Umetuazibu kama ilivyoandikwa katika Sheria ya Musa, lakini mpaka sasa, ee Yawe, Mungu wetu, hatukuomba musamaha wako kwa kuziacha zambi zetu na kutambua uaminifu wako.

14 Kwa hiyo, ee Yawe, Mungu wetu, ulikuwa tayari kutuazibu, na ukafanya hivyo, kwa sababu unafanya mambo yanayokuwa ya haki, nasi hatukukusikiliza.

15 Na sasa ee Bwana, Mungu wetu, uliyewaondoa watu wako katika inchi ya Misri kwa nguvu yako kubwa na kulifanya jina lako litukuzwe mpaka sasa, tunasema kwamba tumetenda zambi; tumefanya maovu.

16 Ee Bwana, kwa kadiri ya matendo yako ya haki usiukasirikie wala kuwa na hasira kwa ajili ya muji wako Yerusalema, mulima wako mutakatifu. Watu wote wa inchi za jirani wanauzarau Yerusalema na watu wako, kwa sababu ya zambi zetu na maovu babu zetu waliyotenda.

17 Kwa hiyo, ee Mungu, usikilize malalamiko yangu na maombi yangu mimi mutumishi wako. Kwa ajili ya heshima yako, ulionee tena hekalu lako lililoharibika huruma.

18 Tega sikio, ee Mungu wangu; angalia uone taabu tunazokuwa nazo na jinsi huo muji unaoitwa kwa jina lako unavyotaabika. Tunakutolea maombi yetu si kwa sababu tumetenda haki, lakini kwa sababu wewe una huruma nyingi.

19 Ee Yawe, utusikie; utusamehe ee Yawe. Ee Yawe, kwa ajili ya heshima yako utusikie na utende, wala usikawie, ee Mungu wangu, kwa ajili ya muji huu na watu hawa wanaoitwa kwa jina lako!


Malaika Gabrieli anafafanua unabii

20 Basi, nilipokuwa nikiomba, nikiitikia zambi zangu na zambi za watu wangu wa inchi ya Israeli, pamoja na kumusihi Yawe kwa ajili ya mulima wake mutakatifu,

21 yule mutu Gabrieli, ambaye nilikuwa nimemwona katika maono hapo mbele, alishuka kwa haraka mpaka pahali nilipokuwa. Ilikuwa wakati wa kutoa sadaka ya magaribi.

22 Basi, akaniambia: Danieli, nimekuja kukupa hekima na uwezo wa kufahamu.

23 Ulipoanza kuomba, Mungu alitoa jibu, nami nimekuja kukuelezea jibu hilo kwa sababu unapendwa sana. Kwa hiyo, usikilize kwa uangalifu jibu hilo na kuelewa maono hayo.

24 Muda wa miaka saba mara makumi saba umewekwa kwa ajili ya watu wako na juu ya muji wako mutakatifu kwa kumaliza makosa, kukomesha zambi, kusamehe uovu, kuleta haki ya milele, kutia muhuri juu ya maono na unabii na kupakaa mafuta katika Pahali Patakatifu Sana.

25 Basi, ujue na kufahamu jambo hili: tangu wakati amri itakapotolewa ya kujengwa upya Yerusalema mpaka kuja kwa yule aliyepakwa mafuta, yule anayekuwa mukubwa, ni muda wa majuma saba. Kwa muda wa majuma makumi saba na mawili, Yerusalema utajengwa upya, wenye barabara kubwa na kuta, lakini wakati huo utakuwa wa taabu.

26 Kisha majuma hayo makumi saba na mawili, yule aliyepakwa mafuta atauawa na hatabaki na kitu. Muji na Pahali Patakatifu Sana vitaharibishwa na waaskari wa mutawala atakayekuja kushambulia. Mwisho wake utafika kama mafuriko, kukiwa vita na maangamizi kama yalivyopangwa na Mungu.

27 Mutawala huyo atafanya mapatano imara na watu wengi kwa muda wa miaka saba. Kisha nusu ya muda huo atakomesha sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka zingine. Pahali pa juu katika hekalu patasimamishwa chukizo linaloleta uharibifu, nalo litabaki pale mpaka yule aliyemusimamisha atakapoangamizwa kama ilivyopangwa na Mungu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan