Danieli 11 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Lakini kwa upande wangu mimi, katika mwaka wa kwanza wa utawala wa mufalme Dario wa Wamedi, nilijitoa kwa kumuimarisha na kumutia nguvu. 2 Sasa nitakuelezea ule ukweli wa mambo haya. Wafalme wengine watatu wataitawala inchi ya Persia. Hao watafuatwa na mufalme wa ine ambaye atakuwa tajiri kuliko wale waliomutangulia. Wakati atakapopata nguvu kwa ajili ya utajiri wake, ataanza kuushambulia ufalme wa Ugriki. Falme za kaskazini na Ugriki 3 Kisha kutatokea mufalme hodari atakayetawala eneo kubwa na kufanya atakavyopenda. 4 Hata hivyo, wakati atakapokuwa na nguvu, ufalme wake utavunjika na kugawanyika katika sehemu ine kuelekea pande ine za mbingu. Wazao wake hawatatawala, wala ufalme hautakuwa katika mikono ya urizi aliotawala, kwa sababu ufalme wake utakamatwa na wengine. 5 Mufalme wa kusini atakuwa mwenye nguvu. Lakini mumoja wa majemadari wake atakuwa na nguvu kuliko yeye na utawala wake utakuwa mukubwa zaidi. 6 Kisha miaka michache, wataungana pamoja; binti wa mufalme wa kusini ataolewa katika jamaa ya mufalme wa kaskazini na kutimiza mapatano hayo, lakini hataendelea kuwa na nguvu, hata mufalme na wazao wake hawatavumilia; na huyo binti, mwana wake na wajakazi aliokwenda nao, wote watauawa. 7 Kisha mutoto mumoja wa ukoo wa huyo binti atakuwa mufalme. Huyo atayashambulia makundi ya waaskari wa mufalme wa kaskazini na kuingia katika miji yao yenye kuzungukwa na kuta na kushinda. 8 Atabeba sanamu za miungu yao na vyombo vya bei kali vya feza na zahabu mpaka katika inchi ya Misri. Kwa muda wa miaka michache, mufalme wa kusini hatamushambulia mufalme wa kaskazini. 9 Lakini nyuma, mufalme huyu wa kaskazini ataushambulia ufalme wa kusini, kisha atarudi katika inchi yake. 10 Wana wa mufalme wa kaskazini watakusanya kundi kubwa la waaskari na kujitayarisha kwa vita. Kundi hilo litasonga mbele kama mafuriko ya maji litapita na kupigana vita mpaka ndani ya muji wenye kuta wa waadui. 11 Halafu, mufalme wa kusini, kwa hasira yake, atapigana vita na mufalme wa kaskazini ambaye naye atamushambulia kwa kundi kubwa la waaskari, lakini litashindwa. 12 Kisha kulishinda vibaya kundi la waasakri wa kaskazini na kuua maelfu, ataanza kujisifu, lakini hataendelea kuwa mushindi. 13 Maana kwa mwisho mufalme wa kaskazini atatayarisha kundi kubwa la waaskari kuliko lile la mbele. Kisha miaka michache atarudi na kundi kubwa la waaskari lenye vifaa vingi vya vita. 14 Wakati huo watu wengi watamwasi mufalme wa kusini. Watu wamoja waovu wa taifa lako wewe Danieli, wataasi kwa kutimiza maono haya, lakini watashindwa. 15 Halafu mufalme wa kaskazini atalundika udongo kando ya muji wenye kuta imara na kuuteka. Waaskari wa kusini hawataweza kuupiganisha, hata wale wafundi wa vita, maana hawatakuwa na nguvu. 16 Mushambulizi atawatendea sawa anavyopenda; hakuna atakeyesubutu kupingana naye. Atasimama katika inchi tukufu, na inchi hiyo yote itakuwa chini ya mamlaka yake. 17 Huyo mushambulizi atakusudia kuja na kundi lake lote la waaskari, naye atafanya mapatano na kuyatimiza. Atamuoesha binti yake mumoja kusudi apate kuuangamiza ufalme wa adui yake; lakini mupango wake hautawezekana, wala kumufaidia kwa jambo lolote. 18 Nyuma ya hayo, atageukia na kushambulia inchi nyingi za kandokando ya bahari na kuzishinda. Lakini jemadari mugeni atamushinda na kuyakomesha majivuno yake mwenyewe; kweli atamurudishia mufalme wa kaskazini majivuno yake mwenyewe. 19 Halafu atageuka kurudi katika kuta za inchi yake mwenyewe, lakini atajikwaa na kuanguka katika vita na huo ndio utakaokuwa mwisho wake. 20 Huyu atafuatwa na mufalme mwingine ambaye atatuma mulipishaji wa kodi kupita katika nafasi ya utukufu ya ufalme wake. Mufalme huyo atauawa kisha siku chache, lakini si kwa hasira wala katika vita. Mufalme mwovu wa kaskazini 21 Mufalme atakayefuata atakuwa wa kuzarauliwa ambaye asiyeweza kupewa heshima ya kifalme, naye atakuja wakati watu wasiouzania na kunyanganya ufalme kwa werevu. 22 Makundi ya waaskari pamoja na kuhani wa hekalu wataangamizwa na kuwaua. 23 Kwa kufanya mapatano, atayadanganya mataifa mengine, na ataendelea kupata nguvu ingawa atatawala taifa dogo. 24 Na kwa wakati wasiouwazia ataingia katika sehemu za jimbo zenye utajiri mwingi na kufanya mambo ambayo hayakufanyika hata na mumoja wa babu zake waliomutangulia. Kisha, atawagawanyia wafuasi wake mali na vitu alivyonyanganya katika vita. Atafanya mipango ya kuishambulia miji yenye kuta, lakini kwa muda tu. 25 Kwa uhodari mwingi, ataunda kundi kubwa la waaskari kusudi apate kuushambulia ufalme wa kusini, naye mufalme wa kusini atajibu mashambulizi hayo kwa kundi kubwa zaidi la waaskari na lenye nguvu sana. Lakini, mufalme wa kusini hatashinda kwa maana watafanya shauri baya juu yake. 26 Wale wanaokula pamoja naye, ndio watakaomwangamiza. Watamwangamiza na waaskari wake watasambazwa na wengi watauawa. 27 Halafu wafalme hao wawili wataikaa kwa meza pamoja, lakini kila mumoja anamuwazia mwenzake uovu, na kudanganyana. Lakini hawatafanikiwa, maana wakati uliopangwa utakuwa bado haujatimia. 28 Mufalme wa kaskazini atarudi katika inchi yake akiwa na mali nyingi, lakini nia yake ndani ya moyo ni kulivunja agano takatifu. Atafanya vile anavyopenda, kisha atarudi katika inchi yake. 29 Katika wakati uliopangwa ataishambulia inchi ya kusini kwa mara ingine, lakini mara hii, mambo yatakuwa tofauti. 30 Mashua kutoka Kitimu zitamushambulia, naye atashikwa na hofu. Kisha atarudi nyuma akiwa amejaa hasira na kuvunja agano takatifu. Halafu atafuata shauri la wale walioasi agano takatifu. 31 Waaskari wake watalichafua hekalu na kuta zake, watakomesha sadaka za kuteketezwa kwa moto za kila siku na kusimamisha kule katika hekalu chukizo linaloleta uharibifu. 32 Atawashawishi kwa werevu wale walioasi agano, lakini watu wanaokuwa waaminifu kwa Mungu wao watasimama imara na kutenda. 33 Wenye hekima kati ya watu watawafundisha wengi. Hata hivyo, kwa siku chache watauawa kwa upanga au kwa moto, watakamatwa mateka au kunyanganywa mali zao. 34 Wakati wanapouawa, watapata musaada kidogo, na wengi wanaojiunga nao, watafanya hivyo kwa unafiki. 35 Wamoja kati ya wenye hekima watauawa, kusudi wapate kuondolewa uchafu, kutakaswa na kusafishwa, mpaka wakati wa mwisho, ambao sasa bado haujatimia. 36 Mufalme atafanya kama anavyopenda. Atajitukuza na kujivuna kwamba yeye ni mukubwa kuliko miungu yote, na kumutukana Mungu wa miungu. Ataendelea kufanikiwa mpaka kasirani ifikie ukomo wake, maana yaliyopangwa sherti yatimie. 37 Mufalme huyo hataijali miungu ya babu zake wala yule anayependwa na wanawake. Ataizarau miungu mingine yote, maana atajiweka kuwa mukubwa kuliko kila mumoja wao. 38 Pahali pa miungu hiyo atamuheshimu mungu mulinzi wa kuta za muji, ambaye babu zake hawakumwabudu hata kidogo. Atamutolea zahabu, feza na mawe ya bei kali, na zawadi za bei kubwa. 39 Atazishugulikia kuta za muji wake kwa musaada wa mungu wa kigeni. Wale wanaomutambua kuwa mufalme, atawaongezea heshima kubwa, atawapa vyeo vikubwa na kuwagawanyia inchi kama zawadi. 40 Wakati wa mwisho mufalme wa kusini atamushambulia mufalme huyo wa kaskazini. Lakini mufalme wa kaskazini atajibu mashambulio hayo kwa nguvu kama zoruba, akitumia magari ya vita, waaskari wapanda-farasi na mashua nyingi. Atashambulia inchi nyingi na kupita katika inchi hizo kama mafuriko ya maji. 41 Atashambulia hata inchi ile tukufu na kuua maelfu ya watu. Lakini inchi za Edomu, Moabu na sehemu kubwa ya Amoni, zitaokoka kutoka katika mikono yake. 42 Wakati atakaposhambulia inchi hizo, hata inchi ya Misri haitaponyoka. 43 Atatwaa akiba za zahabu, feza na mawe yote ya bei kali ya inchi ya Misri. Watu wa Libya na watu wa Etiopia watamufuata. 44 Lakini habari kutoka mashariki na kaskazini zitamutisha. Naye atatoka kwa hasira kubwa kusudi aharibu na kuangamiza watu wengi. 45 Zaidi ya hayo, atapiga mahema yake makubwa kati ya bahari na mulima mutukufu na mutakatifu. Lakini atakuwa amefikia ukomo wake, na hakutakuwa mutu yeyote wa kumusaidia. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo