Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

2 Yoane 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Salamu

1 Barua hii inatoka kwangu mimi muzee. Ninakuandikia wewe mama uliyechaguliwa na Mungu, pamoja na watoto wako ninaowapenda hakika. Wala si mimi peke tu ninayewapenda, lakini vilevile wale wote wanaojua ule ukweli wanawapenda ninyi,

2 kwa sababu ukweli huu unakaa ndani yetu nao utakuwa pamoja nasi hata milele.

3 Mungu Baba pamoja na Yesu Kristo, Mwana wa Baba, watatujalia neema, huruma na amani katika ukweli na upendo.


Kuishi katika ukweli na upendo

4 Nilifurahi sana kuona kwamba wamoja kati ya watoto wako wanaishi katika ukweli kama vile Baba alivyotuamuru.

5 Na sasa Mama, ninakusihi: tupendane. Basi hii si amri mupya ninayokuandikia, lakini ni amri ile tuliyopokea tangu mwanzo.

6 Na upendo ni kuishi katika kutii amri za Mungu. Hii ndiyo ile amri muliyoisikia tangu mwanzo: muishi katika upendo.

7 Kwa maana wadanganyifu wengi wametokea katika dunia. Watu hawa hawakubali kwamba Yesu Kristo amekuja katika mwili wa kimutu. Yule asiyekubali vile ni mudanganyifu na mupinga Kristo.

8 Basi, mujiangalie wenyewe, kusudi musipoteze matunda ya kazi yenu, lakini mupokee zawadi kamili.

9 Kila mutu atakayeenda mbali na asiyedumu katika mafundisho ya Kristo, mutu yule hashirikiani na Mungu. Lakini yule anayedumu katika mafundisho yale, anashirikiana na Baba na Mwana vilevile.

10 Mutu akikuja kwenu, naye asipowafundisha mafundisho haya, musimukaribishe ndani ya nyumba yenu, wala musimusalimie;

11 maana mwenye kumusalimia anashirikiana naye katika matendo yake mabaya.


Salamu za mwisho

12 Nina maneno mengi ya kuwaambia, lakini sitaki kuyaandika ndani ya barua. Ninatumaini nitawatembelea na kusemezana pamoja nanyi uso kwa uso, kusudi tupate kujazwa na furaha kabisa.

13 Upokee salamu za watoto wa dada yako aliyechaguliwa na Mungu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan