Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

3 Yoane 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Salamu

1 Barua hii inatoka kwangu mimi muzee. Ninakuandikia wewe Gayo, mupendwa wangu, ninayekupenda hakika.

2 Mupendwa wangu, ninakutakia maendeleo mazuri katika kila jambo; ninakutakia afya njema katika mwili, kama vile unavyokuwa nayo katika roho.

3 Nilifurahi sana wakati wandugu wamoja walipofika na kunielezea juu ya ukweli unaokuwa ndani yako na kwamba unaishi katika ukweli.

4 Hakuna jambo linalonifurahisha kuliko lile la kusikia kwamba watoto wangu wanaishi katika ukweli.


Uaminifu wa Gayo

5 Mupendwa wangu, wewe ni mwaminifu kwa kazi unayofanya kwa ajili ya wandugu, hata kwa wale wanaokuwa wageni.

6 Wandugu hawa walishuhudia upendo wako mbele ya kanisa. Ninakusihi uwasaidie wapate kuendelea na safari yao kwa namna inavyomupendeza Mungu.

7 Kwa maana hawa walianza safari yao kwa ajili ya kazi ya Kristo bila kupokea musaada wowote toka kwa watu wasioamini.

8 Basi sisi tunapaswa kuwasaidia watu kama hawa tupate kushiriki pamoja nao katika kazi ya kutangaza ukweli.

9 Nimeandikia kanisa maneno machache lakini Diotrefe, anayependa kuwa musimamizi wao, anakataa kututii.

10 Kwa sababu hiyo wakati nitakapokuja, nitaonyesha wazi mambo yote anayotenda akitusingizia sisi maneno mabaya. Lakini hatosheki na mambo yale, yeye mwenyewe anakataa kukaribisha wandugu wale wanaokuwa katika safari. Na wale wanaotaka kuwakaribisha, anawakataza na kuwafukuza katika kanisa.

11 Mupendwa wangu, usifuate mufano mubaya, lakini ufuate mufano muzuri. Mutu anayetenda mema ni mutoto wa Mungu; lakini anayetenda mabaya hashirikiani na Mungu.

12 Watu wote wameshuhudia Demetrio vizuri; hakika ukweli wenyewe unahakikisha jambo lile. Sisi vilevile tunamushuhudia, nawe unajua kwamba ushuhuda wetu ni wa kweli.


Salamu za mwisho

13 Nina maneno mengi ya kukuambia lakini sitaki kuyaandika ndani ya barua.

14 Ninatumaini kwamba nitakuona sasa hivi na wakati ule tutasemezana pamoja uso kwa uso.

15 Ninakutakia amani. Warafiki zako wanakusalimia. Utusalimie warafiki zetu, kila mutu kwa upekee.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan