Danieli 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ndoto ya mufalme Nebukadneza 1 Katika mwaka wa pili wa utawala wake, mufalme Nebukadneza aliota ndoto. Na kwa hiyo roho yake ikahuzunika sana hata hakuweza kupata usingizi. 2 Basi, mufalme akaamuru waganga, walozi na wachawi wa Wakaldea waletwe kusudi wamufasirie ndoto yake. Wote wakakuja na kusimama mbele yake. 3 Mufalme Nebukadneza akawaambia: Niliota ndoto, nayo inanipa wasiwasi, nami ninataka nijulishwe maana yake. 4 Wale Wakaldea wakamwambia mufalme katika luga ya Kiaramu: Uishi milele, ee mufalme! Utuelezee ndoto yako nasi watumishi wako tutakufasiria maana yake. 5 Mufalme akawaambia: Nimetoa neno langu kamili: ikiwa hamutanijulisha ndoto yenyewe na maana yake, mutakatwa vipandevipande na nyumba zenu zitabomolewa. 6 Lakini mukiniambia hiyo ndoto na maana yake, nitawapa zawadi, mapato na heshima kubwa. Basi, munijulishe ndoto hiyo na maana yake! 7 Wao wakamujibu mara ya pili: Mufalme, utuelezee ndoto hiyo, nasi watumishi wako tutakufasiria maana yake. 8 Halafu mufalme akawajibu akisema: Ninajua kweli kwamba munajaribu kupoteza wakati kwa maana munaona kwamba nilikwisha toa neno langu kamili, 9 kwamba musiponijulisha ndoto hiyo, azabu yenu ni moja. Mumepatana kunidanganyadanganya na kuniambia uongo kwa kungojea hali ibadilike. Muniambie ndoto hiyo, nami nitajua kwamba munaweza kunijulisha maana yake. 10 Wale Wakaldea wakamujibu: Mufalme, hakuna mutu yeyote katika dunia anayeweza kutimiza mapenzi yako. Hakuna mufalme yeyote, hata akuwe mukubwa na mwenye nguvu yapata gani aliyepata kuwauliza waganga au walozi au Wakaldea jambo kama hilo. 11 Jambo unalouliza, ee mufalme, ni gumu. Hakuna mutu anayeweza kukufunulia isipokuwa miungu peke yake ambayo haikai kati ya wanadamu. 12 Kusikia hivyo, mufalme Nebukadneza alikasirika na kuwa na hasira sana, akaamuru wenye hekima wote wa Babeli waangamizwe. 13 Basi, tangazo likaenea kuwa wenye hekima wote wauawe; Danieli na wenzake, nao vilevile wakatafutwa kusudi wauawe. Mungu anamufunulia Danieli ndoto 14 Lakini, Danieli akasema na Arioki kwa uangalifu na hekima. Arioki alikuwa ni mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme ambaye alipewa amri ya kuwaua wenye hekima wa Babeli. 15 Danieli akamwuliza: Kwa nini amri ya mufalme ni kali hivyo? Arioki akamwelezea Danieli maneno yote. 16 Halafu Danieli alimwendea mufalme na kumwomba amupatie muda kusudi apate kumujulisha mufalme maana ya ndoto yake. 17 Kisha, Danieli akarudi kwa nyumba, akawajulisha wenzake Hanania, Misaeli na Azaria jambo hilo. 18 Aliwaambia wamwombe Mungu wa mbinguni awaonee huruma juu ya fumbo hilo, kusudi wao wasiangamie pamoja na wenye hekima wengine wa Babeli. 19 Halafu Danieli akafunuliwa fumbo hilo usiku katika maono. Naye Danieli akamushukuru Mungu wa mbinguni, 20 akasema: Jina la Mungu litukuzwe milele na milele. Hekima na nguvu ni vyake. 21 Anabadilisha nyakati na wakati, anaondoa na kuwatawalisha wafalme. Anawapa hekima wenye hekima, anawaongezea wenye maarifa ufahamu. 22 Anafunua siri na mafumbo, anajua kinachokuwa katika giza, mwangaza unakaa kwake. 23 Kwako, ee Mungu wa babu zangu, ninatoa shukrani na kukusifu, maana umenipa hekima na nguvu, umetujulisha kile tulichokuomba, umetujulisha yale maneno ya mufalme. Danieli anafasiria maana ya ndoto 24 Basi, Danieli akamwendea Arioki aliyekuwa amechaguliwa kuwaangamiza wenye hekima wa Babeli, akamwambia: Usiwaue wenye hekima wa Babeli, lakini unipeleke mimi mbele ya mufalme, nami nitamweleza maana ya ndoto yake. 25 Basi, Arioki akamupeleka Danieli mbele ya mufalme kwa haraka na kumwambia: Nimemupata mutu fulani kati ya wafungwa wa Yuda anayeweza kukufasiria maana ya ndoto yako, ee mufalme. 26 Mufalme akamwuliza Danieli, ambaye vilevile aliitwa Beltesaza: Unaweza kunijulisha ndoto niliyoota na maana yake? 27 Danieli akamujibu mufalme: Hakuna wenye hekima, wachawi, waganga wala waaguzi wanaoweza kukujulisha fumbo hilo lako. 28 Lakini, kuna Mungu mbinguni ambaye anafumbua mafumbo, naye amekujulisha, ee mufalme Nebukadneza, mambo yatakayotukia katika siku zinazokuja. Ndoto yako na maono yaliyokufikia ulipokuwa unalala ni haya: 29 Ee mufalme, ulipokuwa unalala katika kitanda chako, mawazo yalikufikia juu ya mambo yatakayotukia kisha; naye Mungu anayefumbua mafumbo, alikuonyesha yale yatakayotukia. 30 Lakini mimi sikufumbuliwa fumbo hili kwa sababu nina hekima kuliko wanadamu wengine, lakini kusudi wewe mufalme, upate kujulishwa maana ya ndoto yako na kujua mawazo yako. 31 Katika ndoto yako, ee mufalme, uliona sanamu kubwa, yenye nguvu na iliyoangaa sana, ikisimama mbele yako. Sanamu hiyo ilikuwa ya kutisha sana. 32 Kichwa cha sanamu hiyo kilikuwa cha zahabu safi, kifua chake na mikono yake vilikuwa vya feza na tumbo lake na mapaja yake vilikuwa vya shaba. 33 Miguu yake ilikuwa ya chuma na vikanyagio vyake vilikuwa vya muchanganyiko wa chuma na udongo wa mufinyanzi. 34 Ulipokuwa ukiangalia, jiwe liliongoka lenyewe, bila kuguswa, na kuipondaponda miguu ya shaba na udongo wa mufinyanzi ya ile sanamu, na kuivunja vipandevipande. 35 Mara moja chuma, udongo wa mufinyanzi, shaba, feza na zahabu, vyote vikavunjika vipandevipande na vikakuwa kama maganda kwenye nafasi ya kupepetea ngano wakati wa jua. Upepo ukavipeperushia mbali wala hakukubakia hata kipande kimoja. Lakini lile jiwe lililoivunja ile sanamu likageuka kuwa mulima mukubwa na kuijaza dunia yote. 36 Hiyo ndiyo ndoto yako, ee mufalme. Na sasa tutakupa maana yake. 37 Wewe, ee mufalme, mufalme wa wafalme! Mungu amekupa ufalme, uwezo, nguvu na utukufu! 38 Amekupa mamlaka juu ya wanadamu wote, nyama wa pori na ndege wote, popote kule wanapokuwa. Wewe ndiwe kile kichwa cha zahabu! 39 Nyuma yako kutafuata ufalme mwingine, lakini ufalme huo utakuwa zaifu. Huu utafuatwa na ufalme wa tatu unaofananishwa na shaba; huo utaitawala dunia yote. 40 Nyuma ya falme hizo, kutafuata ufalme mwingine wenye kuwa imara kama chuma. Na kama vile chuma kinavyovunja na kupondaponda vitu vyote, ndivyo ufalme huo utakavyovunjavunja na kusaga kabisa falme zilizotangulia. 41 Uliona vilevile kwamba vikanyagio na vidole vya sanamu hiyo vilikuwa nusu udongo wa mufinyanzi na nusu chuma. Hii ina maana kwamba ufalme huo utagawanyika; lakini ndani yake kutakuwa nguvu za chuma kwa sababu kulikuwa chuma kilichochanganyikana na udongo wa mufinyanzi. 42 Kama ulivyoona, vidole vyake vya miguu vilikuwa nusu chuma na nusu udongo wa mufinyanzi, na hii ina maana kwamba ufalme ule utakuwa na sehemu moja yenye nguvu na sehemu ingine yenye uzaifu. 43 Hii ina maana kwamba watawala wa ufalme huo watachanganyikana kwa kuoana na watu wasiokuwa wa taifa lao, lakini hawatafikia kuchanganyikana kama vile chuma kisivyoweza kuchanganyikana na udongo wa mufinyanzi. 44 Wakati wa wafalme wale, Mungu wa mbinguni ataanzisha ufalme ambao hautaangamizwa hata kidogo. Watu wengine hawataushinda na kuutawala ufalme huo, lakini ufalme huo utaziponda na kuzikomesha falme zilizotangulia, nao utadumu milele. 45 Uliliona jiwe lililoongoka lenyewe toka kwenye mulima, bila kuguswa, na jinsi lilivyoivunja vipandevipande ile sanamu iliyotengenezwa kwa chuma, shaba, udongo wa mufinyanzi, feza na zahabu. Ee mufalme, Mungu Mukubwa amekufunulia mambo yatakayotukia nyuma. Ni mimi ninayekuelezea hivyo. Ndoto yako ni ya kweli na maana yake ni ya kuaminiwa. 46 Halafu mufalme Nebukadneza akaanguka uso mpaka chini na kumutukuza Danieli na kuamuru wamutolee Danieli sadaka na ubani. 47 Mufalme akamwambia Danieli: Hakika, Mungu wako ni Mungu wa miungu na Bwana wa wafalme, na ndiye anayefumbua mafumbo kwa sababu ameweza kunifumbulia fumbo hili. 48 Kisha mufalme Nebukadneza akamupandishia Danieli heshima kubwa, akamupa zawadi nyingi kubwakubwa, na kumufanya kuwa mutawala wa jimbo lote la Babeli, na mukubwa wa wenye hekima wote wa Babeli. 49 Danieli akamwomba mufalme, naye mufalme akawaweka Sadiraki, Mesaki na Abedenego kuwa wasimamizi wa mambo ya utawala ya jimbo la Babeli. Lakini Danieli akabakia katika nyumba ya mufalme. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo