Danieli 12 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wakati wa mwisho 1 Wakati huo, Mikaeli, malaika mukubwa, anayekuwa mulinzi wa watu wako, atatokea. Halafu kutakuwa wakati wa taabu sana kuliko nyakati zingine zote tangu mataifa yalipoanza kuwa katika dunia. Lakini, wakati huo, kila mumoja wa watu wako ambaye jina lake limeandikwa katika kitabu cha uzima, ataokolewa. 2 Wengi wa wale ambao wamekwisha kufa, watafufuka; wengine watapata uzima wa milele, na wengine watapata haya na kuzarauliwa milele. 3 Wale wenye hekima watangaa kama vile anga linavyongaa, na wale waliowaongoza wengine kutenda mema, watangaa kama nyota milele. 4 Lakini sasa, Danieli, weka kwa siri mambo hayo; funga kitabu na kutia muhuri juu yake mpaka wakati wa mwisho utakapofika. Wengi watakimbilia huko na huko, na maarifa yataongezeka. 5 Kisha, mimi Danieli nikaangalia, nikaona watu wawili wakisimama kwenye ukingo wa muto; mumoja upande huu na mwingine upande wa pili. 6 Nikamwuliza yule aliyesimama upande wa juu wa muto, aliyevaa nguo za kitani: Mambo haya ya kutisha yatadumu mpaka wakati gani? 7 Yule mutu aliyesimama upande wa juu wa muto, aliyevaa nguo za kitani, akainua mikono yake yote miwili kuelekea mbinguni. Kisha nikamusikia akiapa kwa jina la yule anayeishi milele: Itakuwa muda wa nyakati tatu na nusu. Wakati mateso ya watu watakatifu yatakapokomeshwa, mambo haya yote yatakuwa yametimia. 8 Nilisikia lakini sikuelewa. Halafu, nikamwuliza: Bwana wangu, mwisho wa mambo haya yote utakuwa namna gani? 9 Akanijibu: Danieli, ujiendee, maana maneno haya ni siri na yamefungwa kwa kutiwa muhuri juu yake mpaka wakati wa mwisho. 10 Watu wengi wataondolewa uchafu, watatakaswa na kusafishwa. Lakini watu waovu wataendelea kutenda uovu. Hakuna hata mumoja wa hao waovu atakayeelewa; wenye hekima ndio watakaoelewa. 11 Tangu wakati wa kukomeshwa kwa sadaka za kuteketezwa kwa moto za kila siku, ni kusema kutoka wakati ule chukizo linaloleta uharibifu litakaposimamishwa, itakuwa muda wa siku elfu moja mia mbili na makumi kenda. 12 Heri yao watakaovumilia mpaka siku zile elfu moja mia tatu na makumi tatu na tano zitakapotimia. 13 Lakini wewe, ee Danieli, ujiendee, upumzike katika kaburi, na wakati huo utakapotimia, utafufuka na kupata zawadi yako. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo