Amosi 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maono ya kwanza: Nzige 1 Bwana wetu Yawe alinionyesha hivi: Yawe alikuwa anaumba nzige kundi zima, nyuma ya watu kumaliza kukata majani kwa ajili ya nyama wa mufalme. Wakati ule, majani yalikuwa ndio yanaanza kuchipuka tena. 2 Niliwaona nzige hao wakikula na kumaliza kila jani katika inchi. Halafu nikasema: Ee Bwana wetu Yawe, ninakusihi utuhurumie! Wazao wa Yakobo wataweza kuishi namna gani? Wao ni wadogo sana! 3 Basi, Bwana wetu Yawe akabadilisha nia yake, akasema: Halitatukia! Maono ya pili: Moto 4 Bwana wetu Yawe alinionyesha tena maono mengine: Bwana wetu Yawe akiuita moto wa hukumu wa kuwaazibu watu. Moto ule uliunguza vilindi vikubwa vya bahari, ukaanza kuiteketeza inchi kavu. 5 Halafu nikasema: Ee Bwana wetu Yawe, ninakusihi uache kuazibu! Wazao wa Yakobo wataweza kuishi namna gani? Wao ni wadogo sana! 6 Basi, Yawe akabadilisha nia yake, akasema: Hili vilevile halitatukia. Maono ya tatu: Timazi 7 Yawe alinionyesha tena maono mengine: Yawe alikuwa anasimama karibu na ukuta, akishika katika mukono wake uzi wenye timazi. 8 Naye akaniuliza: Amosi, unaona nini? Nikamujibu: Ninaona timazi. Kisha Yawe akasema: Ninaweka timazi kati ya watu wangu Waisraeli. Sitavumilia tena maovu yao. 9 Kule kwenye vilima ambapo wazao wa Isaka wanatambikia, kutafanywa kuwa uharibifu mutupu na mahekalu ya Waisraeli yatakuwa mabomoko. Nitaushambulia kwa vita ukoo wa mufalme Yeroboamu. Amosi na Amazia 10 Basi, Amazia kuhani wa muji wa Beteli, akamupelekea mufalme Yeroboamu wa Israeli habari hii: Amosi analeta fitina juu yako katika ufalme wa Israeli. Hotuba zake ni hatari kwa inchi hii. 11 Anachosema ni hiki: Yeroboamu atakufa kwa upanga nao Waisraeli watapelekwa katika uhamisho, mbali kabisa na inchi yao. 12 Kisha Amazia akamwambia Amosi: Sasa tumechoka nawe, ewe nabii! Uende! Urudie katika inchi ya Yuda, utoe unabii kule upate na chakula chako kulekule. 13 Usitoe tena unabii hapa katika Beteli, kwa sababu hapa ni pahali ya ibada ya mufalme; ni hekalu la utawala huu. 14 Amosi akamujibu Amazia: Mimi si nabii wa mushahara, wala si mumoja wa kikundi cha manabii. Mimi ni muchungaji na mulimaji wa miti ya mikuyu. 15 Yawe alinitosha katika kazi yangu hiyo ya uchungaji, akaniamuru nikuje kuwaambia watu wake wa Israeli unabii. 16 Nawe basi, ewe Amazia, sikiliza neno la Yawe: Wewe unaniambia nisitoe unabii juu ya Waisraeli, wala nisiseme neno lolote juu ya wazao wa Isaka. 17 Kwa hiyo, Yawe anasema hivi: Muke wako atakuwa kahaba katika muji, na wana wako na wabinti zako watauawa katika vita. Inchi yako itagawanywa na kupewa wengine, nawe mwenyewe utakufia katika inchi inayohesabiwa kuwa chafu; nao Waisraeli hakika watapelekwa katika uhamisho, mbali kabisa na inchi yao. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo