Amosi 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Azabu kwa sababu ya kujiaminia 1 Ole kwenu ninyi munaostarehe kule Sayuni, nanyi munaoishi katika usalama kwenye mulima Samaria! Ninyi munaonekana kuwa waongozi wa taifa kubwa, ambao Waisraeli wote wanawategemea. 2 Muende Kalne, muangalie. Tokea kule muende mpaka katika ule muji mukubwa wa Hamati, kisha mutelemuke mpaka Gati kwa Wafilistini. Mutatambua kwamba ninyi si bora kuliko falme zile, hata kama eneo lao ni ndogo zaidi ya lenu. 3 Ninyi munajaribu kuifukuza ile siku mbaya. Lakini munaukaribisha utawala wa mateso. 4 Ole kwenu ninyi munaolalia juu ya vitanda vya pembe za tembo na kujinyoosha juu ya matandiko yao, mukikula nyama za wana-kondoo na wana-ngombe! 5 Ninyi munapenda kuimba ovyo na sauti ya vinubi na kutunga ala mupya za muziki mukimwiga mufalme Daudi. 6 Munakunywa divai katika mabakuli, na kujipakaa marasi mazuri kabisa. Lakini hamuhuzuniki hata kidogo juu ya kuangamia kwa wazao wa Yosefu. 7 Kwa hiyo mutakuwa wa kwanza kwenda katika uhamisho, na karamu za wenye kustarehe zitatoweka. 8 Bwana wetu Yawe ameapa kwa nafsi yake: Ninachukizwa sana na kiburi cha wazao wa Yakobo; tena ninachukia nyumba zao nzuri sana. –Ni ujumbe wa Yawe.– Muji wao na vyote vinavyokuwa ndani yake nitavipatia waadui zake. 9 Kama wakibaki watu kumi katika nyumba moja, wote watakufa. 10 Na mujomba wa yule aliyekufa atakapokuja kuitoa maiti inje aichome, akimwuliza yeyote atakayekuwa ndani pembeni ya nyumba: Kuna mutu mwingine pamoja nawe? Atajibiwa: Hakuna! Naye atamwambia: Nyamaza kimya! Tusilitaje hata jina la Yawe. 11 Yawe anatoa amri, na nyumba kubwa inabomoka vipandevipande, na nyumba ndogo kusagikasagika. 12 Farasi wanaweza kukimbia katika mawe makubwa? Watu wanaweza kulima bahari na ngombe? Lakini ninyi mumeigeuza sheria kuwa sumu, na tunda la haki kuwa uchungu. 13 Ninyi munashangilia juu ya muji wa Bure na kusema mumeuteka muji wa Nguvu kwa nguvu zenu wenyewe. 14 Enyi Waisraeli, kweli nitaleta taifa moja likuje kuwashambulia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nalo litawatesa ninyi kuanzia Hamati upande wa kaskazini, mpaka kwenye kijito cha Araba, upande wa kusini. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo